Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Dini ni nasaha, wakauliza kwa nani ? Akasema Mtume : Kwa Allah, Mtume wake, kwa viongozi wa waislamu na watu wa kawaida" Hadith Tukufu

MAKALA MAALUM-TUMPENDEJE BWANA MTUME ?

Faida

Ndugu waislamu,          Assalaam Alaykum!

Tumo na tunaishi ndani ya mwezi wa Rabiul–Awwal au Mfungo sita kama tulivyozoea kuuita.  Ni katika siku ya Jumatatu ya usiku wa mwezi kumi na mbili wa mwezi kama huu wa mwaka 570 A.D. alizaliwa Bwana wa viumbe wote, kipenzi cha Allah Mtume Muhammad–Rehema na Amani zimshukie.  Katika kutukuza mazazi ya Bwana huyu mtukufu, waislamu wakajiwekea utaratibu usiovunja  cho chote katika misingi ya dini yao; utaratibu wa kusoma MAULID kila unapofika mwezi huu. Maulid hizi ni sherehe za miaka mingi ambazo hujirudia kila mwaka.  Ni sherehe za kukumbuka na kuyaenzi mazazi matukufu ya Bwana huyu Mtukufu. Tunasema kama walivyosema wanazuoni wakubwa wa kutegemewa kwamba si vibaya kusherehekea mazazi ya Bwana Mtume kwa kusoma maulidi lakini tunasema:

ü      Je, ni wangapi miongoni mwetu tunajua maulidi ni nini?

ü      Je, ni nini natija na athari ya maulidi katika maisha yetu ya kila siku sisi kama waislamu?

ü      Je, tunajifunza nini kutokana na hizi sherehe za maulidi za kila mwaka?

Haya ni maswali ambayo kila mmoja wetu ni lazima ajiulize na ayapatie majibu yake. Ni kwa kufanya hivi ndipo tutakuwa tumeyasherehekea maulidi haki ya kuyasherehekea na ndipo lengo la maulidi litakuwa limetimia.  Ni wazi kuwa watu husoma maulidi ili kuonyesha hisia zao katika kumpenda Mtume wao. Hivi ndivyo anavyoweza kukuambia kila msoma maulidi.  Kwa hiyo utaona msingi wa maulidi ni kumpenda Bwana Mtume na kumpenda Mtume ni dini. Ni jambo aliloliamrisha Allah na Mtume wake, kwani imani ya mja haikamiliki ila kwa kumpenda Mtume.

Sasa basi, kutokana na mnasaba huu wa kuingia mwezi huu wa Rabiul-Awwal (Mfungo sita) ambamo waislamu huadhimisha maulidi ya Mtume wao, Website yako; WEBSITE UISLAMU inaungana na waislamu wote katika kusherehekea maulidi kwa kukuletea makala maalumu. Website yako inataraji utafaidika na makala haya na yatakusaidia kujua namna ya kusheherekea maulidi matukufu ya Mtukufu Mtume wako. Karibu uwe pamoja nasi katika makala:

 

TUMPENDEJE BWANA MTUME?

 

          Miongoni mwa “Qurubaati” (mambo ambayo mja huyafanya ili kujiweka karibu zaidi na Mola wake) ni kumpenda Mtume wake– Rehema na Amani zimshukie.  Hili ni jambo lisiloweza kunpigwa wala kukanushwa na ye yote miongoni mwa waislamu.  Na suala hili la kumpenda Mtume huambatana na alama kadhaa ambazo husadikisha ukweli wa madai ya wanaodai kumpenda Mtume wa Allah.  Miongoni mwa alama zinazoweza kuwa ni kigezo na kielelezo cha kumpenda Mtume ni pamoja na:

  1. Kigezo Chema:

Katika jumla ya alama kubwa zinazoonyesha mahaba ya mtu kwa Mtume wake ni kumfanya Bwana Mtume kuwa ndio kigezo pekee chake chema.  Na kumfanya Bwana Mtume kuwa ni kigezo, maana yake ni kumfuata katika yote aliyokuja nayo kutoka kwa Mola wake Mtukufu, miongoni mwa maamrisho na makatazo.  Ni kuushika mwendo wake na kuongozeka na muongozo wake.  Hivi ndivyo anavyotuambia Allah Mola Mwenyezi ndani ya kitabu chake kitukufu alichomteremshia Mtume wake: “SEMA IKIWA NYINYI MNAMPENDA ALLAH, BASI NIFUATENI (hapo) ALLAH ATAKUPENDENI NA ATAKUGHUFIRIENI MADHAMBI YENU NA ALLAH NI MWENYE MAGHUFIRA (na) MWENYE REHEMA (3:31)

