Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Dini ni nasaha, wakauliza kwa nani ? Akasema Mtume : Kwa Allah, Mtume wake, kwa viongozi wa waislamu na watu wa kawaida" Hadith Tukufu

KUUELEKEA MUSTAKBALI KWA NDOTO ZENYE MATUMAINI MEMA NA MATAMANIO TU.

 Faida

 

          Mtazamo huu hasi wa mustakbali; msimamo wa kukosa matumaini na kukata tamaa, unakabiliwa na mtazamo  chanya.  Huu si mwingine zaidi ya msimamo wa kuuelekea mustakbali kwa ndoto tupu zenye matumaini mema na matamanio bila ya kuwa na elimu inayoenda sambamba na wakati, kazi wala mikakati ya kimaendeleo. Si hatia kusema kuwa ndoto zenye matumaini mema na matamanio pekee hazijengi utukufu/heshima na wala haziyathibitishi matumaini hayo. Sayyidna Aliy Ibn Abuu Twalib–Allah amuwiye radhi–alimuasa mwanawe: “Tahadhari na kuyategemea matumaini tupu, kwani kwa yakini (matumaini) hayo ni bidhaa ya mtu mpumbavu (asiye na akili).”

Na alisema mshairi mmoja:

Na wala usiwe mtumwa wa matumaini tupu,

Kwani matumaini hayo ni rasilimali ya watu muflisi (wa mawazo/fikra).

 

Qur-ani Tukufu imeyapinga vikali madai ya Ahlul-Kitaab (Watu wa kitabu) Mayahudi na manaswara. Madai ya kuingia peponi kwa matumaini/matamanio matupu bila ya kufanya yale ambayo  ndio sababu ya kuingilia huko peponi: Allah Mola Mtukufu anatuambia: “NA WALISEMA: HATAINGIA PEPONI ILA ALIYE MYAHUDI AU MNASWARA (mkristo) HAYO NI MATAMANIO YAO TU (si hukumu ya Allah) SEMA: LETENI DALILI ZENU (juu ya madai yenu haya) KAMA NYINYI NI WASEMA KWELI. NAAM, WANAOELEKEZA NYUSO ZAO KWA ALLAH NA WAKAWA NI WATENDAJI MEMA (kwa viumbe wenziwao) BASI WAO WATAPATA MALIPO YAO KWA MOLA WAO, WALA HAITAKUWA KHOFU JUU YAO WALA HAWATAHUZUNIKA.”  (2:111–112)

Qur-ani haikukomelea tu katika kuyapinga madai na matamanio haya ya Ahlul-Kitaab, bali imewachanganya pamoja nao waislamu wanaodhania kwamba kujinasibisha kwao na Uislamu bila ya kuishi kwa mujibu wa Uislamu wao, kutawaokoa mbele za Allah. Hawa wanaambiwa na Allah: “(Kuingia Peponi) SI KWA MATAMANIO YENU, WALA SI KWA MATAMANIO YA WATU WALIOPEWA KITABU (kabla yenu lakini mambo ni haya) ATAKAYEFANYA UBAYA ATALIPWA KWA (ubaya) HUO WALA HATAPATA MLINZI WALA MSAIDIZI KWA AJILI YAKE MBELE YA ALLAH. NA WATAKAOFANYA VITENDO VIZURI, WAKIWA WANAUME AU WANAWEKA, HALI WAO NI WENYE KUAMINI, BASI HAO WATAINGIA PEPONI WALA HAWATADHULUMIWA HATA TUNDU YA KOKWA YA TENDE.”  (4:123–124)

Ni vema ikaeleweka kwamba inachopinga na kukanusha Qur-ani ni mtu kuyategemea matamanio tu bila ya kufanya kile kitakachoyathibitisha matamanio hayo.  Lakini Qur-ani haipingi matumaini mema ya siku za usoni na imetofautisha baina ya mambo mawili haya. Matumaini ni yale yanayokwenda sambamba na amali (matendo) itakayoyafanikisha, na kama matumaini hayakukutanishwa na amali yake, basi hicho si kingine bali ni matamanio matupu. Ni kwa sababu hii ndio hadithi ya Bwana Mtume–Rehema na Amani zimshukie–ikazingatia kuwa ni ajizi na upumbavu kuyafuata matamanio ya nafsi kwa kutegemea maghfira (msamaha) ya Allah na ukunjufu wa rehema zake. Huu ni uwendawazimu, kwani mtu mwenye fikra lemavu hizi haijagonga ngoma za masikio yake kauli ya Allah: “…BILA SHAKA REHEMA YA ALLAH IKO KARIBU SANA NA (wale waja wake) WANAOFANYA MEMA.”  (7:56)

Na kauli yake: “...NA REHEMA YANGU INAWEZA KUKIENEA KILA KITU. LAKINI NITAWAANDIKIA (kweli kweli kabisa) WALE WANAOJIKINGA NA YALE NILIYOWAKATAZA, NA WANAOTOA ZAKA NA WANAOZIAMINI AYA ZETU.”  (7: 156)

Katika kuiweka wazi maana hii, imekuja hadithi ya Mtume wa Allah– Rehema na Amani zimshukie: “Mwenye akili/busara ni yule aliyeihifadhi nafsi yake na akatenda amali (njema) kwa ajili ya (maisha) baada ya mauti. Na dhaifu wa akili ni yule aifuatishiaye nafsi yake matamanio yake (maovu) na akatamani kwa Allah matamanio (matupu bila ya amali).” Tirmidhiy, Ahmad & Maajah.

