Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Dini ni nasaha, wakauliza kwa nani ? Akasema Mtume : Kwa Allah, Mtume wake, kwa viongozi wa waislamu na watu wa kawaida" Hadith Tukufu

3. KUTHIBITI ZINAA KWA KUDHIHIRI MIMBA NJE YA NDOA

Faida

Mafaqihi (wanazuoni wa sheria ya Kiislamu) wamekhitilafiana katika kadhia ya mwanamke kuwa na mimba bila ya mume. Je, anawiwa na ‘hadda’?, wamekhitilafiana kwa kauli mbili:-

KAULI YA KWANZA:

Itakapodhihiri mimba kwa mwanamke asiye na mume, mimba hii haimpasishii ‘haddi’. Lakini ataulizwa, akidai kuwa alibakwa bila ya khiari yake au aliingiliwa katika mazingira ya ‘shubuha’. Au hakukiri kuzini, katika hali na mazingira haya hapasiwi na ‘haddi’. Haya ndio madhehebu ya maimamu; Shaafiy, Abu Haniyfah na Ahmad Ibn Hambal-Allah awarehemu. Rejea kitabu [AL-MUGHNIY pamoja na SHEREHE yake cha Ibn Qudaamah Al-Maqdisiy 10/192]

 

DALILI/USHAHIDI WA KAULI HII:

Maimamu walioisimamia kauli hii katika madhehebu ya Hambal, Shaafiy na Hanafiy wameyafanya kuwa dalili yao majumuisho ya Ibn Qudaamah Al-Maqdisy katika kadhia hii pale aliposema: “Na kwetu sisi kwa hali ilivyo inamkinika kuwa mimba hiyo inatokana na kuingiliwa kwa kubakwa au kwa shubuha. Na hali ilivyo ni kupomoka haddi kwa matendo ya shubuha. Na imekwishasemwa kwamba mwanamke anaweza kushika mimba bila ya kuingiliwa kimwili. Na hili hupatikana kwa kuingia mbegu za kiume (manii) ukeni kwake ima kwa kitendo chake mwenyewe akajiingizia au kwa kitendo cha mtu mwingine kama daktari na kadhalika. Hii ndio picha inayoweza kuchorwa kwa ujauzito wa mwanamwali; bikira na hili limewahi kutokea.

Ama maswahaba wa Mtume-Rehema na Amani zimshukie-riwaya zilizopokewa kwao zimekhitilafiana. Said amepokea: “Alituhadithia” Khalf Ibn Khaliyfah “Ametuhadithia” Haashim: “Kwamba mwanamke fulani alipelekwa mbele ya (Amirul-Muuminina) Umar Ibn Al-Khatwab akiwa na mimba bila ya mume. Umar akamuuliza (nae) akajibu: Mimi ni mwanamke mwenye kichwa kizito (obtuse), niliingiliwa na mwanamume fulani nikiwa nimelala. Basi sikuamka ila baada ya yeye kukidhi matamanio yake, (kwa utetezi wake huu) Umar akamuondoshea adhabu”.

Na Al-Baraai Ibn Swabrah akapokea kutoka kwa Umar: “Kwamba aliletwa mwanamke mjamzito, akadai kuwa alibakwa, (Umar) akasema: Muachieni njia yake (aende huru)”. Na akawaandikia maamirijeshi ya kwamba asiuliwe mtu ye yote ila kwa idhini yake.

Na imepokewa kutoka kwa Sayyidina Ibn Abbas na Aliy-kwamba wao wamesema: “Yatakapokuwepo katika (kadhia ya) haddi maneno ‘huenda’ na ‘pengine’, basi (haddi) ni yenye kuzuiliwa (kutekelezwa)”.

Na imepokewa na Daaruqutwniy kwa isnadi yake kutoka kwa Abdillah Ibn Masoud na Muaadh Ibn Jabal na Uqbah Ibn Aamir kwamba wao wamesema: “(Suala la) haddi litakapokutatiza, basi iepushe kiasi uwezacho”.  Na wala hapana makindano kuwa haddi huepushwa au huzuiwa kwa matendo ya shubuha na hili limethibiti hapa”. Zimekoma dalili za Ibn Qudaamah, rejea kitabu [AL-MUGHNIY pamoja na SHEREHE yake cha Ibn Qudaamah Al-Maqdisiy 10/192-194]

 

KAULI YA PILI:

Mwanamke atakapoonekana na ujauzito bila ya kuwa na mume, atalazimikiwa haddi kwa sababu ya mimba hiyo. Wala madai yake ya kubakwa hayatakubaliwa ikiwa hayakuambatana na ushahidi wa kulithibitisha hilo. Ama akileta ushahidi unaozingatiwa mbele ye sheria, basi hatapasiwa na haddi. Ushahidi huu ni kama vile mwanamke kuja huku akitokwa na damu nae akipiga mayowe ya kuomba msaada. Au akaja akiwa kamkwida mbakaji wake huyo, haya ndio madhehebu ya Imamu Maalik-Allah amrehemu. Rejea SHEREHE ya Al-Kharsiy juu ya MUKHTASWAR KHALIYL-5/333.

 

DALILI/USHAHIDI WA KAULI HII YA PILI:

Watu waliosimamia kauli hii ambao ni wafuasi wa madhehebu ya Imamu Maalik wametoa ushahidi kwa riwaya iliyotolewa na Imamu Bukhaariy kutokana na kauli ya Sayyidina Umar, pale aliposema: “Na kupopolewa kwa mawe ni wajibu kwa kila ambaye amezini miongoni mwa wanawake na wanaume atakapokuwa ni muhswani (mwenye ngome). (Hivyo ni iwapo) utapatikana ushahidi, au ikadhiri mimba au akakiri”. Angalia rejea iliyotajwa hapo juu.

 

 


Forum | Guestbook | Tuandikie |