Hapa Allah anafanya kumfuata Mtume wake kuwa ni alama ya mahaba ya mja kwa Mola wake. Kwa kumfuata Bwana Mtume–Rehema na Amani zimshukie–hupatikana mahaba mawili kwa pamoja. Mahaba ya mja kumpenda Mola wake na mahaba ya Mola kumpenda mja wake, kwani suala si kumpenda Allah tu bali hali ilivyo ni Allah kukupenda wewe.  Allah anatuambia juu ya hili: “...ATAWAPENDA NAO WATAMPENDA…” (5:54).  Lau Allah hakuwapenda waja wake, waja wasingeliweza kumpenda yeye na wala Allah hampendi mja mpaka amfuate Mtume wake kwa dhahiri na siri. Akamsadikisha kwa yale yote aliyoyaeleza, akamtii katika maamrisho na makatazo na akampenda zaidi kuliko kiumbe cho chote kiwacho.  Hivi ndivyo anavyotuambia Bwana Mtume Rehema na Amani zimshukie: “Haikamiliki imani ya mmoja wenu mpaka (mimi Mtume) niwe kipenzi zaidi kwake kuliko mzazi wake, mwanawe na watu wote”. Ahmad, Bukhaariy, Muslim, Nasaai Ibn & Maajah.

Akasema tena katika kauli nyingine: “Mambo matatu yatakayokuwa kwake, atapata (mtu huyo) utamu wa imani:

  1. Allah na Mtume wake kuwa ni vipenzi mno kwake kuliko wasio wawili hao, na
  2. Kumpenda mtu kwa ajili ya Allah tu, na
  3. Kuchukia kurudi ukafirini baada ya kuokolewa na Allah kutoka huko, kama achukiavyo kutupwa motoni”. Ahmad, Bukhaariy, Muslim, Tirmidhiy, Nasaai & Ibn Maajah.

Mja atapoonja utamu wa imani na kupata ladha yake, matunda ya imani hiyo yatadhihiri kupitia viungo na ulimi wake. Hapo ndipo ulimi wake utaiona tamu dhikri ya Allah kuliko tamu ya vitamu vyote ilivyopata kuvionja na viungo navyo vitaharakia katika twaa ya Allah. Hapo ndipo penzi la imani litaugubika moyo kama maji baridi yakiingiavyo kiu katika siku yenye joto kali kwa mtu mwenye kiu kikali kabisa. Taabu ya twaa humuondokea kwa kuionea kwake tamu, kwa hivyo basi twaa hubakia kuwa ndio chakula cha moyo wake. Na huwa ndio furaha ya kifua chake, burudani ya macho yake na neema ya roho yake.  Huiona ladha mno kuliko ladha za kiwiliwili kiasi cha kutoona taklifu wala kuhisi taabu katika suala zima la ibada. Na wala hakuna awezaye kupinga kwamba hakuna daraja tukufu na bora zaidi kuliko daraja ya kumfuata kipenzi Bwana Mtume–Rehema na Amani zimshukie. Kumfuata katika maamrisho na makatazo yake, matendo na tabia zake bali mwenendo wake mzima. Wala kamwe haitomuangazia ye yote nuru ya imani ila kwa kufuata sunah ya Mtume na kujiepusha na bidaa. Imepokelewa kutoka kwa Anas–Allah amuwiye radhi–akipokea kutoka kwa Mtume–Rehema na Amani zimshukie-kwamba yeye Mtume amesema: “...Na atakayeuhisha sunah (mwendo) yangu, kwa yakini huyo amenipenda”. Tirmidhiy

 

