|
Mtazamo
wa sheria ya kiislamu katika dhambi/kosa la zinaa unatofautiana
mtofautiano wa mbingu na ardhi na ule wa kanuni za kibinadamu
zilizopitishwa na mabunge ya nchi mbalimbali ulimwenguni. Sheria ya
kiislamu inakizingatia kitendo cha ndoa kinachofanywa nje ya ndoa
halali kuwa ni zinaa inayompasishia muhusika adhabu kisheria. Bila ya
kuangalia kuwa tendo hilo limetendwa na mtu aliyemo ndani ya ndoa halali,
au alipata kuwa ndani ya ndoa au hajapata kuyaonja maisha ya ndoa
aslani. Hivi ndivyo Uislamu unavyoitazama dhambi ya zinaa. Ama kwa
upande wa sheria za kimataifa kwa ujumla wake, sheria zilizotungwa na
wanadamu kwa ajili ya wanadamu. Huku zinaa yenye kupasisha adhabu inakomea
katika tendo la ndoa linalofanywa na mwandoa nje ya ndoa yake. Huyu
ataadhibiwa tu na sheria hii kwa sababu tu ya kuvunja ahadi ya uaminifu
katika ndoa aliyokula kiapo cha kuilinda wakati wa kufunga ndoa. Hivyo
basi, kwa mtazamo wa sheria hii tendo la ndoa linalofanywa na asiye
mwanandoa halizingatiwi kuwa ni zinaa ikiwa litatendwa kwa maridhiano
binafsi baina ya wenza wawili hao. Ama likiwa si kwa maridhiano
litazingatiwa kuwa ni ubakaji (raping/violation), au mwanamke alikuwa
chini ya umri wa miaka kumi na nane (18years). Utaona ni namna gani
mapungufu ya mwanadamu mpungufu yanavyojidhihirisha katika sheria hii.
Sheria moja inakataza kitendo kimoja; kile kile kwa mlango huu na kwa
wakati huo huo kukiruhusu kupitia mlango mwingine. Ni wazi kuwa sheria
kama hii haiwezi kutekeleza jukumu la kuizuia, kuikomesha na hatimaye
kuitokomeza zinaa katika jamii, bali kinyume chake inaweza kuichochea.
Isitoshe sheria hii haimuadhibu mwanandoa aliyetenda tendo la ndoa nje ya
ndoa mpaka pale mwanandoa mwenza atakaposhitaki mbele ya vyombo vya
sheria. Iwapo mwanandoa atatenda tendo hili kwa ridhaa ya mwenza wake kama
linavyojitokeza hili katika zile nchi zinazojiita nchi za ulimwengu wa
kwanza. Au akatenda katika mazingira ya uficho bila ya mwenza wake
kutambua, katika hali mbili hizi hakabiliwi na adhabu yo yote kwa tendo
lake hilo. Hali kadhalika ikiwa tendo hili litatendeka baina ya wawili
walio nje ya ndoa; mwanamume hajaoa na mwanamke hajaolewa. Tendo hili
likatendeka katika mazingira ya ridhaa isiyozingatiwa na ridhaa
haizingatiwi iwapo mwanamke ana umri wa chini ya miaka kumi na nane. Hapa
sheria hii pungufu haihukumu ila upande mmoja tu, adhabu inamuangukia
mwanamume peke yake na kumtakasa mwenza wake huyo. Na hivi hivi ndivyo
linavyohukumiwa tendo la liwati (sodomy/homosexuality); kumuingilia
mwanamume au mwanamke kinyume na maumbile.
Ama
tukija katika sheria ya kiislamu tunaiona ikimuhukumu mzinifu mwanandoa na
asiye mwanandoa pindi ikithibiti kwa mujibu wa sheria kuwa katenda tendo
hilo chafu. Sheria inamuhukumu bila ya kuangalia kuwa amezini katika
mazingira ya maridhiano au nje ya mazingira hayo. Sheria itamuhukumu kwa
kuzingatia kuwa anavunja mjengo, usalama na afya ya jamii. Katika sheria
ya kiislamu kosa la zinaa ni kosa linaloigusa jamii nzima kwa
sababu madhara yake huenea na kuigharimu jamii nzima na wala sio muhusika
pekee. Ama katika sheria za kibinadamu zinaa huzingatiwa kuwa ni miongoni
mwa masuala binafsi yanayogusa mafungamano na mahusiano baina ya mtu mmoja
mmoja. Ni suala lisilogusa kwa namna yo yote maslahi ya jamii. Hili
linadhihirika pale ambapo sheria hii haitoi adhabu kwa tendo la zinaa ila
tu litakapotendwa na mwanandoa na akapelekwa na mwenza wake katika vyombo
vya sheria. Kama hakumshitaki au alimshitaki kisha akamsamehe, hapo sheria
haina uwezo wa kumuadhibu mzinifu huyu kwa kuzingatia kuwa hilo ni suala
binafsi na wenyewe wameamua kulimaliza kwa ridhaa yao. Kadhalika
ukilinganisha kosa na athari ya kosa hilo na adhabu itolewayo havilingani
hata kidogo na wala adhabu hiyo haiwazuilii watu kutenda uoza huo.
