|
Amirul-Muuminina;
Aliy-Allah amuwiye radhi-alipo maliza suala la Khawaariji,
akawaamrisha wafuasi wake kwenda Shamu kupigana na Muawiya na
washirika wake. Wakamwambia: Ewe Amirul-Muuminina! Hakika tumeishiwa
zana za vita, mishale imetuishia, panga zetu na mikuki yetu imekuwa
butu. Basi hebu na turudi mjini kwetu ili tufanye maandalizi.
Maneno
yao haya, yanafahamisha kwamba watu wale tayari wamesha vunjika moyo
na wamekimwa na vita. Ikiwa hiyo ndio hali ya jeshi, basi usije
kushangaa hali iliyo mpata Amirul-Muuminina Aliy bin Abi Twaalib.
Nguvu zake zikaanza kupungua kila siku, naye kila muda akiutumia
ufasaha wake alio pewa na Allah kuwahimiza na kuwatia mori wa
kuipigania dini. Lakini wapi, yote hayo hayakuwazidishia ila ulegevu,
ni wachache tu miongoni mwao ndio walio mtakashia kauli na maneno.
Kutokana na hali hiyo, Khawaariji wakapata nguvu na hoja yao waliyo
iunda nayo si nyingine ila kwamba yeye amehukumiana na watu katika
dini ya Allah na ilhali hapana hukumu ila ya Allah tu.
Na
akawa katika jumla ya walio muasi Imamu, ni Al-Khiriit bin Raashid
An-naahiy na kundi la watu mia tatu la ukoo wa Naahiya, akamuendea
Imamu Aliy, akamwambia: Ewe Aliy! Wallah, sitaitii amri yako na wala
sitaswali nyuma yako na hakika mimi nitajitenga nawe kesho. Imamu
akamwambia: Kwa kufanya hivyo utakuwa umemuasi Mola wako Mlezi na
utakuwa umeitangua ahadi yako. Na (kwa kufanya kwako hivyo) hauidhuru
ila nafsi yako. Hebu niambie, kwa nini unafanya hivyo? Akajibu: Ni
kwa sababu wewe umefanya “tahkiimu” na wale watu na umeinyongesha
haki na umeegemea upande wa madhaalimu. Ni kwa ajili hiyo basi, mimi
ninajitenga nawe na wao ni mwenye kuwalipia kisasi. Sayyidna Aliy
akamwambia: Njoo nikusomeshe kitabu cha Allah na nifanye nawe mdahalo
katika Sunna. Na nikupe ufunguzi wa mambo ambayo mimi ninayajua sana
kuliko wewe. Basi huenda wewe ukayajua hivi sasa haya unayo yapinga.
Akasema: Mimi ninakupa ahadi. Imamu akamwambia: Shetani asikughuri na
wala wasikupaparishe watu majaahili. Wallah, ukitaka maongozi yangu
na ukayakubali, bila ya shaka nitakuongozea kwenye njia ya uwongofu.
Lakini wapi, Al-Khiriit hakuyasikia maneno mazuri hayo, huyo
akaelekea upande wa Nafar na kundi lake.
Akamtuma
Ziyaad bin Hafsah Al-Bakriy kuwafuatia na akamwambia: Nenda mpaka
ufike kwenye maboma ya Abu Mousa, usubiri amri yangu hapo. Ziyaad
akaenda mpaka akafika kwenye maboma ya Abu Mousa. Baada ya kuondoka
kwake, Qurdhwah bin Ka’ab Al-Answaariy akamtumia ujumbe Imamu Aliy,
akimwambia ya kwamba wafuasi wa Al-Khiriit wamemuua mmojawapo wa
machifu ambaye alikuwa amesilimu. Kufuatia khabari hiyo, Sayyidna
Aliy akampelekea ujumbe Ziyaad ya kwamba awafuatilie na awatake
wamtoe mtu aliye muua mtemi muislamu. Akisha mtia mkononi, amrejeshe
kwake na iwapo watakataa, apambane nao.
Ziyaad
akaipokea amri ya Amirul-Muuminina, akawafuatilia mpaka akawakuta
nyanda za juu, Ziyaad akamwambia Al-Khiriit: Ni lipi lililo kufanya
uwe na kinyongo kwa Amirul-Muuminina na kwetu sisi, mpaka ukajitenga
nasi? Akajibu: Mimi sijamridhia mtu wenu huyo kuwa Imamu (kiongozi)
na wala sikuuridhia mwenendo wenu kuwa ndio mwenendo wa kufuatwa. Kwa
minajili hiyo basi, nikaona bora nijitenge na nijiunge na lile kundi
litoalo wito wa shura. Ziyaad akamuuliza: Hivi kweli watu wanaweza
kukusanyika kwa mtu anaye lingana na mtu wako huyu uliye jitenga
naye, kwa kumjua Allah, kanuni zake na kitabu chake. Pamoja na udugu
wake na Mtume wa Allah na utangu wake katika Uislamu?