  1. Kumfanya Bwana Mtume kuwa ndio Hakimu:

Hii pia ni alama ya mahaba ya mtu kwa Mtume wa Allah–Rehema na

Amani zimshukie. Mwenye kudai kumpenda Bwana Mtume aridhie sheria ya Allah aliyoiteremsha kupitia ulimi wa Mtume wake iyatawale maisha yake yote. Bila ya kuwepo mwanya hata mdogo ambamo sheria hiyo ya Allah itakuwa haina nafasi, airidhie sheria hii kiasi cha kutoona uzito ndani ya nafsi yake kutokana na hukumu za Allah na Mtume wake.  Hivi ndivyo Allah Bwana Mlezi wetu anavyotuambia: “NAAPA KWA (haki ya) MOLA WAKO WAO HAWAWI WENYE KUAMINI (kweli kweli) MPAKA WAKUFANYE (wewe ndiye) HAKIMU (mwamuzi) KATIKA YALE WANAYOKHITALIFIANA, KISHA WASIONE UZITO NYOYONI MWAO JUU YA HUKUMU ULIYOTOA NA WANYENYEKEE KABISA”. (4:65)

Hapa Allah anaikanusha imani kwa mtu atakayeona uzito ndani ya nafsi yake kutokana na hukumu iliyotolewa na Mtume na akaacha kuinyenyekea na kusalimu amri kwayo. Kwa hivyo utaona imani ya kweli haipatikani ila kwa yule atakayemfanya Allah na Mtume wake kuwa ndio mahakimu wake. Hukumu zao zitawale nafsi na mali yake, kauli na matendo yake, kufuata na kuacha kwake, kupenda na kuchukia kwake bali maisha yake yote. Kisiwepo kipengele au nyanja yo yote ya maisha yake isiyotawaliwa na kuongozwa na hukumu (sheria) za Allah na Mtume wake. Kisha Allah hakutosheka tu na kuikanusha imani ya asiyemfanya Bwana Mtume kuwa ndio Hakimu wake, bali akaliapia hilo kwa kauli yake: “NAAPA KWA (haki ya) MOLA WAKO. WAO HAWAWI WENYE KUAMINI (Kweli kweli) MPAKA WAKUFANYE (wewe ndiye) HAKIMU (mwamuzi) KATIKA YALE WANAYOKHITALIFIANA…”

Kiapo hiki cha Allah Mola Muumba mbingu na ardhi na vyote vilivyomo ikiwa kinaashiria jambo, basi haitakuwa ila ni kudhihirisha sharafu ya Mtume na jinsi Mola wake anavyomjali. Hili linajionyesha wazi pale Allah alipoifanya hukumu itayotolewa na Mtume wake ndio hukumu yake yeye Allah na twaa ya Mtume ndio twaa yake yeye.  Kisha akawawajibishia waja wake kusalimu amri kwa hukumu ya Mtume wake na kuifuata, kwani Mtume ni kama alivyomsifu Mola wake: “WALA HASEMI KWA MATAMANIO (ya nafsi yake). HAYAKUWA HAYA (anayosema) ILA NI WAHYI (ufunuo) ULIOFUNULIWA (kwake)”.  (53:3-4)

Kwa mantiki hii ya aya, hukumu ya Mtume inakuwa ndio hukumu ya Allah. Na huku kumfanya Mtume kuwa ndio Hakimu wa muumini katika yote na vyote ni katika zama zote na mahala po pote.  Ye yote ambaye hakumridhia Bwana Mtume kuwa ndio Hakimu wake, huyo bila ya shaka ye yote ni KAFIRI na amejitoa yeye mwenyewe katika Uislamu. Allah anatutangazia: “MWENYE KUMTII MTUME AMEMTII ALLAH (kwani anayoyaamrisha yametoka kwa Allah). NA ANAYEKENGEUKA (anajidhuru mwenyewe)…” (4:80)

 

