Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Dini ni nasaha, wakauliza kwa nani ? Akasema Mtume : Kwa Allah, Mtume wake, kwa viongozi wa waislamu na watu wa kawaida" Hadith Tukufu

ADHABU YA ZINAA KATIKA SHERIA YA KIISLAMU

Faida

I/. UTANGULIZI:

     01: ATHARI YA ZINAA KWA MTU BINAFSI NA KWA JAMII.

 Inazingatiwa jozi ya uwili, uwili utokanao na ujike na udume unaopatikana katika vitu vyote vilivyomo katika maisha haya (existence). Jozi yenye kupatikana kwa wanadamu, hayawani, mimea, jamadi (inanimate), katika baki ya maada nyingine na hata katika chembe (particle/atom) za vitu vyenye mkondo hasi na chanya. Jozi hii inazingatiwa kuwa ni ajabu (phenomenon) yenye kuvuta akili na fikra za walimwengu kutafiti na kubahithi. Qur-ani Tukufu inauvuta mtazamo na akili ya mwanadamu kuielekea ajabu hii kupitia kauli tukufu ya Allah: “NA KATIKA KILA KITU TUMEUMBA DUME NA JIKE ILI MPATE KUFAHAMU”. [51:49] Akasema tena: “AMETUKUKA ALLAH ALIYEUMBA DUME NA JIKE KATIKA (vitu) VYOTE;KATIKA VILE IVIOTESHAVYO ARDHI (mimea) NA KATIKA NAFSI ZAO (wanadamu) NA KATIKA VILE WASIVYOVIJUA”. [36:36]

Allah Mola Muumba ameumba jozi ya udume na ujike katika kila jinsi na aina ya viumbe vyake. Eneo na dhima ya jozi hiyo hufanya kazi katika ulimwengu wake makhsusi kwa kulingana na nidhamu (utaratibu) thabiti; isiyo ya kubahatisha. Katika eneo la wanadamu tunaiona jozi hii baina ya mwanamume na mwanamke ni chombo/njia ya kuzaana, kuongezeka na kujiimarisha sawasawa (to balance) katika siha ya mwili na nafsi. Na kwa kupitia ujozi huu ndio kizazi cha wanadamu huendelea kubakia katika maisha ya sayari hii ya dunia.

Isitoshe, mafungamano ya kimaumbile baina ya mwanamume na mwanamke kama tuyashuhudiavyo katika uhalisia wa maisha. Mafungamano haya ni alama dhahiri juu ya asili moja inayo wachanganya pamoja mwanamume na mwanamke tangu mwanzo wa kuwepo kwao. Katika asili yao Allah amewaumba wawili hawa kutokana na nafsi moja kama tusomavyo: “ENYI WATU! MCHENI MOLA WENU AMBAYE AMEKUUMBENI KATIKA NAFSI (asili) MOJA. NA AKAMUUMBA MKEWE KATIKA NAFSI IE ILE. NA AKAENEZA WANAUME WENGI NA WANAWAKE KUTOKA KATIKA WAWILI HAO...”. [4:1]

Kwa kuuzingatia ukweli huu ulio dhahiri kwa kila mmoja wetu, tunalazimika kukubali kwamba kila mmoja wa wanajozi hawa; mwanamume na mwanamke ni sehemu isiyotengeka ya mwenzake. Kwa maneno mengine tunaweza kusema kuwa kila mmoja wao ni mpungufu anayekamilishwa na mwenziwe pindi waunganapo kama jozi moja kamili. Wawili hawa kwa pamoja ndio huunda umbile moja kamili la mwanadamu. Umbile ambalo halipatikani ila kwa wawili hawa kuungana na kuchanganyika pamoja katika maisha ambayo yatawaunganisha na kuwa nafsi moja. Na hili la kuwa nafsi na mwili mmoja halipatikani ila kwa njia na msaada wa ndoa na si vinginevyo. Ni kwa sababu hii ndio mfumo wa ndoa katika Uislamu ukawa ni mfumo wa kukamilishana (integration/complementarity) baina ya mwanamume na mwanamke. Kukamilishana huku katika uhalisia wake ni makutano binafsi yanayoubadilisha uhusiano baina ya wanandoa kuwa utulivu wa nafsi (tranquility), mapenzi na huruma (mercy). Hivi ndivyo inavyotubainishia kauli hii tukufu ya Allah: “NA KATIKA ISHARA ZAKE (za kuonyesha ihsani zake juu yenu) NI KUWA AMEKUUMBIENI WAKE ZENU KATIKA JINSI YENU ILI MUPATE UTULIVU KWAO, NAYE AMEJAALIA MAPENZI NA HURUMA BAINA YENU. BILA SHAKA KATIKA HAYA ZIMO ISHARA KWA WATU WANAOFIKIRI”. [30:21]

