|
Ni
jambo lisilo na shaka kwamba suala la kutoa ushahidi wa kutendeka kwa
kosa/hatia ya zinaa ni suala linalohusu kuthibitisha jinai ya kimaumbile
inayomgusa moja kwa moja mtendaji wa jinai hiyo. Jinai inayomfedhehesha
muhusika mbele ya macho ya jamii ukiachilia mbali adhabu kali sana inayoambatana na jinai hiyo. Ni kwa mantiki
hii, ndio sheria ikawa makini na kutia mkazo wa haja katika kuweka njia za
kuithibitisha jinai hii ambayo inaweza kuyagharimu maisha ya atakayetiwa
hatiani. Ni kwa ajili hii jinai/hatia hii ya zinaa ikakhusishwa na
mashahidi wanne watakaoshuhudia juu ya dhati ya kitendo cha zinaa, yaani
kitendo chenyewe khasa na si vinginevyo. Sheria imelenga katika kuweka
mazingira haya magumu ya kupatikana ushahidi wa kuthibitisha kosa la
zinaa, kuweka pazia la sitara na kumuondoshea aibu na fedheha mzinifu na
jamaa zake. Na Allah Mtukufu anapenda kuwasitiri waja wake na
amelipondokesha hilo kwa waja wake pia, kuwa na wao wapende mno kusitiri
kuliko kufedhehesha. Na hii ndio mojawapo ya falsafa ya kauli za Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie: “Atakayemsitiri muislamu, Allah
atamsitiri duniani na akhera”. Rejea kitabu [AT-TARGHIYBU
WAT-TARHIYBU].
Kama
ambavyo Allah alivyokemea uenezaji wa uchafu/uovu kwa jamii: “KWA YAKINI
WALE WANAOPENDA UENEE UOVU KWA WALE WALIOAMINI, WATAPATA ADHABU IUMIZAYO
KATIKA DUNIA NA AKHERA, NA ALLAH NDIYE ANAYEJUA (ya maslaha yenu) NA
NYINYI HAMJUI”. [24:19]
Kwa
hivyo basi, ili kuthibitisha maana ya sitara aliyoipendelea Allah na Mtume
wake, ndipo ikashurutizwa ziada ya idadi ya mashahidi kinyume na ushahidi
wa makosa mengine. Na katika kushurutizwa ushahidi wa watu wanne ni
kuthibitisha maana ya sitara, kwa sababu watu wanne kujua na kushuhudia
uchafu huu wa zinaa ukitendeka ni suala la nadra mno kuweza kupatikana. Na
kanuni zinasema kwamba kila jambo zinapokithiri sharti zake, jambo hilo
huwa kuchache mno kutokea kwake. Kwa sababu kupatikana kwake
kutakaposimama juu ya ushahidi wa mashahidi wanne, hakuwezi kuwa kama
itakavyokuwa kupatikana kwake kutakaposimama juu ya ushahidi wa mashahidi
wawili. Kwa hali na mazingira haya, inathibiti ile maana ya sitara
iliyopendekezwa na sheria. Kisha itakapokuwa sitara imependelewa na
sheria, basi kushuhudia zinaa itakuwa ni kinyume cha ilivyo bora
(khilaful-aula) ambayo marejeo yake ni katika karaha ielekeayo kwenye
uharamu (karahatut-tanziyhi). Na vile vile kwa kuwa sitara ndilo jambo
lililopendekezwa, basi kueneza khabari ya uovu kunakuwa ni jambo lenye
kuchukiza na kulaumiwa.
Ni
vema ikaeleweka kwamba sitara hii ni wajibu iwe kwa mtu ambaye hakuzini
kwa makusudi na wala hakuifichua dhambi hiyo mbele ya kadamnasi kwa
kujinadi na kujinasibu. Ama atakapofikia hatua ya kuivunja mwenyewe sitara
aliyositiriwa na Mola wake, akaifichua na kuieneza khabari ya uchafu na
uovu wake huo kiasi cha kujigamba na kujifakharisha. Mtu kama huyu kutoa
ushahidi dhidi yake kunakuwa ni wajibu na bora zaidi kuliko kuacha kuutoa.
Hivi ni kwa sababu matakwa na shabaha ya sheria ni kuisafisha na kuitakasa
ardhi kutokana na maasi na maovu, kwani imepokelewa kwamba Bwana
Mtume-Rehema na Amani zimshukie-amesema: “Enyi watu,
umekwishakufikieni wakati wa kukomeka na mipaka ya Allah (aliyokuwekeeni
msiivuke). Basi ye yote atakayekiingia cho chote miongoni mwa taka
(madhambi) hizi, basi na ajisitiri kwa sitara ya Allah. Kwani hali ilivyo,
ye yote atakayetufunulia dhambi/kosa lake (alilolitenda sirini)
tutamsimamishia hukumu ya kitabu cha Allah Mtukufu”. Imamu Maalik
(Muwatwaa)-Allah amrehemu.
Na
Imamu Shaafiy-Allah amuwiye radhi-akasema: “Nasi tunapenda mtu
aliyesibu ‘haddi’ (kosa linalompasishia adhabu kwa mujibu wa sheria)
ajisitiri. Na amche Allah Mtukufu na wala asirudie tena kufanya maasia
hayo kwani kwa yakini Allah huwakubalia (huwapokelea) toba waja wake”.
Rejea kitabu (AL-UMMU).
