Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Dini ni nasaha, wakauliza kwa nani ? Akasema Mtume : Kwa Allah, Mtume wake, kwa viongozi wa waislamu na watu wa kawaida" Hadith Tukufu

MTAZAMO SAHIHI KUELEKEA WAKATI ... VII

 Faida

Mtazamo sahihi kuelekea wakati ni ule unaozichanganya pamoja jana,leo na kesho. Huu ndio mtazamo sahihi, mtazamo unaozitazama zama zilizopita ukaziunganisha na za sasa, ukazitazama zama zilizopo ukaziunganisha na zile zijazo.

 

HATUNA BUDI KUZITUPIA JICHO ZAMA ZILIZOPITA:

  • Tunalazimika kuzitupia jicho zama zilizopita ili:-

  • Tuchukue mazingatio kupitia matukio yaliyopita.

  • Tuwaidhike na miisho ya nyumati zilizopita, vipi ulikuwa mwisho wao.

  • Tuangalie namna Allah alivyowatendea (alivyowaadabisha).

Kwa hivyo basi utaona kwamba zama zilizopita ni chombo cha matukio na ni khazina ya mazingatio na mafunzo. Hebu tuzitafakari pamoja kauli hizi za Allah Mola Muumba wetu:

“ZIMEPITA ADABU NAMNA KWA NAMNA WALIZOTIWA WALIOKUWA

KABLA YENU. BASI SAFIRINI KATIKA NCHI NA MUONE ULIKUWAJE

MWISHO WA WALE WALIOKADHIBISHA (amri zetu). HAYA NI MAELEZO YALIYO WAZI KWA WATU (wote wa zama zote) NA UWONGOZI NA MAUIDHA KWA WAMCHAO.” (3:137-138)

Aya inawaelezea watu wa nyumati zilizoishi ulimwenguni hapa kabla yetu na kututaka tujionee wenyewe namna Allah alivyowaadhibu kutokana na kuzikhalifu amri zake. Tukishaona maangamivu ya watu shupavu, wakukutavu wa nyoyo, ndipo tukae chini tutafakari na kujiuliza kwa nini yaliwasibu yaliyowasibu? Tukishayajua tujiepushe nayo ili kuepuka yasijetufika mithili yaliyowafika wao. Hivi ndivyo tunavyoweza kujifunza kutoka katika zama zilizopita mafunzo yanayotufaa leo katika zama hai. Tuzidi kutafakari:- “KAMA YAMEKUPATENI MAJARAHA, BASI NA WATU HAO YAMEWAPATA MAJARAHA KAMA HAYA. NA SIKU ZA NAMNA HII TUNAWALETEA WATU KWA ZAMU…” (3:140)

Tukipata machungu katika kuipigania dini ya Allah, basi tutambue kwamba sisi sio wa kwanza kufikwa na hayo. Wenzetu waliotu tangulia katika imani pia yaliwapata machungu tena pengine makali kuliko yetu, wakasubiri na Allah akawapa ushindi. Kwa hivyo ni juu yetu nasi kuipigania dini ya Allah huku tukiwa tumeshika silaha kali subira, tuone Allah atakavyotunusuru: “ENYI MLIOAMINI! MKIINUSURU DINI YA ALLAH, NAYE ATAKUNUSURUNI NA ATAITHUBUTISHA MIGUU YENU.” (47:7)

Tuzidi kuwaidhika na yaliyopita na tuchukue mazingatio yatakayotufaa leo: “NA MANABII WANGAPI WALIPIGANA NA MAADUI NA PAMOJA NAO KULIKUWA NA WATAKATIFU WENGI. HAWAKULEGEA KWA YALE YALIYOWASIBU KATIKA NJIA YA ALLAH, WALA HAWAKUDHOOFIKA WALA HAWAKUDHALILIKA NA ALLAH ANAWAPENDA WAFANYAO SUBIRA.” (3: 146)

Kuzitazama zama zilizopita na kujifunza kutokana na matukio yake ni amri ya Allah iliyokuja ndani ya Qur-ani Tukufu: “JE, HAWATEMBEI KATIKA ARDHI ILI WAPATE NYOYO (akili) ZA KUFAHAMIA, AU MASIKIO YA KUSIKILIA? KWA HAKIKA MACHO HAYAPOFOKI (yakadhuru katika dini) LAKINI NYOYO AMBAZO ZIMO VIFUANI NDIZO ZINAZOPOFOKA (zikadhuru katika dini).” (22: 46)

Kingine wanachoweza kufaidika nacho watu wa zama za leo kutokana na urithi wa waliowatangulia ni pamoja na elimu zao za fani mbalimbali, ustaarabu na utamaduni wao. Lakini kufaidika huku ni baada ya kuchekecha na kuchuja, tukayachukua yale mazuri yanayoenda sambamba na zama pamoja na hali zetu. Ni haki yetu kuwarithi waliotutangulia, kwani Mtume wa Allah–Rehema na Amani zimshukie –anatuambia: “Neno lenye hekima (busara/elimu) ni kipotewa cha muumini, po pote atapokikuta basi yeye ana haki nacho zaidi (kuliko mtu mwingine).” Tirmidhiy & Ibn Maajah

