Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Dini ni nasaha, wakauliza kwa nani ? Akasema Mtume : Kwa Allah, Mtume wake, kwa viongozi wa waislamu na watu wa kawaida" Hadith Tukufu

WAKATI WA MWANADAMU BAINA YA JANA, LEO NA KESHO ..... VI

 

b) WENYE KUFUNGAMANA (MAKHADIMU) NA MUSTAKBALI (WAKATI UJAO/KESHO):

Tukiwaweka kando watu wa kundi hili la jana ambao daima huangalia nyuma kwa sura moja au nyingine. Tunakutana na kundi jingine lenye kufungamana na kuamini katika mustakbali (zama za usoni/zijazo mbele yao). Kundi hili ni la watu ambao huzipa mgongo wa kwa heri ya kuonana zama zilizopita. Watu wa kundi hili daima huangalia mbele hawageuki nyuma, msimamo wao huu huwafanya waitupilie mbali historia (tarekh) na hivyo kujidhulumu wenyewe fursa ya kujifunza kutokana na historia. Hawana haja kabisa na historia ya watu/nyumati zilizokuwa kabla yao na wala hawataki kabisa urithi wa kitamaduni, kidini wala ule wa kiustaarabu. Bila ya kuangalia mazuri yatokanayo na urithi huu wakayaenzi kwa kuyaendeleza na kuyaboresha na kuyatupilia mbali yaliyo mabaya na ya upotofu. Hawa ni wale ambao aghlabu husikika wakinena: (Hebu tuondokeeni na hadithi za mababu waliokufa na kushiba mauti na tuacheni tutafiti vijana watakaokuwa viongozi wa kesho). Na pengine hunena: (Kwa yakini macho yetu hayakuumbwa visogoni mwetu hata tuweze kutazama nyuma. Bali yameumbwa nyusoni mwetu ili tuweze kuangalia mbele). Hunena maneno haya na mithili yake, maneno haya huwa ni haki iliyokusudiwa batili iwapo mtu atalenga kuzisahau kabisa zama zilizopita na yake yote. Na kukataa urithi na yote yaliyomo ndani yake na kuimwagia mchanga (kuizika) historia na yote iliyoyasheheneza miongini mwa darsa, mazingatio, maongozi na mashauri yanayoongoza akili na nyoyo. Ee uzuri ulioje wa kauli ya Allah iliyomo ndani ya kitabu chake kitukufu ikizindua kustafidi na kuwaidhika na yaliyopita: “JE, HAWATEMBEI KATIKA ARDHI (wakaona athari za mambo ya kale) ILI WAPATE NYOYO (akili) ZA KUFAHAMU AU MASIKIO YA KUSIKILIA? KWA HAKIKA MACHO HAYAPOFOKI (yakadhuru katika dini) LAKINI NYOYO AMBAZO ZIMO VIFUANI NDIZO ZINAZOPOFOKA (zikadhuru katika dini)”. (17:46)

 

MTAZAMO HASI/LEMAVU KUELEKEA MUSTAKBALI (MTAZAMO WA KUKATA TAMAA):

Wako miongoni mwa watu ambao huitazama kesho na kuifikiria kwa mtazamo wa mtu aliyekata tamaa. Mtu aliyevaa mawani meusi tii (mno) anautazama uhai, viumbe hai, zama na mahala kwa nyuma ya mawani hayo. Mara tahamaki mtu huyu hukata tamaa na kesho na kupoteza kabisa matumaini na kufaulu kutokana na kuyatazama kwake mambo/vitu kwa kutumia zana isiyo sahihi wala muafaka. Imekita ndani ya nafsi yake dhana ya kwamba kamwe mambo hayabadiliki kutoka katika hali mbaya ila kwenda katika hali mbaya zaidi kuliko ya sasa/iliyopita. Na kwamba maisha ni mithili ya usiku wa kiza totoro usiochomozewa na alfajiri wala kiza chake hakiondoshwi na mwangaza mkali wa jua. Huu bila ya shaka yo yote ni mtazamo bomoa; unaombomoa yeye binafsi, maisha yake na jamii yake. Maisha ya mtu yasiyo na mionzi ya matumaini ya mustakbali ni ya dhiki zaidi kuliko dhiki ya ngamia kuingia katika tundu ya sindano. Maisha ya jamii iliyokosa matumaini na mipango ya baadae ni maisha mafu yasiyo na roho wala harakati Lau si matumaini na mipango ya mustakbali, asingelijenga aliyejenga akakaa na tukakaa, asingelima aliyelima akavuna akala na tukala na wala elimu/sayansi na teknoloja isingelipiga hatua mbele na kufika hapa ilipo leo. Natija ya haya yote ni kwamba dini, historia na uhalisia wa mambo, vyote hivi vinatufundisha kwamba:-

  • Maisha hayana maana ikiwa yanasuhubiana na kukata tamaa.

  • Hakika pamoja na dhiki huja faraja au faraja husuhubiana na dhiki au faraja imo ndani ya dhiki.

  • Baada ya usiku kuondoka hatimaye huchomoza alfajiri.

  • Kudumu kwa hali moja milele ni muhali, yaani ni jambo lisilowezekana kwani mambo huenda na kubadilika.

