|
Kimsingi wakati
ambao mwanadamu anaishi ndani yake unagawanyika katika vigawanyo vikuu
vitatu:-
Watu katika
mahusiano/mafungamano yao na wakati kupitia vigawanyo vyake hivi, wako
katika makundi kadhaa. Kidesturi na kiuzoefu makundi haya husimama baina
ya ncha mbili; ubadhirifu (utumiaji mbaya) na upotezaji wa wakati. Kwa
mizani hii tunakutana na makundi yafuatayo:-
Makhadimu (watumwa)
wa wakati uliopita.
Makhadimu wa
hadhiri,
Makhadimu wa
mustakbali, na
Wakatikati ambao
hukipa kila kigawanyo cha wakati haki yake.
A: WENYE KUFUNGAMANA
(MAKHADIMU) NA ZAMA ZILIZOPITA (JANA):
Ni ukweli
usiopingika kwamba katika jamii zetu liko kundi la watu ambao hawajui
katika zama (wakati) ila jana iliyopita tayari. Hawa kutokana na ufahamu
wao huu wa wakati, huendelea kuishi katika wakati uliopita (jana) na hali
ya kuwa tayari wamo katika hadhiri (wakati uliopo/leo). Hawashughuliki
kabisa na leo yenye kushuhudiwa na viumbe wote, wala hawana khabari kabisa
na kesho yenye kuwaita. Ni mamoja ikiwa ujana/ukale wao ni natija ya nafsi
zao, au wameurithi kwa wahenga wao au unatokana na kaumu zao zilizopita.
Kundi hili la makhadimu wa ukale/jana lina sura kadhaa:-
Hujifakharisha kwa
yaliyopita wakiamini kufanya hivyo ni kuwaenzi wahenga wao. Lakini hufanya
hivyo bila ya wao kuongeza jipya katika yale yaliyopita au wao kuleta
ziada itakayoiunganisha jana ya wahenga wao na leo yao wao. Hawa ni watu
ambao daima husikika wakisema: Tulikuwa bwana..., baba zetu na mababu zetu
ndio walikuwa.... Wala huwasikii wakisema: Sisi tumefanya kadha au
tumeanzisha kadha au tunasimamia kadha. Allah amrehemu yule aliyesema:
“Kwa yakini kijana ni yule asemaye: Mimi ndiye. Wala kijana si yule
asemaye: Baba yangu alikuwa”.
Hakuna anayekanusha
wala kupinga kwamba mtu kujifakharisha na kujitukuza na wahenga wetu wema
na kuyaenzi mambo yao mema ni jambo jema linalofaa kutendwa na kila mmoja
wetu. Lakini swali linalojitokeza ni kuwa tujifakharishe na kuyaenzi vipi
mema hayo? Je, kunatosha tu kusema babu zetu walikuwa au haya ni urithi wa
babu zetu? Bila ya shaka fakhri na maenzi mazuri ni
kuyakamilisha/kuyaendeleza yote mema waliyoyaanza na kutuachia. Na kuwaiga
katika mambo ya kheri waliyokuwa wakiyafanya.
Huamini katika
urithi wa wahenga. Watu hawa hudai utakatifu katika kila kilichoachwa na
wahenga na kuona kuwa ni kosa kuufanyia uchunganuzi wenye kulenga
kuyaendeleza yote yaliyo ya sawa na kuyaacha yasiyo ya sawa. Haya hutokana
na kuamini kwamba daima zama zilizopita ni bora kuliko zama tulizomo leo.
Na kwamba watu wa leo hawana kipya wanachoweza kukifanya ambacho
hakikufanywa na waliopita. Hapa ni wajibu wetu kujua maana na eleweko la
urithi/mirathi na kisha kuifanyia tathmini. Wako watu wanaoenda sambamba
na eleweko la urithi kama lilivyo ndani ya Qur-ani Tukufu na Sunah.
Waislamu hawana khiari katika kulazimikiana na kushikamana na eleweko hilo
kwa mujibu wa imani yao: “HAIWI KWA MWANAMUME ALIYEAMINI WALA KWA
MWANAMKE ALIYEAMINI, ALLAH NA MTUME WAKE WANAPOKATA SHAURI, WAWE NA KHIARI
KATIKA SHAURI LAO...” [33:36]
Urithi kwa janibu ya
ki-Mungu hauna nafasi ya kuwekwa katika mizani ya kupimwa au kusita katika
ama kufuata au kutokufuata. Bali ni wajibu wa kila muislamu kulifuata kila
lililoachwa na wahenga wetu wema (salafu) ambalo imethibiti kuwa latoka
kwa Allah na Mtume wake. Ama janibu ya kibinadamu, hii ni wajibu kuiweka
katika chekeche litakalochekecha na kuchuja baina ya likubaliwalo na Allah
na Mtume wake na lisilokubaliwa. Katika mirathi hii ya kibinadamu yako
mambo yanachukua sifa ya kitaifa na si ya kimataifa. Haya yatabeba chapa
ya mahala husika na wala hayafai mahala pengine. Kadhalika yako ambayo
yanayochukua chapa ya zama za zake na hayafai katika zama nyingine.
