Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Dini ni nasaha, wakauliza kwa nani ? Akasema Mtume : Kwa Allah, Mtume wake, kwa viongozi wa waislamu na watu wa kawaida" Hadith Tukufu

KUTUKANA (KUSINGIZIA) DAHARI (ZAMA/WAKATI) ...X

Faida

Miongoni mwa maafa yenye kuogopewa (makubwa) na pingamizi hasi ni kuitupia lawama dahari na manun’guniko dawama juu ya dhulma ya dahari na ugumu wa siku. Kiasi cha mtu kufikia kuisawirisha dahari kuwa ni khasimu anayemdhulumu na kumtesa, au ni adui anayemngojelea misiba. Au ni mtawala dhalimu anayemuonea mtu asiye na hatia, huku akimkumbatia mtu muovu. Hizi zote ni nadhari (mitazamo) shurutizi ambazo ama mtu mmoja mmoja au makundi ya watu hujaribu kuzitoa nafsi zao hatiani kupitia nadharia hizo. Wakakimbia kubeba mzigo wa matendo/makosa yao na badala yake kujaribu kuwabebesha wengine au kuibebesha dahari, kadari, bahati mbaya, sadfa na kadhalika.

Wajibu wao ulikuwa ni kujaribu kuchunguza kwa nini wamefikwa na nakama (adhabu) na wameondokewa na neema. Kisha watafute ufumbuzi na suluhisho la kina linaloviunganisha pamoja visababishi  na sababu. Linalojumuisha pamoja natija (matokeo) na vyanzo (chimbuko) kulingana na suna (taratibu/kawaida/kanuni) ya Allah Mola Muumba kwa viumbe vyake. Kwani kwa yakini dahari ni chombo tu kinachobeba matukio yanayoendeshwa na kupitishwa na Allah Muumba dahari, matukio na watukiwa (viumbe). Huyapitisha matukio hayo kwa mujibu wa sheria na utaratibu wake aliojipangia Yeye mwenyewe. Hii ndio maana muradi ya hadithi hii sahihi: “Msiitukane dahari, kwani kwa yakini Allah ndiye DAHARI”. Muslim-Allah amrehemu

Mapendeleo na makusudio ya kauli ya Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie: “...Allah ndiye DAHARI”, ni kuwa Yeye Allah ndiye muweka kawaida/kanuni za maumbile na ndiye mpitishaji na muemdeshaji wake.

Tujifunze kutoka na  historia na matukio ya kweli yaliyowafika wenzetu waliotutangulia katika imani. Waislamu waliposhindwa katika vita vya Uhud wakiwa pamoja na Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-na maswahaba sabini wakafa shahidi. Walikaa chini wakajiuliza sababu ya donda na balaa lililowasibu baada ya ushindi. Jawabu ya Qur-ani ikawa: “NYINYI ULIPOKUFIKENI MSIBA AMBAO NYINYI MMEKWISHAWATIA (maadui) MARA MBILI YA HUO, MNASEMA: UMETOKA WAPI HUU? SEMA: HUO UMETOKA KWENU WENYEWE. HAKIKA ALLAH NI MWENYE UWEZA JUU YA KLA KITU”. [3:165] Qur-ani Tukufu inaikariri kanuni/kawaida hii jumla pale inaposema: “HAYO (ya kuwafika balaa hizi) NI KWA SABAU ALLAH HABADILISHI KABISA NEEMA ALIZOWANEEMESHA WATU, HATA (mpaka) WABADILISHE WAO YALIYOMO NYOYONI MWAO (wende nyendo mbaya ndipo Allah awaondoshee neema yao)...”. [8:53]

Kutokana na ukweli huu ulio wazi kabisa ni vema wanadamu wakazirushia lawama nafsi zao huku wakijaribu kusawazisha kombokombo (makosa) zao na kutengeneza palipofisidika badala ya kuilaumu dahari na kuzikosoa zama. Ni wajibu wa muumini anaposhukiwa na jambo baya (maafa) kuirejea nafsi yake na kuangalia sababu ya hayo yaliyomsibu kutokana na ukweli kwamba: “NA MISIBA INAYOKUPATENI NI KUTOKANA NA VITENDO VYA MIKONO YENU...” [42:30] Na aseme kama alivyosema nabii Musa; mneni wa Allah-Amani imshukie-wakati aliporejea kwa kaumu yake akitoka kuzungumza na Mola wake. Akawakuta watu wake wamekwishapotea, wamejifanyia kigombe kilichokuwa na sauti (hakina roho) kuwa ndio Mungu wao wakikiabudu. Wakazitupa nyuma ya migongo yao nasaha za nabii Haarun-Amani imshukie-wakamdharau wasisikilize maneno yake na hata wakakaribia kumuua. Hapo ndipo nabii Musa akamuelekea Mola wake kwa unyenyekevu akimuomba: “...MOLA WANGU! NISAMEHE MIMI NA NDUGU YANGU NA UTUINGIZE KATIKA REHEMA YAKO, MAANA WEWE NDIYE MWENYE KUREHEMU ZAIDI KULIKO WENYE KUREHEMU (wote)”. [7:151] Na aseme kama walivyosema watakatifu wa Allah wakati wenzao walipokufa mashahidi: “...WALA HAWAKUDHOOFIKA WALA HAWAKUDHALILIKA. NA ALLAH ANAWAPENDA WAFANYAO SUBIRA. WALA HAIKUWA KAULI YAO (watakatifu hao) ILA NI KUSEMA: MOLA WETU! TUGHUFIRIE MADHAMBI YETU NA KUPITA KWETU KIASI KATIKA MAMBO YETU NA ITHIBITISHE MIGUU YETU NA UTUSAIDIE JUU YA WATU MAKAFIRI. ALLAH AKAWAPA MALIPO MAZURI YA DUNIANI NA MALIPO MAZURI YA AKHERA. NA ALLAH ANAWAPENDA WAFANYAO MEMA”. [3:146-148]

Mpenzi msomaji wetu, Allah akunufaishe na mfululizo wa makala hizi zilizokuwa chini ya anuani: WAKATI KATIKA MAISHA YA MUISLAMU. Makala zilizokuwa zikikujia kupitia jukwaa lako la (NASAHA ZA WIKI). Tunapenda bali tunalazimika kumshukuru Allah kwa ukamilifu na tunamuomba maghfira kwa mapungufu yaliyojitokeza katika makala hizi. Mpaka hapa makala hizi zitakuwa zimetamatia huku tukitaraji kuwa zitakuwa zimekuelimisha na kukunufaisha kwa namna moja au nyingine. Tunakutakia usomaji mwema na endelea kunufaika na kufaidika na chakula cha roho kinachotayarishwa na kupikwa na mtumishi wa uma (WEBSITE UISLAMU), kwani ipo na itaendelea kuwepo inshallah kwa ajili yako. Tukutane juma lijalo inshaallah.

 



Forum | Guestbook | Tuandikie |