|
Kunamkinikia
mtu aliyeruzukiwa taufiq ya kuutumia vema wakati wake, kuurefusha umri
wake na kuupanua mpaka apatakapo Allah hata baada ya kufa kwake.
Akaendelea kuwa hai na ilhali amekufa, hili litawezekana tu ikiwa atakuwa
ameacha nyuma yake kitakachoendelea kuinufaisha jamii. Akaacha elimu yenye
manufaa inayowasaidia watu katika utendaji wa maisha yao ya kila siku. Au
akamuacha mtoto mwema atakayemnufaisha yeye na jamii yake kutokana na
matendo yake mema. Au akaacha athari njema au mwendo mwema utakaoigwa na
kuendelezwa na waliobakia nyuma. Au akaasisi jambo la hisani na ufadhili
litakaloendelea kutoa matunda baada ya kufarikiana kwake na ulimwengu huu.
Haya yanatokana na kauli ya Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie: “Afapo
mwanadamu, thawabu za amali zake zote njema hukatika ila (thawabu za)
mambo matatu:
1.
sadaka yenye kuendelea, au
2.
elimu yenye kunufaisha, au
3.
mtoto mwema
atakayemuombea Mungu”.
Muslim
Na
katika hadithi nyingine iliyokusanya mambo mengine zaidi ya mambo matatu
haya, Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-anasema: “Hakika
miongoni mwa amali (matendo) mema
yake yanayomfuata baada ya kufa kwake (ni pamoja na)
1.
elimu aliyoifundisha na kuineza, au
2.
mtoto mwema aliyemuacha, au
3.
msahafu aliourithisha, au
4.
msikiti alioujenga, au
5.
nyumba ya wasafiri (walioharibikiwa), au
6.
kisima alichokichimba, au
7.
sadaka
aliyoitoa katika mali yake katika uhai na uzima wake, itakayomfuata baada
ya kufa kwake”.
Ibn Maajah & Al-Baihaqiy-Allah awarehemu.
Mtume
wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-akasema tena: “Ye yote atakayeanzisha
suna (mwendo) njema, basi utamthibitikia ujira wake na ujira wa
watakaomfuata (watakaoifanyia kazi suna hiyo) mpaka siku ya kiyama”.
Muslim
Hivi
ndivyo Qur-ani Tukufu inavyosema kuhusiana na athari ya amali baada ya
mauti: “KWA YAKINI SISI TUTAWAHUISHA WAFU NA TUNAZIANDIKA (amali zao
wanazozifanya zisiwache) TAATHIRA NYUMA NA (zile wanazozifanya zikawacha)
TAATHIRA ZAO (nyuma)...”. [36:12] Ikasema tena: “SIKU HIYO
ATAAMBIWA MWANADAMU ALIYO YATANGULIZA (yasiache athari) NA
ALIYOYAAKHIRISHA (yakaacha athari)”. [75:13]
Wanazuoni
wanakongamana na kuwafikiana kwamba utajo mwema anaouacha mwanadamu baada
ya kufa kwake. Huzingatiwa kuwa ni umri wake mwingine usio na mpaka baada
ya umri ule wenye mpaka. Hili ndilo aliloliomba baba wa mitume; nabii
Ibrahim-Amani imshukie: “NA UNIJAALIE KUTAJWA KWA WEMA NA WATU
WATAKAOKUJA BAADAYE”. [26:84]
Kuna
tofauti kubwa ya dhahiri baina ya mtu anayekufa na ilhali nyoyo
zinahuzunika juu yake, macho yanabubujika machozi kwa ajili yake na ndimi
zote zinamsifia kwa sifa njema na kumuombea rehema. Na yule anayekufa
pasipatikane hata jicho la kumtolea machozi, usihuzunike moyo kwa
kufarikiana naye na wala ndimi zisimuombee rehema. Hii ndio hali ya watu
walioishi katika ulimwengu huu na kujifanya miungu wanaoabudiwa na
kutukuzwa, wakiwanyanyasa wanadamu wenziwao na kuwadhulumu. Hii ndio aina
ya watu anaowataja mshairi katika ubeti wake:-
Huyo ndiye ambaye akiishi hana manufaa * Na akifa hawamuhuzunikii
zake jamaa (seuze watu kando)!
Hawa
ndio walengwa wa kauli tukufu ya Allah: “MABUSTANI MANGAPI NA CHEMCHEM
NGAPI WALIZIACHA (baada ya kugharikishwa) NA MIMEA NA MAHALI PAZURI NA
NEEMA (kubwa kubwa) WALIZOKUWA WAKIJISTAREHESHA. NAMNA HIVI (tumewafanya)
NA TUKAWARITHISHA HAYA WATU WENGINE. MBINGU NA ARDHI HAZIKUWALILIA
(walioko ardhini hawakuwalilia wala walioko mbinguni kwani walikuwa watu
wabaya). WALA HAWAKUPEWA MUDA (wa kurejea tena ulimwenguni)”.
