|
Kama inavyotupasa kuziangalia zama za kisogoni (zilizopita), hali
kadhalika imetupasa kuzitupia jicho zama za usoni (zijazo), leo. Ni
dhahiri kuwa maumbile ya
mwanadamu yamefungamana zaidi na mustakbali wake kuliko zama zake
zilizopita. Mtu mwenye akili timamu hawezi kabisa kughafilika na
mustakbali wake. Kama ambavyo
alivyopewa mwanadamu kumbukumbu zinazomsaidia kumuunganishia leo yake na
yaliyopita. Katika mkabala wa
hilo akapewa uwezo wa kuwazia mambo asiyoyaona ili umsaidie kusawirisha na
kumpa picha ya mustakbali wake na yanayotazamiwa ndani yake.
Miongoni mwa sifa na tabia za mustakbali ni kuwa kwake ghaibu
(Hidden/unseen) na majuhuli (unknown). Hakuna ye yote ajuaye ni lipi
litamtokea kwa hakika na ni kheri au shari ipi imjongeleayo.
Hivi ndivyo Allah Mola Muumba wetu anavyotuambia: “….NA
NAFSI YO YOTE HAIJUI NI NINI ITACHUMA KESHO, WALA NAFSI HAIJUI ITAFIA
ARDHI GANI. BILA SHAKA ALLAH NDIYE MJUZI (ndiye) MWENYE KHABARI (ya
mambo yote)” (31:34)
Sifa nyingine ya mustakbali ni kuwa kila kijacho ndani yake, basi
hicho ki karibu ajapodhania mwanadamu kuwa ki mbali au kinachelewa. Hii ndio sababu pakasemwa na wenye busara waangaliao mambo
kwa uhalisia wake (kesho i pamoja na leo na kesho kwa mwenye kuitazamia
i karibu) Allah anatuambia ndani ya Qur-ani Tukufu kuhusiana na kiyama
ambacho mwanadamu anakiona kuwa ki mbali: “…WALA HALIKUWA HILO JAMBO
LA (kufika) SAA (ile ya Kiyama) ILA NI KAMA KUPEPESA JICHO AU NI KARIBU
ZAIDI…” (16:77)
Mwenye akili timamu ni yule anayefanya maandalizi ya mustakbali
wake leo na kujitayarisha kwa jambo kabla ya kutokea kwake. Hivi ndivyo
Allah anavyotuasa kwa njia ya amri: “ENYI MLIOAMINI! MCHENI ALLAH NA
KILA MTU AANGALIE (atazame) ANAYOYATANGULIZA KWA AJILI YA KESHO (Akhera/maisha
ya mbeleni)”… (59:18)
Wale wenye dhana na fikra potofu kwamba dini inamdunisha na
kumuweka nyuma mwanadamu kwa sababu inamfungamanisha na yaliyopita na
kumalizika. Hawa ni walemavu
wa akili na fikra zao pia ni lemavu kama wao wenyewe.
Wameshindwa kufahamu johari na hakika ya dini ni kumuandaa
mwanadamu na maisha ya milele; maisha ya mustakbali wake.
Maisha ya nyumba ambayo hiyo ni bora na yenye kusalikia milele
kuliko nyumba aliyomo hivi sasa (dunia).
Nadharia ya mustakbali ni nadharia ya msingi
katika nguzo/shina la dini. Imethibiti
katika hadithi kwamba: “Hakika mja yu baina ya khofu mbili: Baina ya
muda uliopita ambao hajui Allah atamfanya nini katika muda huo na muda
uliosalia ambao hajui Allah atamuhukumia nini ndani yake.
Basi na ajitwalie kutokana na nafsi yake kwa manufaa ya nafsi yake.
Na achukue duniani kwake kitachomfaa katika akhera yake.
Na achukue cha kumfaa ujanani kabla ya ukongwe. Namuapia yule
ambaye nafsi yangu i mikononi mwake, hakuna baada ya mauti wa kumlaumu. Na
wala hakuna nyumba nyingine baada ya dunia ila ni pepo au moto.”
Hii haimaanishi kwamba mwanadamu haushughulikii ila mustakbali wake
wa akhera tu basi na aache kuungalia mustakbali wake katika dunia hii
aishimo. La hasha, hayo siyo
makusudio na muradi wa Uislamu katika aya na hadithi tulizozitaja.
Hii ni kwa sababu Uislamu umemfundisha muislamu kuizengea kesho
yake (mustakabali) kwa kuifanyia maandalizi kwa kupitia sababu (njia)
zitakazomsaidia kuithibitisha ndoto yake kuielekea kesho yake.