Huyafuata ya kale
kwa kuiga tu bila ya kuwa na hoja za msingi ila kusema tu hivi ndivyo
walivyokuwa/walivyofanya wazee wetu waliotangulia. Hawataki kabisa
kuyatahini na kuyahoji ya wazee ili kujua haki na batili, uongofu na
upotofu wake. Hawa msimamo wao ni msimamo wa mtu mwenye kupokea na
kutekeleza/kufuata kama alivyopokea bila ya kuhoji usahihi au ubatili
wake. Hawa ndio watu ambao Qur-ani Tukufu inasema juu yao: “NA
WANAPOAMBIWA: FUATENI ALIYOYATEREMSHA ALLAH, HUSEMA: BALI TUTAFUATA YALE
TULIYOWAKUTA NAYO BABA ZETU. JE, HATA KAMA BABA ZAO WALIKUWA HAWAFAHAMU
CHO CHOTE WALA HAWAKUONGOKA (watawafuata tu)?” [2:170] Huu ndio
msimamo/hoja walizokabiliana nazo Mitume wa Allah wakati wa kufikisha
ujumbe wa Mola wao kwa waja wake. Hii ndio kaumu ya Nabii Huud-Amani ya
Allah imshukie-inamuambia Mtume wao: “...JE, UMETUJIA ILI TUMUABUDU
ALLAH PEKE YAKE NA TUYAACHE WALIYOKUWA WAKIYAABUDU BABA ZETU?...” [7:70]
Na hivi ndivyo Thamudi walivyomwambia mtume wao Nabii Swaleh-Amani ya
Allah imshukie: “ ...EWE SWALEH! BILA YA SHAKA ULIKUWA UNAYETARAJIWA
(kheri) KWETU KABLA YA HAYA (sasa umeharibika). OH! UNATUKATAZA KUABUDU
WALIOWAABUDU BABA ZETU?...” [11:62]
Na Nabii
Ibrahimu-Amani ya Allah imshukie-alipoiambia kaumu yake: “...NI NINI
MASANAMU HAYA MNAYAKALIA WAKATI WOTE (kuyaabudu)? WAKASEMA: TULIWAKUTA
BABA ZETU WAKIYAABUDU (basi na sisi tunayaabudu)”. [21:52-53]
Na hivyi hivyo
ndivyo kaumu ya Nabii Shuaib ilivyomwambia Mtume wao: “...EWE SHUAIB!
SWALA ZAKO (zinakuzuzua sana)! ZINAKUAMRISHA (utuamrishe) TUYAACHE
WALIYOKUWA WAKIYAABUDU BABA ZETU...” [11:87]
Hivi ndivyo Qur-ani
Tukufu ilivyoikariri suna (mwenendo) hii na kuisajili: “NA KADHALIKA
HATUKUPELEKA MUONYAJI KATIKA MJI WO WOTE ILA MATAJIRI WAKE WALISEMA: KWA
YAKINI TULIWAKUTA BABA ZETU JUU YA DASTURI (zao makhsusi) NA HAKIKA SISI
TUTAFUATA NYAYO ZAO”. [43:23]
Qur-ani Tukufu
imeupinga uchovu na ugumu huu wa kiakili wa kundi hili la watu wa kufuata
waliyoyarithi kutoka kwa baba (wazee) zao ufuataji mpofu. Qur-ani
ikawarudi kama ifuatavyo: “...JE, HATA KAMA BABA ZAO WALIKUWA HAWAFAHAMU
CHO CHOTE WALA HAWAKUONGOKA (watawafuata tu)? [2:170]
“...JE, HATA KAMA
BABA ZAO WALIKUWA HAWAJUI KITU WALA HAWAKUONGOKA (watawafuata tu)?”
[5:104]
“AKASEMA (huyo
Mtume wao): HATA KAMA NAKULETEENI (dasturi) YENYE UWONGOFU BORA KULIKO
MLIYOWAKUTA NAYO BABA ZENU (mtaendelea na dasturi ya wazee wenu)?...”
[43:24]
Kadhalika waliomo
katika zama za leo lakini wao wanaishi katika zama zilizopita. Hawa ni
wale wanaouonea majonzi na majuto wakati uliokwishawapita tayari, daima
husikika wakisema: Laiti ningefanya/nisingefanya kadha, lau ningelifanya
kadha ingelikuwa kadha. Aina hii ya fikra/hisia humtia mtu katika utumwa
wa huzuni kuu na kumfanya aishi katika uchungu unaomkosesha raha na
furaha. Aishi katika masumbuko ya moyo yasiyo na sababu, masumbuko ambayo
pengine yakamsababishia maradhi ambayo yakawa ndio sababu ya mauti yake.
Ni kwa kuyazingatia na kuyajua haya ndio wenye hekima wakasema:
“Kuyashughulikia yaliyofutu katika wakati uliopita ni kupoteza wakati wa
sasa”. Si ajabu wala jambo la kushangaza Qur-ani Tukufu na Sunah
kuupinga mwenedno na tabia hii. Allah Mola Mwenyezi anawaambia waislamu
baada ya kusibiwa na yaliyowasibu katika vita vya Uhud: “ENYI MLIOAMINI!
MSIWE KAMA WALE WALIOKUFURU NA WAKASEMA JUU YA NDUGU ZAO WALIPOSAFIRI
KATIKA NCHI AU WALIPOPIGANA (wakafa): WANGALIKUWA KWETU WASINGALIKUFA WALA
WASIMGALIUAWA. (Allah amewatia dhana hii) ILI AFANYE HAYO KUWA MAJUTO
KATIKA NYOYO ZAO...” [3:156]
Nae Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-anasema: “Muumini mwenye nguvu ni mbora
na anapendeza zaidi mbele za Allah kuliko muumini dhaifu. Na kila mmoja
yuna kheri (yake), pupia (kufanya) yatakayokunufaisha na umtake msaada
Allah. Na (kamwe) usiwe na ajizi na wala usiseme: Lau mimi ningelifanya
kadha ingelikuwa kadha. Lakini (wewe) sema: (Hivi ndivyo) alivyokadiria
Allah na alitakalo (Yeye) huwa/hulitenda. Kwani (neno) ‘LAU’ hufungua
amali ya shetani”. Muslim
|