Allah Mola Mjuzi wa yote anatuambia ndani ya kitabu chake kitukufu: “…HAWAKATI TAMAA NA REHEMA YA ALLAH ISIPOKUWA WATU MAKAFIRI”. (12:87)

Na katika aya nyingine anasema: “….NA NANI ANAYEKATA TAMAA YA REHEMA YA MOLA WAKE ISIPOKUWA WALE WALIOPOTEA?” (15:56)

Miongoni mwa sura za kukata tamaa na kukosa matumaini ni ile itikadi iliyoenea miongoni mwa watu wengi kwamba hivi sasa tunaishi na tumo katika zama za mwisho. Umri wa dunia umekwisha na kwamba alama za kiyama zilizotajwa na Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-zimeshadhihiri dhahiri shahiri. Na kwamba kheri katika zama hizi za mwisho ni mtu kujiweka nyuma na shari iko katika kujiweka mbele kimaendeleo. Na kwamba taa ya dini inazimika siku baada ya siku mpaka itazimika kabisa na kumaanisha kufutika kwa kitu dini katika uso wa ardhi hii. Na hivyo kutoa fursa ya kuenea kwa ukafiri dunia nzima mpaka kiyama hakitasimama ila kwa kafiri mwana wa kafiri. Kwa hivyo basi kwa kuyazingatia yote hayo kunakuwa hakuna mantiki ya mtu kuwa na mipango ya baadae ya kmaendeleo. Hii ni kwasababu hakuna matumaini wala tamaa ya kuirekebisha au kuibadilisha hali hii iliyokabili usoni mwetu. Dalili na ushahidi wanaoutoa juu ya nadharia yao hii ya kukata tamaa ni hadithi zilizopokelewa kutoka kwa Bwana Mtume– Rehema na Amani zimshukie–zikitaja khabari za fitna na alama za kiyama.

Lakini uhalisia na ukweli wa mambo na hali si kama walivyofahamu watu hawa kwa nadharia yao hii inayotazama mambo kwa ujuu juu tu bila ya kuzama ndani. Huu ni ufahamu mfupi kwani aya na hadithi zilizokuja katika kutaja ukaribu wa kusimama kwa kiyama na kudhihiri kwa alama zake. Aya na hadithi hizi hazimaanishi kwamba kiyama hicho ki mlangoni. Hii ni kutokana na ukweli kwamba ukaribu na umbali wa kitu ni dhana ya ulinganifu wa kitu kimoja baina ya kingine. Ni nani ajuaye, huenda baina yetu na hicho kiyama kuna maalfu ya miaka. Hajui kusimama kwa kiyama ila Allah pekee ambaye yeye ndiye Msimamishaji wa hicho kiyama. Na nani ajuaye huenda hicho kiyama ki karibu yetu zaidi kuliko tunavyofikiria na kusawirisha! Na kuhusiana na hicho kiyama Qur-ani Tukufu

haikuzidisha zaidi ya kusema:

“….PENGINE KIAMA KIKO KARIBU”. (33:63)

“...LABDA KIAMA KIMEKARIBIA”. (42:17)

“...HAITAKUFIKIENI (saa hiyo–yaani kiama) ILA KWA GHAFLA (tu

hivi)…” (7:187)

Kuletwa kwa Mtume wetu-Rehema na Amani zimshukie–peke yake ni miongoni mwa alama za kiyama, kwani Mtume ndiye aliyesema:

“Nimetumilizwa (nimepewa utume) mimi na kiyama kama viwili hivi….na akapacha baina ya dole gumba na kidole cha kati.”

Buhkaariy & Muslim

Kwa hivyo basi kuacha kufanya amali za kimaendeleo kwa lengo la kuustawisha na kuuamirisha uliwengu. Kwa madai ya kuhuisha sheria ya Kiislamu, uma wa Kiislamu na dola ya Kiislamu kwa kungojea kusimama kwa kiyama. Na kwa kutegemea kwamba sisi tuko katika zama za mwisho, hili ni suala lipingwalo na kukanushwa na dini kwa nguvu zote. Kwani ni dini hii ndio iliyomuamrisha muislamu kujitahidi kufanya amali maadam yu hai. Na waislamu kwa kulizingatia hili ni uma wenye kuamrishwa kufanya amali mpaka ufungwe mlango wa toba. Na hili la kufungwa mlango wa toba litapatikana katika siku za mwisho za umri wa duniani, ambapo jua litachomoza kutokea upande wa magharibi: “…SIKU ZITAKAPOFIKA BAADHI YA ISHARA ZA MOLA WAKO, BASI MTU (kafiri) HAITAMFAA IMANI YAKE, AMBAYE ALIKUWA HAKUAMINI ZAMANI, AU (muislamu) HAKUCHUMA KHERI KATIKA UISLAMU WAKE….” (6:158)

Na kwa yakini imekuja kutoka kwa Mtume wa Allah amri ya kuendelea kufanya amali za kidunia (za maendeleo), dunia ambayo si cho chote katika mtazamo wa dini. Amri hii ni pale aliposema: “Kitakaposimama kiyama na ilhali mkononi mwa mmoja wenu kuna mche, basi akiweza kisisimame mpaka aupande basi na aupande”. Ahmad & Bukhaariy

Basi ikiwa muislamu ameamrishwa asiuache mche wake hata kama kasikia mpulizo wa parapanda mpaka aikamilishe kazi yake hiyo kiasi ya uwezo wake. Anaamrishwa hivyo hata kama yeye hatanufaika na mche huo wala ye yote baada yake. Iweje basi baina yetu na kiyama ambacho ki masafa yasiyojulikana ila na Muumba wa ulimwengu pekee?! Kwa yakini kufanya kazi ni suala linalotakiwa hata kama kazi hiyo haikumpa matunda muhusika. Ikimpa matunda mbele atakuwa amefuzu kwa kupata vizuri viwili; dunia na akhera. Na kama haikumpa matunda mbele (hapa duniani), basi inatosha kwamba yeye amejitahidi, ametekeleza wajibu wake na amepata udhuru wa kumsemea mbele ya Allah.



Forum | Guestbook | Tuandikie |