Hii ni bila ya kuangalia na kuibagua kesho yake hiyo katika matapo
mawili; ya kidunia na ile ya kiakhera.
Ikiwa tunakubali kwa mujibu wa imani yetu kwamba Bwana Mtume ndio
kigezo kikuu cha kuigwa na waumini wote.
Hebu muangalie anavyoutafuta mustakbali wa ujumbe wake (da’awah)
wakati makabila mawili ya Madinah Ausi na Khazraji yalipompa kiapo/ahadi
ya uaminifu na utii. Akafikiria suala la Hijrah ambayo ilimgharimu kuuacha
mji aliozaliwa na kuuzoea kwa
ajili tu ya kusimamisha sheria na jamii ya Kiislamu. Yote haya hayakuwa
ila ni mikakati iliyopangwa barabara ya mustakbali wa Uislamu. Na katika
masuala ya kidunia tunamkuta Mtume wa Allah– Rehema na Amani zimshukie–akiiwekea
familia yake akiba ya chakula cha mwaka mzima. Wala hakuona kwamba hili
linapingana na kadhia ya kumtegemea Allah.
HAJA
YA KUJISHUGHULISHA NA LEO (ZAMA AISHIMO MTU).
Iwapo imemlazimu mwanadamu kusita na kufanya kituo pamoja na zama
zilizopita. Kituo ambamo
atautupia jicho wakati uliopita, akayazingatia matukio yaliyopita
akafaidika nayo na kuikagua nafsi yake. Kama ilivyompasa kuungalia
mustakbali wake na kuufanyia maandalizi. Haya yote hufanyka leo, yaani ndani ya zama aishizo mwanadamu.
Kwa mantiki hii basi, kumemuwajibikia mwanadamu huyu kuipa umuhimu maalum
na wa upendeleo leo yake. Anufaike nayo kabla haijamponyoka na kumpotea
asiipate tena kwani tayari itakuwa imeshakuwa jana.
JINSI
GANI MWANADAMU ANAWEZA KUUREFUSHA UMRI WAKE?
Si jambo la kutiliwa shaka kwamba kimaumbile mwanadamu ni kiumbe
apendaye kuishi na anapenda umri mrefu bali kuishi milele kama
angeliweza. Qur –ani Tukufu inalithibitisha umbile hili kupitia
kwa Mayahudi: “NA UTAWAONA (Mayahudi) WANA HAMU KUBWA YA KUISHI
KULIKO WATU WENGINE, NA KULIKO WALE WAMSHIRIKISHAO ALLAH (wasioamini
Akhera); KILA MMOJA KATIKA WAO ANAPENDA APEWE UMRI WA MIAKA ALFU….” (2:96)
Mlango
huu wa maumbile; maumbile ya kupenda kuishi milele ndio alioingilia
Ibilisi kwa baba yetu Adamu. Akamghuri, akala katika matunda ya mti
aliokatazwa kuyala: “(Lakini) SHETANI ALIMTIA WASIWASI (alimchokoachokoa)
AKAMWAMBIA: EWE ADAMU, JE! NIKUJULISHE MTI WA MILELE NA WA UFALMEUSIOKOMA?
BASI WAKAULA WOTE WAWILI (Adamu na Hawa) ….”
(20:120-121)
Dini
ya Kiislamu kwa dhati yake inauzingatia umri mrefu kuwa ni neema
utakapotumiwa
katika kuinusuru haki na kutenda amali njema.
Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-aliulizwa ni mtu yupi aliye
bora kuliko watu wote? Akajibu kwa kusema: “Mtu uliyekuwa mrefu umri
wake na yakawa mema matendo yake”. Tirmidhiy, Twabaraaniy,
Al-Bihaqiy & wengineo.
Kwa
upande mwingine ni jambo lisilo na shaka kwamba mauti huja ghafla na
kumpokonya mwanadamu matumaini na mapenzi yake haya ya kuwa na umri mrefu.
Mauti ndio mwisho wa mizunguko na uhai wa mwanadamu katika ulimwengu huu
wa muda mfupi. Ni jambo
lisilopingika kwamba umri ni mfupi sana usiokidhi mipango na matumaini ya
mwanadamu. Kila afaye huwa
hajakamilisha mambo na mipango yake aliyojipangia. Hili linatokana na
ukweli kwamba uhai ni siku chache tu, ni pumzi kidogo tu zinazokatishwa na
mauti bila hata ya kubisha hodi au kutoa taarifa. Bwana-Mtume Rehema na
Amani zimshukie-anasema:
-
“Ishi
utakavyoishi (lakini tambua) hakika wewe utakufa, na
-
Mpende
umpendaye/kipende ukipendacho, hakika utafarikiana (utatengana) nacho
(siku moja), na
-
Tenda
ulitakalo (lakini tambua) hakika utalipwa kwalo na utaulizwa kuhusiana
nalo.” Twabaraaniy
Bado
haijaweza na kamwe haitaweza elimu ya sayansi ya utabibu ambayo imefikisha
mwanadamu kupandikiza moyo mahala pa moyo mwingine. Wala elimu ya
teknolojia iliyomuwezesha mwanadamu kufika mwezini haijaweza na katu
haitaweza kupambana na uzee, haijaweza kumrudishia mzee ujana wake.