Kutokwenda sambamba kwa adhabu zitolewazo ukilinganisha na uzito na athari
mbaya itokanayo na kosa lenyewe. Kumetoa mwanya wa kuongezeka kwa kiwango
cha kutisha kwa vitendo vya ubakaji na ulawiti, kiasi cha mtu mzima
kutoona soni wala haya kukibaka kitoto kidogo kisichojua cho chote. Haya
yote yanaonyesha ni kwa kiasi gani wanadamu wanahitaji muongozo sahihi na
sheria kamili zisizo na mapungufu zitakazo wahakikishia amani, usalama na
utulivu wa kweli. Na hili halitapatikana ila tu kwa kujisalimisha katika
sheria za Allah Mola Mjuzi wa maslahi na manufaa ya waja wake. Tuufuate
kikamilifu muongozo wa Allah ambao anatuambia: “...BASI WATAKAOFUATA
MUONGOZO WANGU HUO HAITAKUWA KHOFU JUU YAO WALA HAWATAHUZUNIKA”.
[2:38]
03.
AINISHO/MAANA YA ZINAA KILUGHA NA KISHERIA.
Neno
‘ZINAA’ katika mizani na mtazamo wa Uislamu kama dini na mfumo sahihi
wa maisha, lina maana/tafsiri mbili. Maana mojawapo ya mbili hizo inarejea
katika lugha, yaani katika matumizi yasiyo ya kisheria. Na ieleweke
tunaposema au kutumia neno ‘lugha’ hapa, huwa hatuilengi ila lugha ya
Qur-ani Tukufu (Kiarabu). Wakati ile maana ya pili ya neno zinaa inarejea
katika sheria tukufu ya Allah. Sheria aliyowaletea waja wake wote kwa
tofauti ya rangi na lugha zao kupitia ulimi wa mja wake ampendaye kuliko
wote; Nabii Muhammad-Rehema na Amani zimshukie. Hebu sasa na tuzitupie
jicho na fikra maana/tafsiri hizo moja baada ya nyingine ili tuende
sambamba wakati tutakapokuwa tunalitaja au kulitumia neno
‘zinaa’.
- ZINAA
KILUGHA:
Neno
‘zinaa’ katika lugha ya Kiarabu limetumika kwa maana kadhaa kama
ifuatavyo:-
I.
DHIKI/KUBANWA-Maana hii tunaipata kupitia kauli yake Bwana
Mtume-Rehema na Amani zimshukie-wakati akiuelekeza uma wake juu ya swala
tano: “Asiswali mmoja wenu na ilhali yeye ni ZANAA”. Yaani
akiwa ni mwenye dhiki au kubanwa na mkojo.
II.
UFINYU- Waarabu wanaposema (ZANAL-MAUDHWIU), maana: (Mahala/sehemu
imezini) wanamaanisha kuwa sehemu/mahala hapo pamekuwa finyu, yaani
hapatoshi, hapakidhi haja.
Hivi
ndivyo ilivyoelezwa katika kamusi ya lugha inayoitwa (LISAANUL-ARAB),
mtunzi: Ibn Mandhuur. Na katika kamusi (TAAJUL-ARUUSI), mtunzi: Zabiydiy.
III.
UOVU- Waarabu wanaposema (ZANAR-RAJULU), maana: (Mtu amezini)
wanakusudia kuwa amefanya uovu.
Hivi
ndivyo lilivyotafsiriwa neno ‘zinaa’ katika kamusi iitwayo
(AL-BAHRUL-MUHIYTW). Hizi ni baadhi ya maana za neno ‘zinaa’ kama
linavyotumiwa na Waarabu katika mazungumzo (matumizi) yao ya kawaida;
yasiyo ya kisheria.
- ZINAA
KISHERIA:
Mafaqihi
wa kiislamu wameiarifisha zinaa kuwa: ni kila maingiliano ya kimwili
baina ya mwanamke na mwanamume yaliyofanyika nje ya ama ndoa sahihi,
shib-hu ya ndoa au miliki ya kuumeni. Hivi ndivyo mafaqihi
walivyoitafsiri zinaa kama tunavyoweza kusoma katika vitabu kadhaa vya
fani ya Fiq-hi mithili ya BIDAAYATUL MUJTAHIDI WA
NIHAAYATUL-MUQTASWID.
|