Al-Khiriit akasema: Mimi sisemi hapana katika yote hayo. Ziyaad
akamuuliza: Ikiwa hivyo ndivyo, basi ni kwa lipi umemuua muislamu
uliye muua? Akajibu: Sikumuua mimi, lakini ameuawa na kundi la
wafuasi wangu. Akamwambia: Basi wasalimishe (hao wauaji) kwangu.
Akasema: Mimi sina njia ya kulifanya hilo. Kwa kukataa kwake
kuwasalimisha wauaji ili wachukuliwe kisasi, kamanda Ziyaad
akalazimika kupambana nao. Akapambana nao mpaka usiku, wakazidiwa
nguvu na kiongozi wao Al-Khiriit akakimbia.
Ziyaad
alipo uona utimua mbio huo, na kusambaratika kwa genge la waasi hao,
akaamua kurejea Basrah ili kuwaganga majeruhi alio nao. Na akamtumia
Imamu Aliy taarifa ya kazi aliyo mtuma na namna mambo yalivyo jiri.
Kisha ndipo akamtuma Ma’aqal bin Qays Ar-riyaahiy kukiongoza kikosi
cha askari elfu mbili, kwenda kupambana na Khawaariji. Na
akamwandikia waraka Ibn Abbas aliyeko Basrah, amuongezee nguvu kwa
kikosi cha watu elfu mbili cha wenyeji wa Basrah, kiongozwe na mtu
mwenye weledi wa vita. Ma’aqal akasonga mbele na ikaungana nae ile
nguvu ya wazalendo wa Basrah, wakawakuta Khawaariji karibu ya
mojawapo ya majabali ya Raamahurmuz. Wakaingia mapambanoni nao mpaka
wakauawa katika watu wa Ma’aqal kiasi cha askari sabini, Al-Khiriit
na baadhi ya wafuasi wake wakazidiwa nguvu, wakatimua mbio tena.
Amirul-Muuminina; Sayyidna Aliy-Allah amuwiye radhi-akamuamrisha
kamanda Ma’aqal awafuatilie mpaka awasage wote na kuukata mzizi wa
fitina. Kamanda Ma’aqal akaipokea amri hiyo, haraka akawafuatilia,
akawaangushia kisago kikali mpaka akawafyeka wote na akamuua na
kiongozi wao Al-Khiriit.
Baada
ya hapo, likafumuka wimbi la uasi dhidi ya Amirul-Muuminina; Sayyidna
Aliy, yakaasi makundi mengi ya Khawaariji. Kila alipo jaribu kuuzima
moto wa fitina wa kundi moja, ndipo lilipo ibuka kundi jingine.
Ama
tukirejea kwa upande wa Muawiyah, yeye tangu alipo pewa kiapo cha
utii cha ukhalifa, mambo yalimuendea vema huko Shamu. Na watu wake
wakawa ni jeshi la kupigiwa mfano katika utii kwa kiongozi wao.
Kutokana na unyoofu huo wa hali na mambo, akaona sasa ni fursa yake
ya kuwakusanya Waislamu wote chini ya utii wake, kama alivyo kuwa
akitaka kufanya hivyo Amirul-Muuminina; Sayyidna Aliy-Allah amuwiye
radhi. Katika kuitekeleza kivitendo fikra yake hii, akaamua kumtuma
balozi wake Misri; Amrou bin Al-Aaswi. Na khabari ya Misri ilikuwa
kwamba Imamu Aliy alikwisha pata kiapo cha utii kutoka kwa watu wa
huko. Alimtuma huko Qays bin Sa’ad bin Ubaadah, kama tulivyo
tangulia kueleza. Balozi huyu wa Imamu kwa watu wa Misri, alipo fika
huko wengi wa watu wa Misri walimkubali Sayyidna Aliy na wakambai.
Isipo kuwa kundi dogo miongoni mwao, ambalo lilijitenga katika sehemu
ya “Kharabtaa”, likiongozwa na Yazid bin Al-Haarith Al-Mudlajiy.
Kundi hili lilishikilia na kuyatumia mauaji ya Sayyidna Uthman,
kufanya uasi dhidi ya Amirul-Muuminina na kuitumia fursa hiyo kupata
waunga mkono. Akajiunga na kundi asi hili, Maslamah bin Mukhallad,
gavana Qays yeye akajizuia kujiunga nalo, kwa kujua kwamba hilo si
kundi hatari. Imamu Aliy alipo lifahamu hilo, akamuandikia Qays
waraka amrishi/elekezi, akimuamrisha kuwapiga vita waasi hao, kwa
kuuzingatia msingi usemao “Chanzo cha moto mkubwa, ni cheche
ndogo”. Qays akamuandikia Imamu Aliy waraka rejezi: (Ama
baad...Ninakushangaa, unaniamuru kuwapiga vita watu ambao wamejizuia
kukufanyia uadui na ambao wanashughulika na adui yako! Na tutakapo
waghadhibisha, watamsaidia adui yako dhidi yako. Basi nakuomba
unitii, ewe Amirul-Muuminina na uachane nao. Kwani fikra sahihi ni
kuwaacha. Wassalaamu).