  1. Kukithirisha kumtaja Bwana Mtume:

Miongoni mwa alama zinazoonyesha mahaba ya mtu kwa Mtume wa Allah–Rehema na Amani zimshukie-ni kukithirisha kumtaja. Kwani mtu akipendapo kitu hukithirisha kukitaja, yaani hukitaja mara kwa mara. Kumtaja kwake Mtume kuambatane na taadhima, kudhihirisha unyenyekevu na kujiweka chini yake.  Hii ni kwa sababu kimaumbile mtu akipenda kitu hukinyenyekea na kukitii. Hivi ndivyo walivyokuwa wengi miongoni mwa maswahaba Allah awawiye radhi–wanapomtaja Bwana Mtume hunyenyekea,  nyoyo na ngozi zao (miili) husisimka  na wakalia kwa mahaba na shauku. Kwa hivyo basi inamuwajibikia kila muumini wakati anapomtaja Bwana Mtume–Rehema na Amani zimshukie–au anapotajiwa aonyeshe utii na kujiweka chini yake na aione haiba na utukufu wake kama kwamba huyo hapo Mtume amesimama mbele yake. Hizi ndizo mizani tatu; kumfuata Mtume, kumfanya Hakimu na kumuadhimisha, mizani za kupimia mahaba ya mtu kwa Mtume wa Allah.  Atakayeyakuta mambo matatu haya nafsini mwake basi na amuhimidi Allah na kama hana basi na atake maghfira na atubie kwa Mola wake. Hebu sasa tuangalie ni namna gani wenzetu walivyompenda kidhati Bwana Mtume–Rehema na Amani zimshukie:

v     Abdullah Ibn Zubayr–Allah amuwiye radhi-alikuwa anapotajwa Mtume mbele yake, hulia mpaka akaishiwa na machozi; yakawa hayatoki tena.

v     Ja’afar Ibn Muhammad alikuwa mwingi wa mzaha na tabasamu, anapotajiwa Bwana Mtume hapo hapo rangi yake hupiga manjano na hali yake hubadilika.

v     Abdur-rahman Ibn Qaasim, alikuwa anapotajwa Mtume wa Allah, huangaliwa rangi yake na kuonekana kama mtu aliyetokwa na damu. Ulimi kinywani umekauka kutokana na haiba ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie.

Hivi ndivyo waja hawa wa Allah, wanadamu kama sisi walivyomuweka Mtume wa Allah, unyenyekevu na utii wao huu kwa Mtume hata wawapo mbali nae ukawapa nafasi ya kuwa karibu na Mtume.  Na ni ukweli usiopingika kwamba ye yote aliye karibu na Mtume huyo ameshafuzu duniani .  Hii ni kwa sababu kuwa karibu na Bwana huyu ni kuwa karibu na Allah ambaye: “ALIYEMTUMA (aliyemleta) MTUME WAKE KWA UWONGOFU NA DINI YA HAKI, ILI AISHINDISHE JUU YA DINI ZOTE….”  (48:28)

 

ALAMA NYINGINE ZA MAHABA YA MTUME.

 

                                      I.     Kufurahishwa na misiba:

Hili pia ni miongoni mwa vielelezo vya mahaba ya mtu kwa Mtume wa Allah. Mtu anayedai kumpenda Bwana Mtume utamuona anaposibiwa na misiba/majanga ambayo ni sehemu ya maisha, hapapatiki wala kubabaika.  Na badala yake huionea furaha misiba hiyo, kwa sababu mpenzi wa Mtume huona ladha katika kumpenda kwake Bwana huyu kiasi cha kumsahaulisha na kutompa nafasi ya kukumbuka uzito na uchungu wa misiba iliyomsibu. Huyu haguswi na misiba kama wanavyoguswa watu, vipi basi iwe hivyo na il-hali saa zote yu na kipenzi chake Bwana Mtume ambaye tayari ameshamfundisha akabiliane vipi na misiba.  Huyu anakuwa kama kwamba kavikwa tabia na umbile jingine lisilo la kawaida.  Hawa ndio wale ambao anafiwa na mwanawe, watu wanaenda kuzika yeye anabaki akigawa mirathi ya kipenzi chake, anasomesha elimu.

 

                                  II.     Kupenda kukutana nae:

Mtu mwenye kumpenda kidhati Bwana Mtume–Rehema na Amani zimshukie-huwa na shauku kuu ya kukutana nae. Maswahaba Allah awawiye radhi–walipozidiwa na shauku ya kumuona Bwana Mtume, walimkusudia khasa (walimuendea) wakahisi raha mno kwa kule kumuona tu na kuponywa shauku yao.  Wakazidi kuona raha na tamu kwa kukaa pamoja nae huku wakimuangalia na kutabaruku nae.  Huku ndiko kumpenda Mtume wa Allah kweli kweli.