[44:25-29]
Mara
nyingi wanapokufa watu waovu wa namna hii, hayafi pamoja nao madhambi na
dhuluma zao au ukafiri na upotofu wao. Bali huwarithisha mabaya haya
wafuasi wao ambao huzifuata nyayo zao. Ikiwa kwa mujibu wa maneno ya
Mtume-Rehema na Amani zimshukie-ye yote mwenye kuasisi suna njema, atapata
ujira wa suna hiyo na ujira wa watakaoifanya kazi/suna hiyo mpaka siku ya
kiyama. Hali kadhalika mwenye kuasisi suna mbaya, yatamthibitikia madhambi
yake suna hiyo na madhambi ya watakaomfuata katika kuitenda na kuiendeleza
suna/mwenendo huo mbaya ulioasisiwa nae. Na kama ambavyo mtu akiacha nyuma
yake elimu yenye manufaa, ujira wa amali yake hiyo njema haukatiki. Basi
hali ni kama hiyo kwa mtu atakayeacha athari mbaya na fikra potevu, ujira
wa amali yake hiyo mbaya utaendelea kumfuata huko kaburini aliko hadi kule
akhera. Hili ndilo lililowafikisha waja wema wa Allah-Allah
awarehemu-kusema: (Furaha na raha
iliyoje kwa yule anayekufa na yakafa pamoja nae madhambi (maovu) yake. Na
adhabu kali (ole wake) yule aliyekufa na ilhali maovu yake yako hai baada
yake).
TAHADHARI NA
MAJANGA YENYE KUANGAMIZA WAKATI WAKO...IX
Baada
ya kutambua na kufahamu umuhimu na thamani ya wakati na namna bora ya
kuitumia rasilimali hii kuu. Hebu sasa kwa msaada wa Allah Mola Mjuzi wa
kila kitu, tujaribu kuyaangalia mambo yanayoweza kuwa ni majanga
yanayouangamiza wakati wa mwanadamu. Kwa hakika yako maafa mengi ambayo
kwa namna moja au nyingine yanaweza kuwa ni chanzo cha kuuangamiza wakati
wa mwanadamu na kumuacha bila ya kunufaika nao. Iwapo mtu hatazinduka
mapema atajuta wakati ambapo majuto yake hayo hayatamnufaisha kwa cho
chote, kwani umri (wakati) uliopotea hautarudi tena. Miongoni mwa maafa ya
wakati ni kama yafuatavyo:-
I.
MGHAFALA:
Haya
ni aina ya maradhi yanayoisibu akili na moyo wa mwanadamu. Maradhi haya
humuondoshea mwanadamu nguvu hisia ambazo hufanya kazi ya kuhifadhi,
kuchambua na kuzingatia mambo. Kukosekana kwa nguvu hisia hizi humaanisha
kukosekana kwa mzinduko angavu wa maana na matokeo mwisho ya vitu/mambo.
Kwa mantiki hii basi mkosa nguvu hisia huhusika na vitu/mambo kwa njia ya
picha tu ya macho na si kwa njia ya maana inayomfanya aone na kusikia kwa
moyo. Huyaangalia mambo kwa dhahiri tu na si kwa hakika ya maumbile yake.
Huyaona maganda ya mambo na si kokwa ya ndani na uoni wake hukoma katika
kuangalia mwanzo wa mambo na si mwisho wake. Qur-ani Tukufu
inawatahadharisha sana waislamu na maradhi haya mabaya ya mghafala.
Qur-ani imekwenda kina sana kiasi cha kuwafanya wana mghafala kuwa ni kuni
za jahanamu na kuwa ni wapotevu kuliko hata wanyama wasio na akili. Hebu
na tuizingatie kwa pamoja aya hii tukufu: “NA BILA YA SHAKA
TUMEWAUMBIA MOTO WA JAHANAMU WENGI KATIKA MAJINI NA WANADAMU (kwa sababu
hii): NYOYO WANAZO LAKINI HAWAFAHAMU KWAZO, NA MACHO WANAYO LAKINI HAWAONI
KWAYO. NA MASIKIO WANAYO LAKINI HAWASIKII KWAYO. HAO NI KAMA WANYAMA,
BALI WAO NI WAPOTEVU ZAIDI, HAO NDIO WALIOGHAFILIKA”. [7:179]
Allah
anamkhutubu Mtume wake-Rehema na Amani zimshukie-anasema: “NA MTAJE MOLA
WAKO MOYONI MWAKO KWA UNYENYEKEVU NA KHOFU NA BILA YA KUPIGA KELELE KATIKA
KAULI (yako hiyo, mkumbuke Mola wako umtaje) ASUBUHI NA JIONI, WALA
USIWE MIONGONI MWA WALIOGHAFILIKA”. [7:205] Na katika aya nyingine
akamwambia: “...WALA USIWATII WALE AMBAO TUMEZIGHAFILISHA NYOYO ZAO
WAKAFUATA MATAMANIO YAO NA MAMBO YAO YAKAWA YAMEPITA MIPAKA (yaani
makafiri)”. [18:28]
Ee
balaa adhimu iliyoje kwa jamii kupitiwa na matukio yanayoyatetemesha
majabali, lakini jamii hiyo haiyazingatii na wala haibadilishwi na matukio
hayo. Matukio kwao ni mithili ya mchezo wa kuigiza na si uhalisia wa
mambo.
|