Kufuatia
kuikaidi kwake amri halali ya Amirul-Muuminina, Sayyidna Aliy
akamuuzulu katika kiti cha ugavana wa Misri na akamtawaza mahala pake
Muhammad bin Abubakar As-siddiq. Gavana mteule; Muhammad alipo fika
Misri, akasema: (Kila sifa za jinsi kamali ni stahiki yake Allah,
ambaye ametuongoza sisi na nyinyi katika ile haki waliyo khitalafiana
kwayo watu. Na ambaye ametuonyesha sisi nanyi yale ambayo wamepatwa
upofu nayo watu majaahili. Ehee fahamuni ya kwamba Amirul-Muuminina
amenitawalisha uongozi wenu na ameniusia mliyo yasikia. Na sipati
kuwezeshwa haya ila na Allah, kwake Yeye ninategemea, na kwake Yeye
naelekea. Basi mkiona katika uongozi wangu na kazi zangu utii,
muhimidini Allah kwa hayo kwani hakika Yeye ndiye Muongozi. Na iwapo
mtamuona mtendaji wangu yeyote hakutenda haki, basi leteni mashitaka
kwangu na mnilaumu kwa sababu yake. Kwani mimi nitafurahi sana ikiwa
mtafanya hivyo, nanyi mnastahiki kufanya hivyo. Allah atuwezeshe sisi
nanyi kutenda matendo mema kwa rehema zake). Alipo maliza khutba yake
akashuka mimbarini.
Na
baada ya mwezi mmoja tangu kuwasili kwake Misri, akawatumia ujumbe
watu wale walio jitenga huko Kharabtaa, akiwapa khiyari ya ama kumtii
Amiri au kuondoka Misri. Wakamjibu sisi hatuyafanyi yote hayo, hebu
tuache tuangalie suala letu litakuwaje, usifanye haraka kutupiga
vita. Gavana mteule akawakatalia hilo. Nao wakajitia ngomeni na kuwa
katika hali ya tahadhari na gavana Muhammad. Ilipo patikana tahkiimu,
wakawa na tamaa nayo na wakamtupia maneno ya kejeli. Kufuatia
uchokozi huu gavana akaamua kuchukua hatua, akawapelekea kikosi
kuwapiga, waasi wale wakakizidi nguvu kikosi cha gavana Muhammad na
wakamuua kiongozi wake. Akatuma kikosi kingine, nacho pia akauwa
kiongozi wake. Kisha akatoka Muawiya bin Khudeiji As-sakuuniy akitaka
kisasi cha damu ya Sayyidna Uthman. Amirul-Muuminina; Sayyidna
Aliy-Allah amuwiye radhi-alipo pata khabari hiyo, akaona hali ya
Misri imesha kuwa tete na kwamba Muhammad hawezi kupambana. Ndipo
akafikia uamuzi wa kumuengua na nafasi yake ikashikwa na Al-Ashtar
bin Al-Haarith An-nakh’iy. Na akamuandikia usia ambao alikusanya
ndani yake siasa ya Dunia na utengevu wa Akhera. Kwa bahati mbaya,
gavana huyu mpya akafa akiwa njiani kuelekea Misri kukalia kiti cha
ugavana. Muhammad bin Abubakar kukamuwia uzito kuuzuliwa kwake,
kufuatia hali hiyo Imamu Aliy akamuandikia waraka:
(Ama
baad...Hakika imenifikia khabari ya kughadhibika kwako kutokana na
kumteua kwangu Al-Ashtar kushika nafasi yako. Nami sikulifanya hilo
ila ni kwa ajili ya kuongeza jitihada zako kwangu, lau kitakuponyoka
kilichoko mkononi mwako, nitakutawalisha kilicho chepesi kwako na
kinacho pendeza mno kwako. Hakika huyo mtu ambaye nilikuwa
nimemtawalisha uongozi wa Misri, alikuwa ni mtu mwenye nasaha kwetu
na ni mwenye nguvu kwa adui yetu. Naye amekwisha zikamilisha siku
zake za kuishi na amekutana na mauti yake hali ya kuwa sisi tu radhi
naye, basi tunamuomba Allah naye amuwiye radhi na amrudufishie
thawabu.
Msubirie
adui yako na uvipanyie vita na ulinganie kuelekea kwenye njia ya Mola
wako Mlezi, kwa hekima na mawaidha mema. Na kithirisha kumdhukuru
Allah na kumuomba msaada, na umkhofu naye atakutoshea na ya
kutatizayo na atakuauni {atakusaidia} katika utawala wako).
Muhammad
naye akamuandikia Amirul-Muuminina kumjibu waraka wake: (Ama baad ...
Nimeupokea na kuufahamu waraka wako na hapana yeyote katika watu
anaye iridhia mno rai ya Amirul-Muuminina, wala mwenye kumtaabisha
mno adui yake, wala mwenye huruma mno kwa mtawalishwa wake, kuliko
mimi. Nami nimekwisha toka na kupiga kambi na nimewapa amani watu
wote ila wale walio tuwashia moto wa vita na kutukhalifu. Nami
ninaifuata amri ya Amirul-Muuminina na ninailinda. Wassalaamu).
|