|
ALASIRI (JIONI):
Unapoingia wakati wa Alasiri na muadhini akalingana na
kunadi: Haya njooni kuswali. Hapo muislamu huamka kutoka katika mapumziko
ya mchana kama alikuwa amelala. Au ataacha kazi yake kama alikuwa kazini,
akichapukia msikitini kuswali swala ambayo huzingatiwa kuwa ni ‘Swala ya
kati na kati’ ya siku. Hakujuzu kwa muislamu kuipuuzia swala hii bali na
swala nyingine zote kwa kisingizio cha kubanwa na kazi. Akajipa uhalali na
kibali cha kuendelea na kazi/biashara na kuacha kuuitikia wito wa swala
uliogonga ngoma za masikio yake na kupenya mvunguni mwa moyo wake. Wasifu
wa waumini wa kwelikweli ni kama alivyoueleza Allah Mola Mtukufu ndani ya
kitabu chake kitukufu kwamba ni: “WATU AMBAO BIASHARA WALA KUUZA
HAKUWASHUGHULISHI (hakuwasahaulishi) KUMKUMBUKA ALLAH, NA KUSIMAMISHA
SWALA NA KUTOA ZAKA. WANAIOGOPA SIKU AMBAYO NYOYO ZITADAHADARI NA MACHO
(pia yatadahadari)” [24:37]
Haifai kabisa kwa muislamu kuiakhirisha swala ya Alasiri
kwa uzembe tu mpaka jua likapiga umanjano na kuelekea kuzama. Hiyo ni
swala ya wanafiki kama alivyosema Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie: “Hiyo ni swala ya mnafiki, hiyo ni swala ya mnafiki achungae
(afuatiliaye) mionzi ya jua hata linapokuwa (jua) baina ya pembe mbili za
shetani. (Hapo ndipo) huinuka na kuidonoa swala (rakaa) nne, hamdhukuru
Allah ndani yake ila kidogo tu”. Muslim
MAGHRIBI:
Jua linapotua na kuzama, muislamu huharakia kwenda kuswali
swala ya maghribi katika wakati wake wa mwanzo. Muislamu hufanya hivi kwa
kuzingatia udhiki wa wakati wa swala hii ya maghribi. Akimaliza kuiswali
swala hii ya fardhi sambamba na suna zake andamizi, husoma kiasi
kimkinikacho cha nyiradi na dhikri za jioni zilizopokewa kutoka kwa Mtume
wa Allah. Kisha muislamu hula chakula chake cha usiku bila ya israfu wala
kujidhili. Halafu tena huswali swala ya Ishaa pamoja na suna zake zote na
huiakhirisha suna ya Witri kama ana mazoea ya kuamka usiku kuswali. Na
iwapo hana mazoea hayo huiswali kabisa kabla ya kulala. Na pengine
muislamu anaweza kuakhirisha kula chakula chake cha usiku mpaka baada ya
kuswali swala ya Ishaa. Ni sawa kufanya hivyo ila tu kama kitawekwa
chakula sambamba na kuingia wakati wa swala, hapo atatakiwa kula kwanza
kisha ndio aswali kama ilivyokuja katika hadithi ya Mtume-Rehema na Amani
zimshukie: “Itakapokimiwa swala na ikahudhuria ‘Ashaa’-(chakula cha
usiku), basi anzeni na hiyo Ashaa”. Bukhaariy & Muslim.
Falsafa na hekima ya kauli hii ya Mtume inayotupa fursa ya
kukitanguliza chakula juu ya swala ni kumfanya muislamu aswali bila ya
moyo wake kushughulishwa na kitu kingine zaidi ya kunong’ona na Allah
Bwana Mlezi wake. Kabla ya kulala muislamu anaweza kukidhi baadhi ya haki,
mithili ya ziara fupi kwa ndugu, jamaa na marafiki bila ya kuwasahau
majirani. Kadhalika kunampasa muislamu kujipangia utaratibu wa kujisomea
kila siku kwa lengo la kujiongezea maarifa yake kama Allah alivyomwambia
Mtume wake: “...NA (uombe) USEME: MOLA WANGU NIZIDISHIE ELIMU”
[20:114]
Kauli hii ya Allah kwa Mtume wake kama inaashiria jambo,
basi jambo hili halitakuwa jingine bali ni kumtaka muislamu awe na njia na
utaratibu ambao utamuhakikishia kuzidi kielimu siku hata siku. Na ni vema
kwake yeye ikiwa atateua kujisomea vitabu na magazeti/majarida
yatakayomnufaisha katika dini na dunia yake.
