Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Dini ni nasaha, wakauliza kwa nani ? Akasema Mtume : Kwa Allah, Mtume wake, kwa viongozi wa waislamu na watu wa kawaida" Hadith Tukufu

KUTENGUKA KWA IKRARI YA ZINAA.

Faida

Katika macho ya sheria ikrari huzingatiwa kuwa ni hoja dhidi ya mwenye kukiri; yaani ni hoja inayomtia hatiani na kumpasishia adhabu kwa mujibu wa sheria. Wala hakusihi kukana/kutengua ikrari baada ya kuthibiti kwake mbele ya kadhi katika masuala ya haki ila katika masuala ya “haddi” kama zinaa, wizi, unywaji wa pombe na kadhalika. Masuala haya ya haddi (adhabu) kunasihi kukana/kutengua ikrari kwa mwenye kukiri. Mathalan, mtu akikiri uzinifu au kuiba au kunywa pombe, halafu akaitengua ikrari yake, utenguzi wake huo husihi mbele ya sheria na kwa kusihi kwake huko humpomoshea adhabu iliyomkabili kutokana na kosa hilo. Mithili ya kucharazwa bakora au kupopolewa kwa mawe kufuatia hatia ya uzinifu, au kucharazwa bakora kufuatia hatia ya unywaji pombe na kukatwa mkono kufuatia hatia ya wizi. Haya ni kwa upande wa haki za Allah Mola Mwenyezi, ama kwa upande wa haki za waja wa Allah (wanadamu wenziwe), hakusihi kutengua kwake ikrari baada ya kuthibiti mbele ya kadhi. Hakupomoki kurudisha kitu kilichoibwa kwa mwenyewe aliyeibiwa baada ya kukiri kuiba kisha akatengua ikrari yake, kwa sababu hiyo ni haki ya waja na si haki ya Allah.

Kumependelewa kwa Imamu katika “haddi” ya zinaa kumfundisha mtu aliyekiri kosa la zinaa kutengua ikrari yake. Angalia, mtu atakapokiri kutenda kosa la zinaa, halafu akatengua ikrari yake. Linalofuatia utenguzi huo wa ikrari ni kupomokewa na haddi (adhabu) iliyompasia kutokana kukiri kwake mara ya kwanza. Bila ya kujali kuwa utenguzi huo ulikuwa ni kabla ya kuanza kutekelezwa kwa adhabu husika au ni baada ya kuanza kutekelezwa kwa adhabu hiyo (ndani ya adhabu). Ikiwa ni kabla ya kuanza kutekelezwa kwa adhabu, kutasimamishwa kucharazwa bakora na kupopolewa kwa mawe. Na ikiwa ni baada ya kuanza kutekelezwa kwa adhabu husika, yaani baada ya kuanza kucharazwa bakora kadhaa au kupopolewa kwa mawe. Pale pale baada ya kutengua ikrari yake, atasikilizwa na adhabu itakoma mara moja na haitokamilishwa. Ni mamoja ametaja sababu ya utenguzi wake huo au hakutaja. Hii ni kwa sababu Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-alipomdhihirishia Maaiz kutengua ikrari yake kwa kumwambia “Huenda wewe ulibusu, au ulikonyeza au uliangalia tu”. Lau kauli hii ya Bwana Mtume ingelikuwa haimpomoshei adhabu husika ingelikuwa haina maana. Na kwa sababu walipoanza kumpopoa kwa mawe, Maaiz alisema: Nirudisheni kwa Mtume wa Allah, wala hawakumsikiliza (wakaendelea kumpopoa kwa mawe mpaka akafa). Walipomtajia hilo Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alisema: Kwa nini hamkumuacha, huenda angelitubia na Allah akampokelea toba yake”.

Ibn Hajar Al-asqalaaniy-Allah amrehemu-amesema: “Imepokelewa na Abuu Daawoud na isnadi yake ni HASAN”.

Ibn Abdul-barri amesema: “Na kauli hii (ya Bwana Mtume) ni dalili ya wazi kabisa inayoonyesha kwamba utenguzi wake unakubaliwa”. Mughnil-Muhtaaj [4/139]

Na kwamba hukumu ni hii hii iwapo mwenye kukiri atakimbia wakati wa kuanzwa kutekelezwa kwa adhabu inayoambatana na ikrari yake. Kukimbia huko kutampomoshea adhabu iliyomuwajibikia, kwa sababu ukimbiaji huo uko katika maana ya utenguzi wa ikrari. Yote haya ndiyo madhehebu ya maimamu wanne wa kisunni; Maalik, Shaafiy, Ahmad na Abuu Hanifah.

Na hali kadhalika atakapokiri chini ya mara nne, hakumlazimikii kukamilisha kiwango cha ikrari kufikia mara nne. Bali kunamuelea Imamu kumuambaa na kumuelezea kutokukamilisha ikrari. Kama Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-alivyompa Maaiz fursa ya kutengua ikrari yake pale alipokiri zinaa mbele yake mara ya kwanza, ya pili na ya tatu. Hivi ndivyo ilivyoelezwa katika kitabu (ZAADUL-MAADI).