Amesema kweli Mtume wa Allah–Rehema na Amani zimshukie: “Allah
hajapatapo kushusha ugonjwa wo wote ila alishusha pamoja nao dawa yake ila
uzee (ukongwe)”. Na katika riwaya nyingine: “….ila mauti.”
Bukhaariy
Sasa
ikiwa huu ndio ukweli kuhusiana na uhai/maisha ya mwanadamu vipi basi
anaweza kuutumainia kiasi cha kujiwekea mipango mingi? Na il-hali ukweli
ni kwamba umri halisi wa mwanadmau ni ile miaka michache anayoipitisha
tangu kuzaliwa kwake mpaka kufa kwake.
Si ajabu ukamkuta mwanadamu kapewa umri wa zaidi ya miaka mia moja
lakini katika daftari lake la amali njema ukakuta sifuri.
Hakujinufaisha yeye mwenyewe kutokana na umri huo wala wengine
hawakunufaika nao. Na mtu mwingine huweza kufa angali kijana mbichi, lakini
akawa amelijaza daftari lake la amali za kheri na kuwaachia wenzake mema
ya kumkumbuka. Kwa mantiki
hii basi, kumbe inawezakana mwanadamu kuurefusha umri wake kwa namna
atakavyowafikiwa. Akaurefusha kwa kumuabudu Allah Bwana Mlezi wake,
kuwatendea wema viumbe wake. Matendo yake haya yakigubikwa na ikhlaswi (utendaji
kwa ajili ya Allah tu) na ukamilifu/ufanisi itakuwa ni bora kwa mtendaji
wake. Na kwa kiasi ambacho matendo yake yatakuwa na faida na kuacha athari
njema kwa wengine ndio huwa kiasi cha thamani na daraja ya mtendaji.
Matendo haya ni kama vile kuwajulisha watu jambo la uongofu,
kuwaokoa katika mambo maovu, kuwatatulia matatizo yao, kuwaondoshea dhulma,
au kuwanusuru dhidi ya adui yao na baki ya matendo mengine ambayo manufaa
yake huirejea jamii. Hapa ndipo utaona amali kama kulingania kwa Allah
(da’awah) na kuipigania jihadi dini ya Allah zikawa katika kilele
cha amali zote kidaraja mbele ya Allah Bwana Mtume–Rehema na Amani
zimshukie–anasema: “Atakayelingania jambo la uongofu, atakuwa na ujira
mithili ya ujira wa watakaomfuata (katika kutenda jambo hilo). Hili (la
kupata ujira mithili ya watendaji) halipunguzi cho chote katika ujira wao
(watendaji).” Muslim
Na akasema tena: “Hakika peponi kuna daraja mia moja ambazo Allah
amewaandalia mujahidina kaitka njia ya Allah. Umbali ulio baina ya daraja
mbili ni kama umbali ulio baina ya mbingu na ardhi.” Bukhaariy
Mmoja miongoni mwa maswahaba wa Bwana Mtume alipita katika njia za
majabalini ambako kuna kijisima cha maji baridi kikamvutia, akajisemea
moyoni: Lau ningelijitenga na watu nikakaa katika njia hii na kufanya
ibada, lakini sitafanya hivi mpaka nimuombe idhini Mtume wa Allah.
Bwana Mtume–Rehema na Amani zimshukie- akamwambia: “Usifanye
hivyo, kwani daraja ya mmoja wenu katika njia ya Allah ni bora kuliko
swala yake aiswaliyo nyumbani kwake kwa miaka sabini. Je, hampendi Allah
akughufirieni na kukuingizeni peponi? Piganeni katika njia ya Allah, ye
yote atakayepigana katika njia ya Allah,
(hata) kiasi cha kumkama ngamia (wake) kumemuwajibikia kupata pepo.”
Tirmidhiy & Al-Haakim.
Hivi ndivyo amali zinavyotofautiana na kuzidiana katika daraja na
ujira na mwenye mafanikio ni yule mwenye pupa ya kulifanya lililo bora: “….NA
KATIKA (kupata) HAYA WASHINDANE WENYE KUSHINDANA.” (83:26)
|