Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Dini ni nasaha, wakauliza kwa nani ? Akasema Mtume : Kwa Allah, Mtume wake, kwa viongozi wa waislamu na watu wa kawaida" Hadith Tukufu

ADHABU YA ZINAA KATIKA SHERIA YA KIISLAMU

Faida

Mpenzi msomaji wetu-Allah akuwafikishe kupenda kujifunza.

Assalaam Alaykum Warahamatullah! Ama baad, kutokana na ukweli kwamba ulimwengu hivi sasa umegubikwa na magonjwa mengi ya hatari  yenye kuambukiza. Magonjwa ambayo historia haituonyeshi kuwepo kwake ulimwenguni katika dunia ile ya wahenga wetu. Magonjwa mithili ya ukimwi, ebola na mengineyo ambayo wataalamu wa sayansi ya tiba wanakiri bayana kuwa chanzo chake kikuu cha kuambukiza kutoka mtu mmoja hadi mwingine ni zinaa. Magonjwa haya ni ushahidi dhahiri wa jinsi ambavyo wanadamu wa leo hawataki kuishi kulingana na mfumo wa maisha waliofumiwa na Allah Mola Muumba wao aliye Mjuzi wa lipi limfaalo mwanadamu na lipi lisilomfaa. Watu wameuvua utu wao na kuuvaa unyama pale walipoacha njia halali na nzuri ya kukidhi haja zao za kimwili na kuzaliana ndani ya ndoa. Wakaamua kufanya zinaa na hata kuthubutu ulawiti na usagaji. Matokeo yake leo serikali mbalimbali duniani badala ya kutenga mabilioni ya pesa katika nyanja za ustawi wa jamii, mapesa hayo yamekuwa yakipotea bure katika jitihada za kujaribu kuupiga vita ukimwi na maradhi mengine yasababishwayo kwa asilimia tisini na tisa kama sio mia na zinaa.

Ni dhahiri isiyo na kificho wala kukubali kupingwa kwamba vita hii ambayo tunajasiri kuiita kuwa ni ‘vita pofu’ dhidi ya janga hili hatari la ukimwi iliyotangazwa na dunia nzima, kamwe haitafanikiwa. Bali janga  na dudu baya hili litaumaliza ulimwengu mzima hata kama bajeti zote za serikali zote duniani zitatumiwa katika kampeni za kuutokomeza ukimwi. Kwa nini tunajasiri kusema hivi na sio kusema tu bali kusema kwa kinywa kipana kabisa. Naam, tunasema hivi kwa sababu ulimwengu hautaki kukiri kuwa adui tunayepambana nae bila ya mafanikio ni matokeo ya matendo yetu machafu. Ni natija ya matendo yetu yasiyo na utu, ni zao litokanalo na kuutupilia mbali mfumo sahihi wa maisha tuliofumiwa na Allah na badala yake tukajiundia mifumo yetu wenyewe. Hili ni tendo lililopindukia ukomo wa ubaya na uovu, kwani japokuwa hatutamki kwa ndimi zetu, matendo yetu haya yanamwambia Allah Muumba wa vyote na yote. Yanamwambia aliyetupa uhai huu kuwa hajui na wala hafai kutupangia sheria za kutuongoza katika maisha haya ambayo kila mmoja wetu anakiri kuwa ni mali na milki yake. Ni sawa na kumwambia kuwa sheria zake zimepitwa na wakati na ilhali hata huo wakati wenyewe umeembwa nae, kwa maana hiyo hazifai na wala hazihitajiki katika zama zetu hizi za maendeleo ya sayansi na teknolojia. Zama za uhuru usio na mipaka; zama za mtu kuishi kwa mujibu wa matashi na matamanio yake.