Si sawa kukiacha cha kale/zamani eti kwa sababu tu ni cha kale. Hii ni kwa sababu viko vitu vingi vinavyozingatiwa kuwa ni vya kale na ambavyo kimaumbile/kiasili havikubali upya vina faida na ubora hadi hii leo. Hebu tuifanye Qur-ani Tukufu kama kigezo, kisha tujiulize: Je, haukuwa ubora wa Qur-ani ni kwa sababu hiyo Qur-ani ni maneno makongwe ya Allah ambayo upya wake hauchakai na wala haipitwi na wakati? Je, ubora wa Al-Ka’abah hautokani na kuwa kwake “nyumba kongwe ya ibada” yenye kukusudiwa na watu zama baada ya zama? Bila ya shaka Qur-ani haifanyiwi upya, ikaonekana hii iliyopo ni ya siku nyingi kwa hivyo imechoka/haifai iondolewe na iletwe mpya. Haya si maumbile ya Qur-ani kwani yenyewe kimaumbile haichakai, ilifaa jana, inafaa leo na itaendelea kufaa kesho na upya wake kuzidi siku hata siku. Hali kadhalika Al-Ka’abah haihitajii kufanyiwa upya, ikaondolewa kwa kuwa ni kongwe na kuletwa nyingine. Kama ambavyo hakika ya hali na mambo isivyo na haja ya kufanyiwa upya.

Wamechupa mipaka watetezi wa upya pale walipokipa kisogo kila cha kale na kukipigia makofi kila kipya kiingiacho. Wamefanya hivi pamoja na ukweli kwamba miongoni mwa vya kale kuna ambavyo vina manufaa makubwa sana mpaka leo. Na katika vipya kuna ambavyo vina madhara tupu na havifai kabisa pamoja na upya wake. Wamesahau na kughafilika kwamba ukale na upya ni masuala mawili yenye kunasibikiana kwa karibu sana. Uhalisia wa mambo ulivyo cha kale/zamani kwa watu fulani hicho ni kipya kwa watu wengine, hivi ni sawa na kusema: (cha kale chako ni kipya cha mwenzio) na kinyume chake (kipya chako ni cha kale cha mwenzio). Kadhalika ieleweke kwamba kipya hakitasalikia kipya milele, hili linatokana na ukweli kwamba cha kale cha leo ndicho kilichokuwa kipya cha jana. Na hivyo hivyo kipya cha leo ndicho kitachokuwa cha kale kesho, huu ndio ukweli tumekubali au tumekataa. Kila mwanadamu hana budi kuwa na kituo cha kuitazama kila siku inayompitia. Katika kituo hicho aikague nafsi yake na kujiuliza:

-Amefanya nini katika siku yake hiyo iliyopita?

- Kwa nini amefanya hivyo? Au

-Kwa nini ameacha kufanya? Na kadhalika.

Ni bora zaidi kama atakuwa na mazoea ya kulifanya zoezi hili kila siku kabla ya kulala. Kwa yakini kipindi hiki cha mwanadamu kuikagua nafsi yake kinachukuliwa kuwa ni kipindi chake cha kupiga hatua mbele. Kipindi cha kujikosoa na kujisahihisha, kipindi cha kukiri udhaifu wake na kujirekebisha. Hiki ni kipindi ambamo mwanadamu huwa ni hakimu wa matamanio yake, hakimu wa dhamira yake. Ni kipindi ambacho muumini huiwekea imani yake askari wa kuilinda na mkaguzi wa kuikagua, sambamba na jaji wa kuihukumu nafsi yake. Kwa mtindo na tabia hii, muislamu hupiga hatua kutoka katika hali ya “Nafsi yenye kuamrisha sana maovu” na kuingia katika hali ya “nafsi inayojilaumu sana katika kutenda maovu”. Katika kuhimiza juu ya zoezi zima la mtu kuikagua nafsi yake, Amirul-Muuminina Umar Ibn Al-Khatwaab-Allah amuwiye radhi–anatuambia: “Zihesabuni/zikagueni nafsi zenu kabla ya kukaguliwa (mbele ya Allah) na zipimeni amali zenu kabla hamjapimiwa.”

Sayyidna Umar mwenyewe alikuwa unapoingia usiku akiipiga bakora miguu yake na kujiambia: Leo nimefanya nini?

Ni muhimu kila mmoja wetu awe na tabia na mazoea ya kuangalia ametenda nini katika ulimwengu na akhera yake kila siku. Akishindwa basi na ajitahidi kulifanya zoezi hili japo mara moja kwa juma ili kujua:

-Ni lipi lilimpasa kulitenda na je, alilitenda?