 

                               III.     Kuipenda Qur-ani:

Katu mtu hawezi kudai kumpenda Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-wakati haipendi Qur-ani aliyomletea kutoka kwa Allah. Ukitaka kuyajua mahaba yako kwa Bwana Mtume, basi yaangalie kwanza mahaba ya Qur-ani tukufu moyoni mwako na jinsi unavyoona raha kwa kuisikiliza. Je, unaionea ladha na tamu Qur-ani kuliko unavyozionea tamu nyimbo na taarabu wakati unapozisikiliza? Imepokelewa kutoka kwa Sayyidna Uthmaan Ibn Affan–Allah amuwiye radhi–kwamba yeye amesema:  “Lau nyoyo zetu zingetwaharika zisingeshiba maneno ya Allah”.

 

                               IV.     Kupenda Sunah yake:

Mtu mwenye kudai kumpenda Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-ni lazima aipende sunah yake na kuzisoma hadithi zake sambamba na kuzifanyia kazi. Kwani mtu ambaye utamu wa imani umepenya moyoni mwake, akilisikia neno moja tu miongoni mwa maneno matukufu ya Allah au katika hadithi za Mtume wake, moyo, roho na nafsi yake hulinywa na kulimeza neno hilo hapo hapo.

 

          Yeyote atakayejipamba na kusifika na alama hizi tulizozidhukuru, basi mtu huyo ni mkamilifu wa mahaba kwa Allah na Mtume wake.  Na huyu ndiye ana kila sababu za kuyasherehekea maulidi. Ama yule atakayezikhalifu baadhi ya alama, akawa hanazo, basi huyo ni mpungufu wa mahaba.  Lakini yumo mahabani na wala hatoki, hili linatokana na kauli yake Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie- kwa yule mtu aliyemtia adabu (haddi) kwa sababu ya kunywa pombe.  Baadhi ya maswahaba walimlaani na kusema: Ee nae kazidi, kila mara kosa hilo hilo tu! Bwana Mtume akasema: “Msimlaani kwani hakika yeye anampenda Allah na Mtume wake”.

 

Kwa kukhitimisha makala yetu haya, hebu sasa tutazame:-

 

PICHA ZA WALIOMPENDA KWELI MTUME WA ALLAH:

 

q       MWANAMKE WA KIANSWARI.

Imepokewa kwamba mwanamke mmoja wa Kianswari aliuliwa baba, kaka na mumewe siku ya vita vya Uhud, walikokwenda kupigana pamoja na Mtume wa Allah–Rehema na Amani zimshukie.  Watu walipokuwa wanarudi vitani aliwakimbilia na kuwauliza: Yukoje Mtume wa Allah? Wakamjibu: Bukheri wa afya kwa himda za Allah kama upendavyo.  Akawaambia: Hebu nionyesheni nimuone, alipomuona akasema: Kila msiba ni mwepesi kwangu ila msiba wako tu, ewe Mtume wa Allah.

 

q       THAUBAAN HURU WA MTUME.

Imamu Baghawiy–Allah amrehemu–amesema katika tafsiri yake kwamba kauli ya Allah Mtukufu: “NA WENYE KUMTII ALLAH NA MTUME, BASI HAO WATAKUWA PAMOJA NA WALE ALIOWANEEMESHA ALLAH: MANABII NA MASADIKI NA MASHAHIDI NA MASALIH (Watu wema) NA UZURI ULIOJE (kwa mtu) WATU HAO KUWA RAFIKI (zake)”.  (4:69)

Imeshuka kwa ajili ya Thaubaan, huru wa Bwana Mtume–Rehema na Amani zimshukie. Huyu alimpenda mno Bwana Mtume, alikuwa hajiwezi kabisa kwake.  Siku moja alimuendea Bwana Mtume na il-hali rangi yake imebadilika, huzuni ikionekana usoni mwake. Mtume wa Allah akamuuliza: “Ni kipi/lipi lililoibadilisha rangi yako?” Akamjibu: Ewe Mtume wa Allah! Mimi sina maradhi wala maumivu yo yote, ili tu mimi nisipokuona hujiona mpweke mno mpaka nikutane nawe.  Kisha ninakumbuka akhera na nikachelea kutokukuona huko kwa sababu wewe utanyanyuliwa pamoja na mitume wenzio katika daraja za juu peponi.  Nami hata nikiingia peponi nitakuwa katika daraja ya chini yako na kama sitaingia peponi ndio sitakuona kabisa (na mimi maradhi yangu ni kukuona wewe) ndipo ikashuka aya hii.

