|
|
|
|
|
| Majibu
: Swali na 1 |
|
|
|
|
|
Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kutuwafikisha
kukuletea majibu ya maswali yako na tunamtakia
Rehma na Amani Mtume wetu Muhammad pamoja na
jamaa na mashaba wake.
1. Tuelewe kwanza kabisa kuwa Mbwa ni najisi kwa
maneno ya wanazuoni walio wengi. Wanaosema kuwa
mbwa ni najisi wametegemea hadithi iliyopokewa
toka kwa Mtume -Rehema na Amani zimshukie- kuwa
alialikwa katika nyumba, akakataa kwenda
alipoulizwa alijibu “Katika nyumba ya fulani
kuna mbwa” akaambiwa : na katika nyumba ya
fulani kuna paka, akasema Mtume “Hakika paka
si najisi”. Maneno haya yanajulisha wazi kuwa
mbwa ni najisi. Pia wanategemea hadithi
iliyopokewa na Abu Hurairah toka kwa Mtume -Rehema
na Amani zimshukie- “Anapoingiza (kinywa chake)
katika chombo cha mmoja wenu basi na amwage (kilichomo)
na aoshe chombo chake mara saba mojawapo (achanganye)
na mchanga” Muslim. Amesema Imaam Malik ambaye
ameiona hadithi hii lakini anasema Mbwa sio
najisi, na kusafisha huku ni kwa ajili ya ibada
tu. Ifahamike pia kuwa kuna hadithi iliyopokewa
na Abdullah bin Omar – Allah awawie radhi-
kuwa mbwa walikuwa wanapita (kwenda na kurejea)
msikitini zama za Mtume wa Mwenyezi Mungu -Rehema
na Amani zimshukie- wala hawakuwa (masahaba)
wakimwagia kitu mahali alipopita.Bukhaariy. Pia
wametegemea aya ya nne katika suratil Maidah
“NA KULENI WALICHOKUSHIKIENI (mbwa)” Dalili
yao ni kuwa Mwenyezi Mungu hakuamrisha kuosha
kilichoshikwa na mbwa hao. Kwa hivyo ndugu yangu
mbwa ni najisi kwa maneno ya wanazuoni waliokuwa
wengi, hata hivyo ukiwa na mtihani wa kuwa na
mbwa wa ulinzi nyumbani basi unaweza ukategemea
maneno ya wanazuoni wanaosema si najisi kama
Imaam Malik. Ama ikiwa unafuga kwa mchezo tu
(hobby) basi ukumbuke hadithi ya Mtume -Rehema
na Amani zimshukie- isemayo “Malaika hawaingii
kwenye nyumba yenye mbwa”
2. Suala la kupangusa juu ya soksi : ni jambo la
kustaajabisha kuwa kuwa kuna watu wanaopangusa
juu ya soksi, tungependa kujua khabari zao.
Kuhusu suala lako, tunaamini kuwa unafahamu wazi
kuwa Mtume -Rehema na Amani zimshukie-
alipangusa juu ya KHOFU na hukmu yake itakuja
kwenye Fiqhi, kwa ufupi ni kama viatu vya ngozi
au mfano wake vyenye kufunika hadi kwenye
vifundo, na hutumiwa sana kwenye sehemu za
baridi kama uturuki. Miongoni mwa shuruti zake
ni kuwezekana kuzitembelea juu yake,
zisizoingiza maji ila penye kiungio, zimewekwa
juu ya tahara na hazina najisi. Hadithi ya khofu
imepokewa na Bukhariy na Muslim. Ama kupangusa
juu ya soksi, kuna hadithi iliyopokewa na
Mughira kuwa Mtume -Rehema na Amani zimshukie-
alipangusa juu ya soksi zake na viatu vyake.
Hadithi hii imepokewa na Tirmidhiy, lakini ni
dhaifu kama alivyobainisha hayo wanazuoni wengi
miongoni mwao akiwa Imaam Nawawiy kwenye kitabu
chake Majmuu, Juzuu ya kwanza. Yeye ameeleza
kwamba ameidhoofisha hadithi maimamu wa hadithi
kama Imaam Ahmad bin Hanbal, Muslim, Sufyanu
Thawriy, Yahya bin Muin Aliy bin Almadiniy na
wengineo.
3. Kuswali na viatu inafaa, Mtume -Rehema na
Amani zimshukie- aliswali na viatu kama
ilivyopokewa kwenye Hadithi ya Bukhariy na
Muslim. Imepokewa pia kuwa aliwahi kuvua viatu
ndani ya swala na kuwaambia masahaba kuwa Jibril
alimwambia kuwa viatu vyake vina najisi. Kwa
hivyo kuswali ndani ya viatu inafaa kama viatu
havina najisi. Lakini, tuiangalie misikiti yetu
na misikiti ya wakati wa Mtume -Rehema na Amani
zimshukie- Misikiti ina mazulia na msikiti wa
Mtume -Rehema na Amani zimshukie- ulikuwa wa
udongo bila hata busati tusije kuanza kuzua vitu
vipya ndani ya misikiti yetu, ikiwa sisi
hatutaki mgeni kuingia nyumbani mwetu na viatu
kwa kuwa sitting room zetu zina mazulia na
ataichafua, vipi kuhusu nyumba za Mwenyezi
Mungu, hizo ni haki zaidi kuziheshimu.
|
|
|
|
|
|
|
| |
|
|
Forum | Guestbook | Tuandikie |
| |
|