Si dhambi na wala si hatia kwa muislamu kuistarehesha
nafsi yake kwa burudani, michezo na pumbao za halali katika sehemu ya
kipindi cha mchana au usiku. Kwa sharti kwamba burudani yake hiyo isichupe
mipaka kiasi cha kumfanya kuipoteza:-
Haki ya Mola wake katika ibada, au
Haki ya jicho lake kaitka kulala, au
Haki ya mwili wake katika kupumzika, au
Haki ya familia yake katika uangalizi na usimamizi, au
Haki ya kazi yake katika tija na ufanisi, au
Haki miongoni mwa haki za watu wengine.
Kadhalika si wema na wala si uwalii na Ucha-Mungu kwa
muislamu kukesha sehemu kubwa ya usiku au kila usiku mpaka akakosa nishati
(nguvu) ya kutekeleza baadhi ya haki zinazompasa na kumuwajibikia.
Muislamu hatakiwi kukesha usiku kucha kuswali, halafu asubuhi akawa
anasinzia kazini na kushindwa kuyatekeleza vema majukumu yake. Bali
anatakiwa kuwa na mizani sawa baina ya amali zake, asipunje au kuzidisha
upande mmoja. Hili linatokana na falsafa ya mizani kwamba kuzidisha upande
mmoja wa kitanga cha mizani kunamaanisha kupunja upande wa pili wa mizani
hiyo hiyo. Na kufanya hivyo ni kuikhalifu amri ya Mwingi wa rehema (Allah)
iliyomo ndani ya kitabu chake kitukufu: “ILI MSIDHULUMU KATIKA KUPIMA
(na mengineyo). BASI PIMENI KIPIMO KWA HAKI WALA MSIPUNGUZE MIZANI”.
[55:8-9]
Na katika jumla ya mambo ambayo muislamu ni wajibu wake
kuyakumbuka na wala asiyasahau katika kila siku inayompitia, ni haki ya
jamii. Hii ni haki ambayo Allah Mola Mwenyezi ameiamrisha katika kitabu
chake aliposema: “MUABUDUNI ALLAH NA WALA MSIMSHIRIKISHE NA KITU CHO
CHOTE. NA WAFANYIENI IHSANI WAZAZI WAWILI, NA JAMAA NA MAYATIMA NA
MASIKINI NA JIRANI WALIO KARIBU NA JIRANI WALIO MBALI, NA RAFIKI WALIO
UBAVUNI (mwenu) NA MSAFIRI ALIYEHARIBIKIWA NA WALE ILIYOWAMILIKI MIKONO
YENU YA KULIA. BILA SHAKA ALLAH HAWAPENDI WENYE KIBURI WAJIVUNAO”.
[4:36] Ya mwanzo na kubwa ya haki zote ni haki ya Allah Mola Mtukufu,
Muumba viumbe, Mmiliki wa vyote, Mtoa bure uhai na Mwenye neema zote:
“NA NEEMA YO YOTE MLIYONAYO, BASI IMETOKA KWA ALLAH...” [16:53] Basi
hakumuhalalikii muislamu ye yote awaye kughafilika na kuzembea katika
kuitekeleza haki ya Allah. Na ya mbele katika haki za kila siku za Allah
ni swala, swala ambayo Allah ameufanya wasifu wa mwanzo wa waumini ni
kunyenyekea ndani yake: “HAKIKA WAMEFUZU WAUMINI. AMBAO KATIKA SWALA ZAO
HUWA WANYENYEKEVU”. [23:1-2] Na wasifu wao wa mwisho ni kuihifadhi
swala: “NA AMBAO SWALA ZAO WANAZIHIFADHI” [23:9]
Na akawafaradhishia jangwa la moto/adhabu kali wale wote
ambao huipuuza swala mpaka ukawafutu wakati wake maalumu uliowekwa na
sheria: “BASI ADHABU KALI ITAWATHIBITIKIA WANAOSWALI. AMBAO
WANAZIAKHIRISHA SWALA ZAO (wakaziswali nje ya wakati wake)”. [108:4-5]
Baada ya haki ya Allah na ya Mtume wake, haki inayofuatia
ni haki ya wazazi wawili; baba na mama. Haki hii ya kuwatendea wema wazazi
katika kitabu cha Allah imekuja ikiiandamia ‘Tauheed’-(kumpwekesha
Allah) na mahala pengine ikiiandamia ‘Ikhlaaswi’-(kufanya ibada kwa
ajili ya Allah tu). Ikiwa kuja kwa haki hii kwa mtiririko huu kunaashiria
jambo, basi jambo hilo halitakuwa ila ni kuonyesha uzito wa haki ya wazazi
wawili. Kwamba hakuna haki iliyo juu ya haki ya wazazi baada ya haki ya
Allah na Mtume wake. Na kati ya haki za wazazi wawili, Qur-ani Tukufu na
suna toharifu zinampa mama umuhimu na upendeleo wa pekee kuliko baba. Hili
linatokana na majukumu mazito anayoyabeba yeye kama mama kwa watoto na mke
kwa mume. Majukumu ambayo hayawezwi kubebwa na mwingine ye yote ila yeye
pekee. Sehemu ya majukumu hayo mazito ni pamoja na taabu na adha
zinazomsibu tangu kutunga kwa mimba, kujifungua na kulea: “...MAMA YAKE
AMECHUKUA MIMBA YAKE KWA TAABU NA AKAMZAA KWA TAABU. NA KUBEBA MIMBA YAKE
HATA KUMUACHISHA ZIWA (uchache wake) NI MIEZI THALATHINI...” [46:15]
Baada ya haki ya wazazi, inayofuatia ni haki ya jamaa.