 

q       ABDULLAH IBN ZAYD:

Huyu alikuwa kiungani  mwake  akijishughulisha  na kazi za  shamba. Mara  mwanawe  wa  kiume akamjia na kumpa  khabari za  kifo cha  Bwana Mtume–Rehema na Amani zimshukie. Akasema  baada ya  kusikia khabari hiyo ya  huzuni: Ewe Mola wa haki  wee! Nakuomba  uniondoshee  uoni wangu ili nisiweze kumuona  yeyote    baada ya kufa  kipenzi changu  Muhammad. Allah akaikubali dua yake, naam  uoni  wake  ukaondoshwa–Allah amuwiye radhi.

 

q       KAULI YA ANAS IBN MAALIK :

Imepokelewa kwamba  mtu  mmoja alimuendea  Bwana Mtume–Rehema  na Amani zimshukie-akamuuliza: Ewe Mtume wa Allah! Kiyama kitakuwa   lini? Mtume  akamuuliza: “Umekiandalia nini  hicho kiama    (unachokiuliza )?” Yule  mtu akamjibu  Mtume: Sikukiandalia wingi wa swala, swaumu  wala sadaka, lakini tu mimi ninampenda Allah   na Mtume  wake. Kusikia kauli  yake hii, Bwana  Mtume akamwambia:       “ Wewe  utakuwa  pamoja  na   umpendaye”. Kisha Anas; khadimu  wa Mtume nae akasema:  “Kwa  yakini mimi ninampenda Mtume  wa Allah,  Abuu  Bakri  na Umar na ninataraji  kuwa pamoja  nao peponi”.

 

q       MUHABESHI  BILALI :

Huyu hapa ndiye Bilali muadhini wa Mtume  wa Allah–Rehema na Amani zimshukie. Ameishi  katika kumpenda Bwana Mtume tangu siku  aliposilimu  mpaka   anaingia kaburini. Alipokufa aliwasikia  baadhi ya watu wake wakilia na kusema: Ee  huzuni iliyoje! Tahamaki kwa mshangao wa  wengi Bilali (maiti) amefungua  macho yake akitabasamu na kusema: Ee furaha iliyoje, kesho tunakutana  na kipenzi Muhammad na kundi lake. Allah  amuwiye radhi Bilali.

 

q       UMMU HUDHAYFAH:

Huyu ndiye Hudhayfah Ibn Al–Yamaan–Allah  amuwiye radhi–anaulizwa na mama yake: Ewe  mwanangu! Lini  ulionana   na Mtume wa Allah-  Rehema na Amani zimshukie? Akamjibu: Siku  tatu zilizopita. Mama yake  akamgomba na  kumwambia: Vipi  unaweza kusubiri ewe  Hudhayfah  kutokumuona Mtume  wako kwa kipindi chote   hicho cha siku tatu? Hudhayfah  akamwambia  mama  yake: Ewe mama yangu niache nimuendee  Mtume niswali nae Magharibi kisha nimuombe  anisamehe mimi na wewe. Hudhayfah anasema:  Nikaenda  nikaswali  Magharibi pamoja na Mtume,  Mtume  akaendelea kuswali (swala zake za Sunah)  mpaka ukaingia  wakati wa swala ya  Ishaa. Akaswali Ishaa kisha akaondoka kuingia nyumbani  mwake nami  nikamfuatia nyuma yake.  Mtume  akasikia sauti yangu, akauliza: Nani huyo? Ni  Hudhayfah?” Nikasema: Naam (ndiye). Akauliza  tena: “Una haja gani?” Allah ameshakusamehe  wewe na mama  yako. Huu  ni muujiza wa dhahiri wa Mtume  wa Allah, anamueleza mtu yaliyomo moyoni  mwake  kabla hata hajamueleza–Allah akurehemu  ewe Mtume wa Allah .