Hii ndio siri na falsafa ya kuumbwa mwanamume na mwanamke kutokana na asili moja. Ndoa ndio mfumo bora unaobeba dhamana ya utwaharifu wa tone la manii (sperm) na ule wa tumbo la uzazi (womb). Ndoa huchukua dhima ya kuhakikisha kuwa manii yametoka ndipo kuingia ndipo, yaani yametoka kihalali kuingia mahala pa halali (mke). Ni katika hali na mazingira haya  ya ndoa ndio hudhibitika na kuthibitika ukweli wa nasabu ya mwanadamu tofauti na ile ya hayawani wengine. Ni chini ya mfumo huu ndio mzazi huwa hana shaka kuwa mzaliwa ni mwanawe atokanaye na damu yake. Na kwa janibu ya mwana pia huwa hana shaka juu ya mzazi wake. Nje ya mfumo huu, mafungamano ya kijinsia baina ya mwanamume na mwanamke kwa njia ya zinaa hupelekea upotevu na kukatika kwa mlolongo wa nasabu ya mwanadamu. Katika hali na mazingira haya machafu yanayokhalifiana na maumbile seuze sheria tukufu. Hakuna baba wa kweli (mume) anayemjua mwana wa uti wa mgongo wake, wala mwanamke anayemjua mwana wa kifua (mbavu) chake aliyembeba katika tumbo lake la uzazi (bowels). Wala mtoto hamjui baba yake aliyemzaa. Kwa sababu hii, bashariya (jamii ya wanadamu wote) inaporomoka hadi kufikia kiwango cha wanyama katika kuzaliana kwao. Ni kwa kuyaangalia madhara na udhalili huu ndipo ndoa katika Uislamu ikawa ndio njia sahihi ya kuigwa na kufuatwa ambayo huwakutanisha pamoja mwanamke na mwamume. Na ndio njia ya kimaumbile ya kuzaliana inayotakiwa kuyatawala maisha ya mwanadamu kwa ajili ya kuhifadhi na kulinda hadhi, utukufu na heshima ya mwanadamu kama mtu binafsi na kama jamii. Allah Mola Mtukufu anatuambia: “NA HAKIKA TUMEWATUKUZA WANADAMU...” [17:70]  Sasa ikiwa Allah Mola aliyetuumba ametutukuza sisi waja wake na akatuwekea utaratibu wa ndoa ili kuuchunga na kuuendeleza utukufu wetu huu. Kwa nini basi sisi tuliofadhiliwa na kupendelewa kwa kupewa hiba ya utukufu huu tunaukataa?! Na badala yake tunautwaa uduni na utwefu kwa kufuata njia chafu na mbaya ya zinaa inayotuweka na kutulinganisha sawa na wanyama ambao hawakupewa utukufu mithili ya tuliopewa sisi?!

Tukiwa wakweli na tukizipa uhuru  fikra na mawazo yetu, tutakongamana na kuwafikiana kwamba zinaa ni chimbuko la fisadi kwa mtu binafsi na jamii kwa ujumla. Zinaa ina athari mbaya zinazomrudia muhusika mwenyewe katika maisha yake na jamii ambazo zinaihalalisha na kuitungia mifumo maalumu. Chini ya mwavuli wa mifumo hii michafu inayonuka, mtu anakuwa hana kinga dhidi ya zinaa kwa nafsi, familia na mke wake. Ukiachilia mbali kwamba zinaa ni mashine yenye jukumu la kuifisidi siha (afya) ya muendekezaji wa tendo hili lisilo la kiutu. Zinaa pia ni kiwanda chenye dhima ya kuzalisha na kusambaza maradhi ya kuambukiza yatokanayo na uoza huu. Maradhi ambayo kwa namna moja au nyingine huharibu kizazi na asili ya kizazi. Ukimwi ni katika jumla ya mazao makuu yanayozalishwa na kiwanda hiki zinaa, huu ni ukweli usiokubali kupingwa wala kukanushwa. Kutokana na kuizingatia fisadi na madhara haya makubwa, ndipo Uislamu kama dini na mfumo sahihi wa maisha ukaikamia na kuikemea vikali kabisa zinaa. Ukaifanya zinaa kuwa ni miongoni mwa madhambi makubwa nyuma ya dhambi za kumshirikisha Allah na kumuua mtu. Kama ulivyofanya kujilinda na kujihifadhi na zinaa kuwa ni miongoni mwa sifa za waumini waliofaulu na kufuzu, kama tusomavyo: “HAKIKA WAMEFUZU WAUMINI. AMBAO KATIKA SWALA ZAO HUWA NI WANYENYEKEVU. NA AMBAO HUJIEPUSHA NA MAMBO YA UPUUZI. NA AMBAO (nguzo ya) ZAKA WANAITEKELEZA. NA AMBAO TUPU ZAO WANAZILINDA. ISIPOKUWA KWA WAKE ZAO AU KWA (wanawake) WALE ILIYOWAMILIKI MIKONO YAO YA KUUME (kulia). BASI HAO NDIO WASIOLAUMIWA. (Lakini) ANAYETAKA KINYUME CHA HAYA, BASI HAO NDIO WARUKAO MIPAKA (ya Allah)”. [23:1-7]