 

  1. KUTHIBITI ZINAA KWA USHAHIDI WA KUONA:

Ushahidi wa mtu kwa kuona kosa la zinaa likitendeka huzingatiwa mbele ya sheria kuwa ni njia ya pili ambayo hatia ya zinaa huthibiti kwayo. Na tafsiri ya “ushahidi”  mbele ya sheria ni: [kutoa khabari au maelezo kuhusiana na jambo fulani kwa tamko maalum, nalo ni kule kusema “ninashuhudia”]

Sharti za shahidi:

Ili ushahidi utolewao uzingatiwe na sheria, kumeshurutizwa huyo shahidi awe:-

  1. muungwana (mtu huru); yaani asiwe mtumwa.
  2. mwenye akili timamu; yaani asiwe mwendawazimu au amelewa.
  3. mkubwa; yaani asiwe mtoto mdogo.
  4. mwenye murua; yaani asiwe mtu mpuuzipuuzi.
  5. si mwenye kutuhumiwa katika ushahidi wake.

{Rejae kitabu-(MUGHNIL-MUHTAAJ)-4/392  na NIHAAYATUL-MUHTAAJ (8/125)}.

Ili ushahidi wa kuona hatia/kosa la zinaa ukubaliwe mbele ya sheria, hapana budi washuhudie mbele ya kadhi mashahidi wanne waadilifu. Washuhudie kuwa mwanamume na mwanamke wametenda tendo khasa la zinaa na washuhudie kwa tamko la “zinaa”, waseme katika ushahidi wao: “tumewashuhudia wakizini”. Na sio kwa tamko jingine lo lote ambalo linabeba maana ya zinaa likichanganya pamoja na maana nyingine. Limekhusishwa tamko “zinaa” katika ushahidi kwa sababu hilo ndilo tamko pekee linalobeba na kumaanisha tendo haramu mbele ya sheria, kinyume na matamko mengine. Hii ni kwa sababu ya kutumika tamko hilo katika kauli tukufu ya Allah: “WALA MSIKARIBIE ZINAA. HAKIKA HIYO (zinaa) NI UCHAFU (mkubwa) NA NI NJIA MBAYA (kabisa)”. [17:32]

  1. SHERIA YA KUSHURUTIZWA MASHAHIDI WANNE KATIKA USHAHIDI WA ZINAA:

Tumeeleza kwamba ili ushahidi wa kuona kosa la zinaa ukubaliwe na uzingatiwe mbele ya sheria, hapana budi ushuhudiwe (utolewe) na watu wanne juu ya tendo lenyewe khasa. Hili la kushurutiza mashahidi wanne limethibiti kupitia kitabu (Qur-ani Tukufu) na sunah (hadithi za Bwana Mtume). Ama kitabu ni kauli tukufu ya Allah: “NA WALE WANAWAKE WAFANYAO MACHAFU MIONGONI MWA WANAWAKE WENU; BASI WASHUHUDISHIENI MASHAHIDI WANNE (waliowaona wanafanya hivyo) MIONGONI MWENU...” [4:15]

Na katika sunah, imepokelewa kutoka kwa Abuu Hurayrah-Allah amuwiye radhi-kwamba Sa’ad Ibn Ubaadah alisema: Ewe Mtume wa Allah, unaonaje nikimkuta mtu na mke wangu, nimpe muda mpaka nilete mashahidi wanne? Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akasema: “Naam”. Imamu Shaafiy & Maalik-Allah awarehemu.

Kwa dalili hizi, hapana budi kupatikana mashahidi wanne katika kutoa ushahidi wa kosa la zinaa. Wakiwa chini ya wanne, sheria itawaona kuwa ni wasingiziaji wenye lengo la kuvunja heshima ya mtu. Na hili linajulikana kisheria kwa jina la “qadhfu” ambayo huambatana na adhabu ya bakora. Kwa mantiki hii basi, kila mmoja wa mashahidi hawa wasiofikia idadi ya wanne watahukumiwa kucharazwa bakora themanini. Hivi ndivyo Amirul-Muuminina Umar Ibn Al-khatwaab-Allah amuwiye radhi-alivyowahukumu mashahidi wasiofikia idadi itambuliwayo na sheria. Akawacharaza bakora kwa kosa la “qadhfu”, na hukumu hii haikutokana na maoni binafsi ya Sayyidina Umar, bali alichofanya ni kuitekeleza kivitendo kauli tukufu ya Allah: “NA WALE WANAOWASINGIZIA WANAWAKE WATWAHARIFU (kuwa wamezini) KISHA HAWALETI MASHAHIDI WANNE. BASI WAPIGENI MIJELEDI (bakora) THAMANINI NA MSIWAKUBALIE USHAHIDI WAO TENA NA HAO NDIO MAFASIKI. ISIPOKUWA WALE WENYE KUTUBU BAADA YA HAYO NA WAKATENGENEZA AMALI NZURI (hao Allah atawasamehe kwani) BILA SHAKA ALLAH NI MWINGI WA KUSAMEHE (na) MWINGI WA KUREHEMU”. [24:4] Na kauli ya Allah: “MBONA HAWAKULETA MASHAHIDI WANE? NA WALIPOKOSA KULETA MASHAHIDI, BASI HAO MBELE YA ALLAH NI WAONGO”. [24:13]

 

 


TUJIFUNZE NA TUKUBALI:

“....Haikudhihiri zinaa kwa watu katu mpaka wakaifanya waziwazi ila itaenea kwao tauni na magonjwa mengine ambayo hayakuwepo kwa wahenga (wazee) wao...” Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Riwaya: Ibn Maajah, Bazaar & Al-baihaqiy-Allah awarehemu.


Forum | Guestbook | Tuandikie |