|
01.
KUTHIBITI ZINAA KWA MUHUSIKA KUKIRI YEYE MWENYEWE.
Kabla
hatujaanza kuangalia ni namna gani hatia ya zinaa inavyothibiti kutokana
na mtu mwenyewe kukiri kutenda kosa hilo bila ya kulazimishwa na
mtu/mamlaka yo yote. Ni vema kwanza tukalibahithi (tafiti) na kulichambua
neno hili ‘kukiri’ nini maana ya kukiri katika lugha na sheria.
A/.
KUKIRI KILUGHA:
Katika lugha ya Kiarabu neno “kukiri” halimaanishi ila kuthibitisha.
Kwa hivyo basi muarabu anaposema: “Fulani amekiri zinaa”,
anamaanisha kuwa fulani huyo amethibitisha yeye mwenyewe kuwa amezini.
B/.
KUKIRI KATIKA SHERIA:
Sheria inalitafsiri neno kukiri kuwa ni mtu kueleza haki awiwazo
nazo bila ya kubagua kuwa ni haki za Allah Muumba wake au ni zile za
wanadamu viumbe wenzake. Kwa maana hii basi mtu anapokiri zinaa mbele
ya kadhi, sheria humchukulia kuwa anatoa khabari kuwa amepasiwa na haki ya
Allah kwa kwenda kinyume na maamrisho au makatazo yake. Kwa hivyo
anastahiki adhabu ya kosa hilo kwa mujibu wa sheria. Kwa mantiki hii basi,
itakudhihirikia kuwa kisheria kukiri ni kinyume cha kupinga/kukanusha.
SHARTI
ZA KUSIHI IKRAARI (KUKIRI) YA MTU:
Ili
kukiri kuzingatiwe na sheria, kumeshurutizwa huyo mwenye kukiri:-
- awe
na akili timamu, asiwe mwendawazimu.
- awe
amebaleghe, yaani awe mtu mzima na wala asiwe mwanamdogo.
Zikikamilika
sharti mbili hizi ndipo hatia ya zinaa inaweza kuthibiti kisheria.
Itathibiti pale tu muhusika atakapokuja mbele ya kadhi yeye mwenyewe bila
ya kushurutishwa na mtu wala bila ya kutenzwa nguvu na mamlaka fulani.
Akaja hali ya kuwa ana akili timamu, mtu mzima akakiri yeye mwenyewe
kuzini walau mara moja tu. Haya ni kwa mujibu wa ilivyopokewa katika kisa
cha “Asiyfu-kibarua/mtumishi”, kama kilivyopokelewa na Abuu Hurayrah
na Zaid Ibn Khaalid-Allah awawiye radhi-wamesema: “Tulikuwa (tumekaa)
mbele ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akasimama mtu mmoja
akasema: Ninakuomba kwa haki ya Allah uhukumu baina yetu kwa kitabu cha
Allah. Khasimu (mgomvi) wake akasimama na alikuwa ni mjuzi zaidi wa sheria
kuliko yeye, akasema: Hukumu kwa (kutumia) kitabu cha Allah na unipe
idhini (ya kusema). Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akasema:
“Sema”. Akaanza kusema: Mwanangu wa kiume alikuwa kibarua kwa (bwana)
huyu, akazini na mkewe (bwana huyu). Nikampa kutokana na kitendo hicho
fidia ya mbuzi mia na mtumishi. Kisha nikawauliza watu wenye elimu,
nao wakanieleza ya kwamba mwanangu anapaswa kupigwa bakora mia moja
na kupelekwa uhamishoni kwa kipindi cha mwaka mmoja. Na kwamba mkewe
(bwana huyu) apigwe mawe mpaka kufa. Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-akasema: “Ninaapa
kwa yule ambaye nafsi yangu i mkononi mwake, nitahukumu baina yenu kwa
kitabu cha Allah uliotukuka utajo wake. Wale mbuzi mia moja na mtumishi
virudishwe, mwanao amepasiwa bakora mia na kupelekwa uhamishoni kwa
kipindi cha mwaka mmoja. Na muendee ewe kiji-Anas (Unaysi) mkewe huyu,
akikiri (zinaa) basi mpopoe kwa mawe mpaka kufa”. (Unaysi)
akamuendea, akakiri nae akampopoa kwa mawe mpaka akafa”. Bukhaariy
& Muslim-Allah awarehemu.
WAJIHI
WA KUITOLEA DALILI HADITHI HII:
Hadithi
hii imefumbuliza kwamba Bwana Mtume-Rehema na Amani
zimshukie-amekuangika (amekutungika) kupopolewa kwa mawe mpaka kufa kwa
utupu wa kukiri bila ya kuongeza kitu. Hivi ndivyo inavyofahamisha kauli
yake Bwana Mtume: “Na muendee ewe kiji-Anas mkewe huyu, akikiri
(zinaa) basi mpopoe kwa mawe mpaka kufa”.
KUTHIBITISHA
USAHIHI WA IKRAARI YA MWENYE KUKIRI ZINAA.
Kunatakikana
kwa Imamu katika hatia hii ya zinaa, kumuuliza mtu aliyekiri mbele yake
kutenda kosa hilo kuhusiana na suala zima la zinaa. Amuulize:-
ü
Zinaa ni nini?