Na kwa mantiki hii hii, Uislamu ukamuweka mtu mwenye kuiacha na kujiepusha na zinaa kuwa ni miongoni mwa aina saba za watu. Watu watakaofunikwa na kivuli cha arshi ya Allah katika siku nzito ambayo hakutakuwepo na kivuli kingine ila hicho tu. Haya ni kwa mujibu wa ilivyopokelewa katika hadihti ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie: “Makundi saba ya watu, Allah atayapumzisha chini ya jivuli la Arshi yake katika siku ambayo hakitakuwepo kivuli cho chote ila kivuli chake (hiyo arshi)...(akamjumuisha miongoni mwao)....na mwanamume aliyeitwa  (katika machafu) na mwanamke mwenye hadhi na uzuri, akasema hakika mimi ninamkhofu Allah....” Bukhaariy & Muslim-Allah awarehemu.

Kwa kuuangalia ubaya na khatari ya zinaa, Allah Mtukufu akaiharamisha zinaa kupitia kitabu chake kitukufu na suna ya Mtume wake Mtukufu, akasema: “WALA MSIIKARIBIE ZINAA. HAKIKA HIYO (zinaa) NI UCHAFU (mkubwa) NA NI NJIA MBAYA (kabisa)”. [17:32] Allah akaifanya zinaa kuwa ni miongoni mwa madhambi makubwa, ikizifuatia nyuma dhambi za kumshirikisha Allah na kuiua nafsi ambayo Allah ameharamisha kuuawa ila kwa haki. Falsafa na hekima ya kufanywa madhambi haya kuwa ni makubwa ni kwa sababu kumshirikisha Allah hufisidi dini. Wakati ambapo kuiua nafsi hufisidi kiwiliwili na kuiachia zinaa kufisidi nasabu za jamii ya wanadamu. Hili ndilo lililompelekea Imamu Ahmad Ibn Hambal-Allah amuwiye radhi-kusema: “Siijui baada ya dhambi ya kuua dhambi iliyo kubwa zaidi kuliko zinaa”. Akaijengea hoja kauli yake hii kwa hadithi ya Abdillah Ibn Masoud-Allah amuwiye radhi-amesema: Nikasema: Ewe Mtume wa Allah ni dhambi ipi iliyo kubwa kuliko zote? Akajibu: Ni kumfanya Allah kuwa ana mshirika (shirki) na ilhali yeye ndiye aliyekuumba”. Akasema: Nikamuuliza (tena): Kisha ipi? Akajibu: “Ni kumuua mtoto wako kwa kuchelea asije kula pamoja nawe (njaa)”. Akasema: Nikaendelea kumuuliza: Kisha (inafuatia dhambi) ipi? Akajibu: Ni kuzini na mke wa jirani yako”. Bukhaariy, Muslim & Nasaai-Allah awarehemu. Katika kuisadikisha kauli ya Mtume wake ndipo Allah Mtukufu akaiteremsha kauli yake: “NA WALE WASIOMUOMBA MUNGU PAMOJA NA ALLAH (shirki), WALA HAWAIUWI NAFSI ALIYOIHARIMISHA ALLAH ISIPOKUWA KWA HAKI, WALA HAWAZINI. NA ATAKAYEFANYA HAYO ATAPATA MADHARA (papa hapa ulimwenguni  kabla ya akhera). NA ATAZIDISHIWA ADHABU SIKU YA KIYAMA NA ATAKAA HUMO KWA KUFEDHEHEKA (muda mrefu kabisa) MILELE. ILA YULE ALIYETUBIA NA KUAMINI NA KUFANYA VITENDO VIZURI, BASI HAO NDIO ALLAH ATAWABADILISHIA MAOVU YAO KUWA MEMA. NA ALLAH NI MWINGI WA KUSAMEHE (na) MWINGI WA KUREHEMU”. [25:68-70]

Uislamu umeiharamisha zinaa kwa sababu ya madhara adida (mengi) yanayotokana nayo na ukaweka adhabu kali kwa kila mwenye kujitumbukiza katika uchafu na njia mbaya hii. Falsafa na hekima ya adhabu kali hii ni kumlinda mtu binafsi na jamii kwa ujumla dhidi ya madhara na taathira mbaya ya zinaa. Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-akatutahadharisha dhidi ya kuacha kuzitekeleza  adhabu hizi kwa kumuonea huruma muhusika,akatuambia: “Itakayemzuilia huruma yake kuitekeleza adhabu miongoni mwa adhabu za (makosa zilizowekwa na) Allah. Bila ya shaka huyo atakuwa amempinga Allah katika amri yake”. Ahmad-Allah amrehemu.

 



Forum | Guestbook | Tuandikie |