-Ni lipi halikumpasa kulitenda, je, aliliacha?

Kisha awe na kituo kirefu cha kutafakari na kujikagua mwishoni mwa kila mwezi. Na si vibaya kuwa na kitabu cha rekodi za matukio ya kila siku, kwani kina msaada mkubwa katika kukumbuka yaliyopita. Halafu tena awe na kituo kirefu zaidi wakati wa kuuaga mwaka unaomalizika na kuupokea mwaka mpya. Hiki ndio kipindi kizuri cha kuyarejea na kuyafanyia uchunguzi wa kina yote yaliyopita katika kipindi cha mwaka mzima. Yaliyopita ni pamoja na mafanikio na matatizo, aangalie ameyafikia vipi mafanikio na kwa nini amepatwa na matatizo. Kadhalika hiki ni kipindi cha kupanga mikakati na mipango ya mwaka uliokabili (mpya) sambamba na kuyatafutia ufumbuzi muafaka na munasibu matatizo yote ya mwaka unaomalizika. Hii ndio hesabu ya kufunga mwaka ya muislamu.

Miongoni mwa bidaa ngeni zilizozushwa na watu wa magharibi, na kwa bahati mbaya zikaigwa na baadhi ya waislamu. Ni mtu kufanya halfa ya furaha na kuandaa vitamu na vinono miongoni mwa vyakula na vinywaji. Hafla hii hufanywa kila unapopita mwaka mmoja katika umri wa muhusika, hiki ndicho kile kinachoitwa “Birthday”. Waislamu wamejiingiza katika mambo ambayo Allah hakuyateremshia dalili, mithili ya kuwasha mishumaa kwa idadi ya umri wa muhusika (mwenye birthday yake) na kisha kuizima kwa mtindo wa kimaigizoigizo. Na watu wakapelekeana zawadi kuonyesha hisia zao za upendo kwa muhusika kutokana na sherehe yake hii. Hivi ndugu zanguni, tuliyoamrishwa na Mola wetu kuyatenda, tumeyatenda yote yamemalizika mpaka tena tukaamua kujibebesha mzigo wa tusiyoamrishwa?! Linalotakikana kufanywa na mtu mwenye akili na busara. Badala ya huku kuiga kiupofu upofu mambo ambayo hayana maana wala faida, angeitumia fursa hii ya kumponyoka mwaka mmoja katika uhai wake kama kituo cha kutafakari na kuzingatia. Akafanya kama afanyavyo mfanyabiashara kila mwisho wa mwaka; huyarejea upya madaftari yake ya kumbukumbu za fedha, hesabu ya mali iliyopo sambamba na madeni awiwayo na awiyayo. Mfanyabiashara hufanya hivi ili kujua khasara na faida. Na muislamu ni mfanyabiashara anayefanya biashara na Mola ambapo rasilimali yake ni uhai wake: “ENYI MLIOAMINI! JE, NIKUJULISHENI BIASHARA ITAKAYOKUOKOENI NA ADHABU IUMIZAYO? (Basi biashara yenyewe ni hii): MUAMININI ALLAH NA MTUME WAKE, NA IPIGANIENI DINI YA ALLAH KWA MALI ZENU NA NAFSI ZENU, HAYA NI BORA KWENU IKIWA MNAJUA. (Mkifanya haya) ATAKUSAMEHENI DHAMBI ZENU NA ATAKUINGIZENI KATIKA MABUSTANI YAPITAYO MITO MBELE YAKE NA (atakupeni) MASKANI MAZURI MAZURI KATIKA BUSTANI ZA MILELE, HUKU NDIKO KUFUZU KUKUBWA.” (61: 10 – 12)

Badala ya kufanya “Birthday” inayoambatana na mambo yasiyo mridhi Allah kila mtu anapotimiza umri wa mwaka mmoja zaidi. Muislamu alipaswa kuitumia fursa hii kuitafakari biashara yake hiyo iliyoelezwa katika aya hizo za Qur-ani. Akapima ufanisi na tija, akaangalia matatizo na mafanikio sambamba na faida (twaa) na hasara (uasi). Na akamuomba Mola wake amtakabalie mema yote aliyoyatenda katika mwaka uliopita na amsamehe madhambi aliyoyatenda. Bila ya kusahau kumuomba ambubujishie kheri, furaha na fanaka katika mwaka wake mpya na amkinge dhidi ya majanga na maafa mbalimbali. Huku akiamini kuwa Allah atamuuliza juu ya mwaka wake huo uliomalizika.

 

 


TUJIFUNZE NA TUKUBALI: “Ewe mwanadamu wee! Kwa yakini wewe si cho chote ila ni siku zilizojumuishwa pamoja. Kila inapokwenda zake siku moja, huwa imeondoka baadhi yako.” Al-hasan Al-Biswriy-Allah amrehemu.


Forum | Guestbook | Tuandikie |