Jamaa zako kiislamu ni pamoja na nduguzo wa kiume na wale wa kike (kaka na
dada zako), maami (baba wakubwa na wadogo), mashangazi, wajomba,
makhalaati (mama wakubwa na wadogo). Na watoto wa wote hawa tuliowataja na
baki ya ndugu wengine wa nasabu (damu). Kisha zinaandamia haki za wanyonge
na wasiojiweza katika jamii, hawa ni pamoja na mayatima, masikini na
wasafiri walioharibikiwa safarini. Halafu tena ndio zinafuatia haki za
jirani wa karibu na yule wa mbali na rafiki wa ubavuni. Huyu ni yule
unayesuhubiana naye pamoja ama mjini ama safarini kwa wasifu wa kudumu au
wa muda maalumu. Na anaingia chini ya tafsiri hii ya ‘rafiki wa
ubavuni’, mke kwa mumewe na mume kwa mkewe. Ya mwisho ya haki hizi ni
haki ya ‘milki ya kuumeni’ : “...NA WALE ILIYOWAMILIKI MIKONO YENU
YA KULIA (kuume)...” Haki hii katika aya hii ijapokuwa inamuelekea moja
kwa moja mtumwa na uwajibu wa kumtendea wema katika zama zile za utumwa.
Lakini aya hii kwa kuzingatia ‘ueneaji wa tamko lake’ inakikusanya na
kukichanganya kila kilicho chini ya milki ya mtu. Hapo ndipo wanapoingia
watumishi wa majumbani, waajiriwa wa maofisini na mashambani, na zana na
vitendea kazi vyote. Wote na vyote hivi anaamrishwa kuvitendea wema kwa
kuvihifadhi, kuvichunga dhidi ya madhara au uharibifu wo wote ule.
KULALA:
Sasa ni wakati wa kulala baada ya kuikamilisha ratiba hiyo
ya kutwa nzima. Muislamu anapotaka kulala, ni suna atie udhu na kuswali
rakaa mbili. Kisha ndipo apande kitandani kwake akilalia ubavu wake wa
kulia, ilhali anamdhukuru Allah kwa dhikri zilizopokewa kutoka kwa Mtume
wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Mithili ya kauli yake Bwana Mtume:
“BISMIKA RABBIY WADHWA’ATU JANBIY, WABIKA ARFA’UHU, IN AMSAKTA
NAFSIY FAGHFIR LAHAA, WA IN ARSALTAHAA FAHFADHW-HAA BIMAA TAHFADHWU BIHII
‘IBAADAKAS-SWAALIHIYN” Na nyinginezo nyingi mithili ya hii. Ni muhimu
muislamu akavisoma vitabu vilivyoandikwa na wanazuoni wetu katika uwanja
wa kauli na amali za kidini anazotakiwa kuzifanya asubuhi, jioni na usiku.
Tunamshauri pamoja na vitabu vinginevyo, kusoma vitabu vifuatavyo:-
‘Amalul-yaumi wal-laylah : Imamu Nasaai
Al-adhkaar : Imamu Nawawiy
Al-hiswnul-haswiyn : Ibn Al-jazariy.
Ndugu mpenzi msomaji wetu, kwa faida yako ili uzijue vema
‘haki jamii’, rejea darsa zetu za HAKI NA WAJIBU katika somo la
AKHLAAQ. Kadhalika kwa ufafanuzi wa taratibu za kulala, tunakushauri
urejee somo la ‘ADABU ZA KULALA’ katika mada ya Akhlaaq.
|