Imepokelewa
kutoka kwa Anas Ibn Maalik-Allah amuwiye radhi-amesema: Nilikuwa kwa
Mtume-Rehema na Amani zimshukie-mara akajiwa na mtu fulani akasema: Ewe
Mtume wa Allah, mimi nimetenda kosa linipasishialo adhabu (haddi), basi
nisimamishie adhabu. Akasema (Anas): Mtume hakumuuliza juu ya kosa
hilo. Akasema: Ukaingia wakati wa swala, (mtu yule) akaswali
pamoja na Mtume. Mtume alipomaliza kuswali, mtu yule akamuinukia
(akamuendea) na kumwambia: Ewe Mtume wa Allah, hakika mimi nimetenda kosa
linipasishialo adhabu, basi ninakuomba unisimamishie hukumu ya kitabu cha
Allah. Mtume akamwambia: “Kwani wewe hukuswali pamoja nasi?”
akajibu: Naam, (nimeswali), Mtume akamwambia: “Basi bila ya shaka
Allah amekwisha kusamehe dhambi yako”. Bukhaariy-Allah amrehemu.
Ibn
Hajar-Allah amrehemu-amesema: “Na hakika si vinginevyo, Bwana Mtume
hakumtaka ufafanuzi wa kosa. Ima ni kwa sababu hilo linaingia katika
mlango wa kupeleleza khabari za watu kulikokatazwa. Na ama ni kwa
kupendelea zaidi kusitiri maovu na akaona kwamba kule kutaka kwake
kusimamishiwa adhabu tayari ni majuto na kurejea (kwa Mola wake). Na ndio
wanazuoni wakapendelea kumfundisha mtu aliyekiri kutenda jambo
linalompasishia adhabu kutengua ikrari yake. Afanye hivyo kwa njia ya
kuambaambaa au kwa njia ya wazi moja kwa moja ili ajiondolee adhabu
(inayomkabili)”. Rejea kitabu (FAT-HUL-BAARIY) cha Ibn Hajar
Al-asqalaaniy (12/122) na (AL-BAHRUR-RAAIQ) cha Ibn Najiym Al-hanafiy
(5/8)-Allah awarehemu.
C/.
MAUDHUI YA MANENO YA KUTHIBITISHA USHAHIDI MBELE YA KADHI (TESTIMONY) NA
MADHUMUNI YAKE.
Ili
kuthibitisha jinai ya zinaa kwa ushahidi unaotolewa mbele ya kadhi
(testimony) na ili ushahidi huo ukubaliwe kisheria. Hapana budi washuhudie
mashahidi wanne juu ya kuona kwa macho yao dhati ya kitendo cha zinaa
baina ya mwanamume na mwanamke. Washuhudie kwamba wao wameiona tupu (ala)
ya mwanamume imeingia ndani ya tupu ya mwanamke mithili ya kijiti cha
wanja kiingiavyo ndani ya kichupa cha wanja. Tena washuhudie kuona kitendo
hicho kwa wakati mmoja na muono mmoja; wote kwa pamoja. Kadhi awadodose
mpaka wathibitishe kwamba hakika wao wameiona kwa macho yao ile ya
mwanamume ikiingia katika ile ya mwanamke uingiaji wa kijiti cha wanja
ndani ya kichupa cha wanja. Kisha kadhi awaulize mashahidi hao:-
ü
Zinaa
ni nini.
ü
Zinaa
huwaje; yaani zinaa hupatikanaje.
ü
Walishuhudia
ikitendeka wapi na wakati gani.
ü
Mwanamume
amezini na mwanamke yupi.
Haya
yote ni kwa sababu Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-alimuhoji sana
swahaba wake Maaiz juu ya hilo na akamwambia: “Mpaka hiyo yako
ikaingia ndani ya ile yake?” Akajibu: Naam, (Mtume) akamuuliza
(tena): “Kama kizamavyo kijiti cha wanja ndani ya kichupa cha wanja
na mithili ya kamba iingiavyo ndani ya kisima?” Akajibu: Naam,
(Mtume) akamuuliza (tena): “Je, unatambua zinaa ni nini?” Akajibu:
Naam, nimemuendea kwa njia ya haramu (zinaa) kama ambavyo mume amuendeavyo
mkewe kwa njia ya halali (ndoa). (Mtume) akamuuliza (tena): “Unataka/unakusudia
nini kwa kauli yako hii?” Akasema: (Ninakusudia) unitwaharishe”.
Sasa
basi, kama ambavyo kadhi anavyowajibikiwa kumuhoji mtu aliyekiri mwenyewe
ili kuithibitisha ikrari yake. Ni hivyo hivyo anao wajibu wa kisheria
kuwahoji mashahidi ili kuuthibitisha ushahidi wao.
TAFSIRI/UFAFANUZI
WA MASWALI YAULIZWAYO.
Ama
lengo la kuwauliza zinaa ni nini, ni kwa sababu ya kuwepo imkani ya
kumaanisha kitendo kingine kisichohusisha tupu (uchi). Swali liulizalo
zinaa ilikuwaje/ilitendeka vipi, ni kwa sababu ya kuwepo imkani ya
kutendeka kwa nguvu; bila ya ridhaa au tupu ziligusana pasina dhakari
kuingia ndani ya uke. Zinaa ilitendeka wapi, swali hili linakuja kwa
sababu yamkinika kitendo alichokishuhudia shahidi huyu sicho
alichokishuhudia shahidi yule. Sasa basi wanaulizwa mahala ili kuoanisha
ushahidi wao. Swali liulizalo zinaa ilitendeka lini, ni kwa sababu
yamkinika kuwa tendo lilitendeka zamani, ujanani mwake au katika hali ya
uwendawazimu. Alizini/amezini na nani, kwa sababu yamkinika mwanamke huyo
kuwa ni mkewe ambaye mashahidi hawa hawamfahamu. Kwa jumla ni kwamba
maswali yote ambayo sheria inamlazimisha kadhi kumuuliza mwenye
kukiri/mashahidi yanalenga kupatikana kwa ithibati kabla ya kutolewa kwa
hukumu inayoambatana na ikrari/ushahidi huo.
|