ü
Zinaa huwaje? Hufanyikaje?
ü
Kitendo cha zinaa hufanyika wapi?
Imamu
hapaswi kumuuliza mtu aliyekiri zinaa swali kama: umezini lini.
Kwani hili ni swali wanaloulizwa mashahidi, haulizwi mwenye kukiri.
Usahihi wa ikraari ya zinaa utazingatiwa pale tu mwenye kukiri
atakapotaja/atakapoeleza tendo lenyewe khasa ili kuondosha “shub-ha”.
[Shub-ha hapa: ni hali ya kutokuwa na uhakika/uyakinifu wa jambo fulani].
Hana budi kufumbuliza (kueleza/kutamka wazi na bayana) kwani
“kinaaya”/fumbo haitoshi katika kadhia hii. [Neno “Kinaaya”
kilugha: ni kuzungumza/kutamka neno fulani ilhali unakusudia kitu kingine,
yaani kuzungumza kwa lugha isiyo wazi; lugha ya fumbo].
Haya
ndiyo maongozi ya kiongozi wa uma-Rehema na Amani zimshukie-kama
alivyoyasimulia Abuu Hurayrah-Allah amuwiye radhi-na kunakiliwa kwetu na
Imamu Abuu Daawoud-Allah amrehemu: “Je, ulimnajisi (ulimchafua)?”
Akajibu: Naam. (Mtume akaendelea) kumuuliza: “Mpaka ikaingia hiyo
iliyoko kwako ndani ya ile iliyoko kwake?” Akajibu: Naam. Akamuuliza
(tena): “Unajua zinaa ni nini?”, akajibu: Naam, nimemuendea kwa njia
ya haramu namna ambayo mwanamume anavyomuendea mkewe kwa halali. (Mtume)
akamuuliza: “Unakusudia nini kwa kauli yako hii?” Akajibu:
Unitwaharishe (kutokana na uchafu huu nilioufanya). Mtume akaamrisha
apopolewe kwa mawe mpaka kufa, akapopolewa”. Rejea kitabu
(FAT-HUL-BAARIY) cha Ibn Hajar Al-Asqalaaniy-Allah amrehemu.
Mwenye
kukiri akileta wasifu wa zinaa na kuithibitisha, kumependelewa Imamu
amlakinie kuirejea (kuitengua) Ikraari yake, kwa kumwambia: Huenda
ulimbusu tu, au ulimgusa tu au ulimuingilia kwa shub-ha. Maneno haya ni
mithili ya maneno aliyoyasema Bwana Mtume-Rehema na Amani
zimshukie-kumwambia Maaiz alipokiri zinaa: “Huenda ulibusu, au
ulikonyeza au uliangalia
tu”. Sahihi-Bukhaariy na sherehe yake Fat-hul-Baariy.
Mwenye
kukiri baada ya kuulizwa maswali yote hayo na akajibu: Hapana. Imamu
anatakiwa kuichunguza akili yake (huyo mwenye kukiri) na ili kupata
ithibati kuwa hana matatizo ya akili awaulize ndugu/jamaa zake. Hivi
ndivyo Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alivyofanya katika kadhia
ya Maaiz, pale alipowapelekea jamaa zake mjumbe akiwauliza: “Je,
mnajua ubaya wo wote kwa akili yake unaokufanyeni msikubali jambo lo lote
kwake?”
Haya
yote ni kwa sababu ya kutokuzingatiwa kwa ikraari ya
mwendawazimu wala punguani. Kwa kuzingatia kuwa akili si kitu-dhati
(chenye kuonekana), Imamu hana budi kulichunguza hilo kwa makini ili
kuepusha hatia ya kumpitishia hukumu mtu asiyezingatiwa na sheria.
Akishatambua kuwa hana matatizo yo yote ya akili, sasa ndipo amuulize juu
ya “Ihswaani”, yaani iwapo ameoa/ameolewa au aliwahi kuoa/kuolewa. Hii
ni kwa sababu ya kukhitalifiana kwa adhabu itolewayo kwa aliye
ndani/aliyewahi kuwa ndani ya ndoa na ambaye hajawahi. Amueleweshe kuwa
adhabu ya jarima ya zinaa kwa aliye ndani/aliyewahi kuwa ndani ya ndoa ni
kupopolewa kwa mawe mpaka kufa. Na bakora mia na kupelekwa uhamishoni kwa
kipindi cha mwaka mmoja kwa aliye nje ya ndoa. Baada ya yote haya ndipo
sasa Imamu atampitishia hukumu ya Allah inayompasa, iwapo hakutengua
ikraari yake. Kama alikuwa ni mtu aliye ndoani, baada ya kufa kwa
kupopolewa kwa mawe, atakoshwa, atakafiniwa (atavikwa sanda) na kuswaliwa
na kisha kuzikwa katika makaburi ya waislamu. Atatendewa yote haya kwa
kuzingatia kwamba yeye ni mwenye kuuliwa kwa haki, kwa msingi huu
atatendewa yote watendewayo maiti wengine waislamu. Maswahaba-Allah
awawiye radhi-walimuuliza Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-juu ya
kumkosha, kumkafini na kumswalia Maaiz, akawaambia: “Mfanyieni
muwafanyiayo maiti wenu”.
|