 

q       ZAYD  IBN DATHINAH :

Mushrikina walimteka Zayd  na wakamtoa  ili  wamuue, wamwambia: Ewe Zayd tunakuonea  huruma kwa mapenzi ya  Allah, je wewe unapenda  Muhammad awe katika nafasi yako hii,  tuipige  upanga shingo yake nawe  uwe  kwa  watu wako nyumbani? Zayd  akacheka  na kuwaambia: Wallah, mimi sipendi  Muhammad hapo  alipo sasa (wacha hapa) achomwe  hata  na mwiba tu,  nami    eti niwe nimekaa nyumbani  (raha mustarehe) na wake zangu  na watoto. Abuu Sufyaan  wakati huo akiwa bado   kafiri akasema:  Wallah, sijapatapo kumuona ye yote  akimpenda  mtu kama  maswahaba wa Muhammad wampendavyo Muhammad.

 

NENO KHITAAM:

          Tambua  na ufahamu ewe ndugu muislamu-Allah akurehemu– kwamba kumpenda Mtume  wa Allah ni daraja ambayo wenye kushindana  huishindania. Mahaba ya Mtume ni chakula cha  nyoyo  na  roho na burudani ya   macho. Mahaba ya   Mtume ni  uhai, atakayenyimwa uhai huu, basi huyo ni katika  jumla ya wafu. Mahaba ya  Mtume ni  nuru, atakayeikosa nuru hiyo  huyo  yumo  katika bahari za viza. Mahaba ya  Mtume  ni roho ya imani, ni roho ya amali (matendo)  na  ni roho ya hali  na makamu yote. Kwa ujumla,  moyo wa mja hauna uhai ila kwa kumpenda   Allah na Mtume wake. Na wala hapana maisha  kama maisha ya wenye kumpenda Bwana Mtume,  macho yao  yakatua kwa kipenzi chao, nafsi zao  zikatulizana kwake na  nyoyo zao zikapata  utulivu kwake. Wakaliwazika kwa kuwa nae  karibu na wakaneemeka na mahaba yake.  Nyoyoni  mwao mna nguvu ya ajabu isiyoweza  kuzuiliwa  ila na mahaba ya Allah  na Mtume  wake. Asiyebahatika  kuyapata mahaba haya,  huyo maisha yake yote ni taabu,  mashaka, huzuni, masumbuko, shida, uchungu na majuto.

          Naam ndugu muislamu, haya  kwa mukhtasari ndio mahaba ya Mtume. Hebu wakati  ukiyasherehekea maulidi  ya Bwana  huyu, jikague:-

ü      Je , kweli wewe una mahaba ya Mtume?  Kama ndivyo kisha jiulize,

ü      Je , inawezekana kweli kwa mwenye kumpenda  Mtume kuacha swala, swaumu, zakah, kusema  uongo kutoa  na kupokea rushwa, kufitinisha, kuhusudi, kuwatupa wazazi, ndugu, jamaa,  mayatima na masikini, kuacha kutafuta  elimu na ---- na----?!

Mwisho kabisa Website yako (WEBSITE   UISLAMU)   inakuomba tuombe pamoja: EWE  MOLA WA HAKI WEE! TUNAKUOMBA UTUJAALIE  MAHABA YAKO NA MAHABA YA MTUME WAKO  YAPENDEZE  ZAIDI KWETU SISI WAJA WAKO KULIKO  VITU VYOTE. KULIKO HATA MAJI YA  BARIDI   YAPENDEZAVYO KWA KIU – Aaamiyn!

 

Tunawatakia waislamu wote popote walipo  heri, fanaka, furaha na baraka ya Maulidi. Maulidi njema kwenu nyote!

Waalaam Alaykum Warahamatullah                    

Mtumishi  wa   umma,

WEBSITE  UISLAMU.

 

 


TUJIFUNZE NA TUKUBALI: Upofu si kupofua macho bali  upofu khasa ni mtu kupofua akili na moyo. Tusome tukipenda: “...KWA HAKIKA MACHO HAYAPOFOKI LAKINI NYOYO AMBAZO ZIMO VIFUANI NDIZO ZINAZOPOFUA (zikadhuru katika dini)”. [22:46]


Forum | Guestbook | Tuandikie |