Ndugu zanguni, tukiri na tukubali ili tusalimike sisi wenyewe na tuusalimishe ulimwengu. Dawa pekee, kinga na tiba sahihi ya maradhi hatari ya ukimwi ni kuacha zinaa na wala sio kutumia kondom. Ni kuunyenyekea na kuufuata mfumo sahihi wa maisha tuliochaguliwa na Allah Mola Mtukufu. Ni kwa kufanya hivi tu ndipo tunapoweza kuokoka na kunusurika na gonjwa hili hatari. Kinyume na hivi ni kucheza na kujidanganya sisi wenyewe, tutatenga mabilioni ya mapesa, tutafundisha elimu ya ngono mashuleni. Tutasambaza vijarida, vipeperushi na matangazo yaelimishayo kuhusu ukimwi, tutakuwa na mpenzi mmoja, tutavaa kondom na....na.... Lakini bado ukimwi utaendelea kutuangamiza mithili ya moto uziangamizavyo nyasi kavu nyikani. Turejee ndugu zanguni kwa Allah, tujisalimisheni katika hukumu na sheria za  Allah, tuishi maisha tuliyopangiwa na Allah aliyetupa bure maisha haya. Kufanya hivi ndio kusalimika na kuokoka  dhidi ya janga angamizi la ukimwi na majanga mengineyo, tukubali au tukatae huu ndio ukweli.

Ndugu msomaji wetu, bila ya chembe ya shaka zinaa ni katika jumla ya madhambi makubwa. Zinaa ni sababu, chemchem na chanzo cha aina mbalimbali za shari, uovu na fisadi kubwa katika jamii ya wanadamu. Zinaa husababisha kudhoofika kwa kizazi, upotevu wa nasabu za wanadamu  na kubomoka kwa familia. Ni kwa ajili ya sababu hizi na nyinginezo, ndio tunauona Uislamu ukiiharamisha zinaa na kuizuia kwa njia za malezi ya kiroho na ndoa. Ili kuhakikisha kuwa tendo hili chafu la zinaa haliichafui na kuifisidi jamii, Uislamu ukaweka adhabu itakayomzuia mzinifu kufanya tendo hilo baya. Kwa kuweka sheria hizi, Uislamu ukawa umemuhifadhi mtu binafsi na jamii nzima kutokana na athari mbaya zitokanazo na uchafu huu wa zinaa. Wakati ambapo Uislamu unayafanya yote haya, kanuni zilizowekwa na kutungwa na binadamu viumbe dhaifu na wapungufu wa kila hali. Sheria binadamu hizi zinampa mtu uhuru wa kufanya zinaa katika hali ya maridhiano na makubaliano baina ya wahusika wa tendo hili. Sote ni mashahidi juu ya fisadi na uharibifu unaotokana na uhuru huu wa maridhiano machafu aliyopewa mwanadamu na mwanadamu mwenziwe. Hii yote inaonyesha udhaifu wa mwanadamu na haja yake ya kuwa na muongozo sahihi wa kumuongoza katika maisha yake. Muongozo huu hauwezi kutoka kwa mwanadamu aliye sheheni mapungufu kama yeye, bali ni kwa Muumba wa walimwengu na ulimwengu.

Kwa kuyazingatia yote haya, Website yako {WEBSITE UISLAMU-MTUMISHI WA UMMA}, inaona fakhri kukutumikia kwa kukuletea mfululizo wa makala zitakazokuwa chini ya anuani: ADHABU YA ZINAA KATIKA SHERIA YA KIISLAMU kupitia jukwaa lako hili la NASAHA ZA WIKI. Lengo mama la makala hizi ni kutaka kukumbusha juu ya maafa ya zinaa na namna ambavyo Uislamu unavyoihifadhi jamii dhidi ya janga hili. Ni matumaini ya WEBSITE UISLAMU kuwa utanufaika na makala hizi na zitakusaidia kuliepuka janga hili la ukimwi. Karibu unufaike kwa msaada na fadhila zake Allah kuanzia wiki kesho.

Wassalaam Alaykum Warahamatullah!

Daima ni Website yako; Website Uislamu-Mtumishi wa umma.

 



Forum | Guestbook | Tuandikie |