Qur-ani Tukufu inayaenzi matumaini/matarajio na kuwasifia watu watarajiao: “HAKIKA WALE WALIOAMINI NA WALE WALIOHAJIRI (wakahama kuja Madinah) NA WAKAPIGANIA NJIA YA ALLAH, HAO NDIO WANAOTUMAI REHEMA YA ALLAH NA ALLAH NI MWINGI WA KUSAMEHE (na ) MWINGI WA KUREHEMU.”  (2:218)

Baadhi ya waja wema wa Allah–Allah awarehemu-wanasema: {Kutaka pepo bila ya amali ni dhambi miongoni mwa dhambi.  Na kutarajia uombezi wa Mtume (shafaa)  bila ya kufuata suna (mwendo wake) ni aina ya ghururi (madanganyo). Na kutarajia rehema ya Allah pamoja na (kufanya maasi) ni ujinga na upumbavu}.

 

c) WAPENZI WA HADHIRI (ZAMA ZILIZOPO):

          Wako watu ambao kamwe hawageuki nyuma kutazama zama zilizopita na wala hawazielekezei nyuso, nyoyo na akili zama zijazo (mustakbali) Hawa huishi kwa ajili ya leo yao na ndani ya leo yao (zama zao) tu Haya ni natija na matokeo ya mtazamo wao kwamba jana (zama zilizopita) imekwishapita na kwenda zake. Na kipitacho huwa kimekufa, kwa hivyo basi haiingii akilini kukishughulikia au kukifikiria kilichokufa. Kwa mtazamo wa kundi hili la watu linaloishi katika jamii yetu, mustakbali (kesho/zama zijazo) ni kitu ghaibu (hidden/unseen) Na kitu ghaibu ni kitu majuhuli (unknown), kwa mantiki hii basi haimfalii mtu mhalisia wa mambo kufungamana na kushikamana na kitu majuhuli. Kwa sababu kufanya hivyo ni kama kujenga nyumba ya barafu au kuandika angani. Je, nyumba hiyo itasimama na maandishi hayo yataonekana na mwenye macho akamakinika kuyasoma?

Hawa kuzama na kujitoa kwao wazima wazima kwa leo yao kumewapumbaza na kuwafanya waisahau kesho yao kama kulivyowapumbaza kustafidi na jana yao.  Hawa ni wana wa leo yao na zama zao tu basi, hawajishughulishi na Akhera kwa sababu hiyo (akhera) ni mustakbali (kitu kijacho). Na wao itikadi yao ni kutokuuza taslimu (cash) kwa deni la muda mrefu wala kilichopo kwa kijacho/kisichopo.  Na wala hawajishughulishi na historia wala urithi wa mambo ya kale, kwa kigezo kuwa hayo yamepita na kumalizika. Tunaposema kwamba watu wenye fikra hizi ni “wana wa leo yao” tunakusudia kuwa wao ni watu wasiofikiria wala kujishughulisha ila na zama waishizo tu. Bila ya kujikumbusha na kuchukua maonyo na mazingatio ya jana (zama zilizopita) wala kuifikiria na kuipangia mikakati inayoambatana na utekelezaji kesho yao (zama za usoni). Haya na tukubaliane nao kwamba mtu ajishughulishe tu na wakati alionao (aishio ndani lyake). Ni kwa nini basi anaupoteza, na ni kwa nini asiutumie katika maendeleo yake binafsi na jamii kwa ujumla?! Ni kwa nini aumalizi muda wake wote huo katika kumtii Mola wake, katika kuinusuru haki (Uislamu) na kutenda mema? Ukweli ulivyo mtu akichunguza na kutafiti kwa makini atagundua kwamba leo (zama zilizopo) ni fungu lililo baina ya jana (zama zilizopita) na kesho (mustakbali). Kwa mantiki hii, hivi ni vitu vyernye uhusiano wa moja kwa moja na mafungamano ya karibu kabisa. Kwa msingi huu tunaruhusika kusema na si kusema tu, bali kusema kwa kinywa  kipana kabisa. Kwamba wema na uzuri wa maisha ya leo (sasa) unategemea kabisa msingi mzuri  uliowekwa katika maisha  ya jana (yaliyopita). Na maisha mazuri  ya baadae (mustakbali mwema) unayategemea kwa kiwango kikubwa kabisa maisha ya sasa (leo). Hivi ni sawa kabisa na kusema kuwa leo inapangwa na  kuandaliwa jana na kesho inaandaliwa leo.  Fikra hizi ndizo zilizomsukuma mshairi mmoja kusema:

[Hazikuwa zama (ulimwengu )ila ni nyakati mbili (tu); Uzingatie wakati uliopita  na ufikirie ujao].

 

Naam, ni kweli na ni dhahiri  kwamba mahala pa kuleta mazingatio ya jana (wakati uliopita) na fikra za kesho (wakati ujao) ni leo (wakati uliopo).

 

 


TUJIFUNZE NA TUKUBALI: “Ewe mwanadamu wee! Kwa yakini wewe si cho chote ila ni siku zilizojumuishwa pamoja. Kila inapokwenda zake siku moja, huwa imeondoka baadhi yako.” Al-hasan Al-Biswriy-Allah amrehemu.


Forum | Guestbook | Tuandikie |