Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Dini ni nasaha, wakauliza kwa nani ? Akasema Mtume : Kwa Allah, Mtume wake, kwa viongozi wa waislamu na watu wa kawaida" Hadith Tukufu

UTARATIBU WA MAISHA YA KILA SIKU YA MUISLAMU...V.

 

Muislamu akitaka kubarikiwa katika umri wake, basi hana budi kuishi kwa kuufuata utaratibu wa maisha ya kila siku kama ulivyo katika mfumo safi na sahihi wa maisha (Uislamu). Utaratibu huu chini ya mfumo huu, unamtaka muislamu kuamka na kulala mapema kama hana la muhimu la kumshughulisha wakati huo. Siku kwa muislamu huanza mapema tangu kuchomoza kwa alfajiri au kwa uchache kabla ya kuchomoza kwa jua. Kwa utaratibu huu wa kuamka mapema, muislamu huipokea asubuhi yake hali ya kuwa ni twahara safi kabla haijachafuliwa na pumzi za wenye dhambi, ambao hawaviachi vitanda vyao ila jua la saa nne saa sita. Utaratibu huu humpa muislamu fursa ya kuipokea siku yake na ‘umapema’ ambao Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-aliuombea umati wake baraka ndani yake: “Ewe Mola wa haki wee! Ubarikie umati wangu katika mapema yao”. Ahmad, Ibn Hibbaan, Al-Haakim, Ibn Maajah & wengineo.

Miongoni mwa maafa/mabalaa waliyotahiniwa nayo waislamu wa leo ni pamoja na kubadilisha kwao utaratibu wa siku yao. Leo utawashuhudia waislamu wakikesha katika luninga (televisheni) zao mpaka usiku mwingi. Kisha ndipo hupanda vitandani wakakoroma mpaka swala yenye fadhila kubwa (Sub-hi) ikawapita. Swala ambayo Allah anaielezea: “...NA (msiache) QUR-ANI YA (swala ya) ALFAJIRI. HAKIKA (kusoma) QUR-ANI KATIKA (kuswali swala ya) ALFAJIRI KUNAHUDHURIWA (na Malaika)”. [17:78]

Mmojawapo wa wahenga wetu wema (salafu)-Allah awarehemu-alipata kusema: “Ninamstaajabia mtu mwenye kuswali (swala ya) Sub-hi baada ya kuchomoza jua, vipi ataruzukiwa!” Imepokewa na Abuu Hurayrah-Allah amuwiye radhi-kutoka kwa Mutme wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-amesema: “Shetani hufunga kichogoni kwa mmoja wenu anapolala mafundo matatu, hupiga chapa katika kila fundo: Uwe juu yako usiku mrefu, lala. Akiamka akamdhukuru Allah, hufunguka fundo moja na akitawadha (kwa ajili ya swala) hufunguka fundo la pili. Na akiswali, hufunguka mafundo yote matatu, basi akaamka akiwa mchangamfu mwenye nguvu na mwema wa nafsi. Na kama hakufanya hivyo atapambaukiwa akiwa mbaya wa nafsi na mvivu”. Bukhaariy

Huu ndio muongozo wa kufuatwa na kila muislamu kwa maslahi na manufaa yake. Muislamu huianza siku yake kwa kumtii Allah kwa kuswali swala ya fardhi na suna. Kwa kusoma nyiradi za asubuhi zilizopokewa kutoka kwa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-mithili ya nyiradi hizi: ASW-BAHANAA WA ASW-BAHAL-MULKU LILLAAH, WAL-HAMDULILLAAH, LAA SHARIYKA LAHUU, LAA ILAAHA ILLAA HUWA, WA ILAYHIN-NUSHUUR” . “ALLAAHUMMA MAA ASW-BAHA BIY MIN-NI’IMATIN AU BIAHADIN MIN KHALQIKA FAMINKA WAHDAKA LAA SHARIYKA LAKA, FALAKAL-HAMDU WALAKAS-SHUKRU”. “ALLAAHUMMA INNIY ASW-BAHATU MINKA FIY NI’IMATIN WA ‘AAFIYATIN WASITRI, FAATIM NI’IMATAKA ‘ALAYYA WA ‘AAFIYATAKA WASITRAKA FID-DUNIYAA WAL-AAKHIRAH”. Kisha asome Qur-ani Tukufu kiasi cha uwezo wake, ayasome maneno matukufu ya Mola wake kwa unyenyekevu mkubwa, ufahamu wa maana na huku akileta mazingatio: “(Na hiki) KITABU; TUMEKITEREMSHA KWAKO, CHENYE BARAKA NYINGI, ILI WAPATE KUZIFIKIRI (kuzizingatia) AYA ZAKE NA WENYE AKILI WAWAIDHIKE”. [38:29] Halafu tena ndipo apate kifungua kinywa chake kwa wastani bila ya kushiba kupita kiasi. Akimaliza ndipo aelekee kazini kwake kwa ajili ya ibada ya kutafuta riziki yake ya halali, kwani muislamu hali bila ya kufanya kazi. Muislamu anatakiwa kuizingatia kazi yake kuwa ni sehemu ya ibada aliyoumbiwa au kwa maneno mengine ni sehemu isiyotengeka ya dini yake. Ibada hii ya kutafuta riziki yake ya halali isimsahaulishe kumdhukuru Allah Mola Mtoa riziki anayoitafuta kila unapoingia wakati wa swala. Kazi hii muda wa kuambiwa kuwa ni ibada na ni ibada kweli inayompatia thawabu ikiwa ni ya halali na kinyume chake pia kinafanya kazi, isiwe ni kisingizio cha kuacha swala kama ibada mama, bali kwa muumini mkamilifu wa imani ni kazi na swala. Na katika huko kufanya kazi, muislamu anatakiwa kuifanya kazi yake kwa ukamilifu na uaminifu utakaoleta tija ili kufikia ufanisi na kupata matunda halali ya jasho lake. Ukamilifu na ufanisi kazini ni fardhi kwa muislamu kama alivyoambiwa na Mtume wake-Rehema Amani zimshukie: “Kwa yakini Allah anapenda anapofanya kazi mmoja wenu, (aifanye kwa) ukamilifu (ufanisi na ustadi)”. Al-Baihaqiy, Abuu Ya’alaa & Ibn ‘Asaakir.

Katika jumla ya wajibu na majukumu ya kila siku ya muislamu ambayo hakumjuzii kuyasahau au kuzembea kuyatekeleza ni wajibu wa utumishi wake kwa jamii yake. Na kuisaidia kwa namna moja au nyingine kufikia malengo na haja zao. Autekeleze wajibu wake huu kwa moyo mkunjufu huku akiamini kuwa hiyo ni sadaka. Imepokelewa na Abuu Muusa-Allah amuwiye radhi-kutoka kwa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie: “Kunamlazimu kila muislamu (kutoa) sadaka, (maswahaba) wakamuuliza: Ewe Mtume wa Allah je, kama hana (cha kutoa sadaka)? Akajibu: “Afanye kazi kwa mkono wake ili ajinufaishe yeye mwenyewe na atoe sadaka. Wakamuuliza (tena): Je, kama hakuweza (kufanya kazi)? Akasema: “Amsaidie mwenye haja aombaye msaada. Wakauliza (tena): Je, kama hakufanya hivyo? Akajibu: “Basi na aamrishe mema (huku akiyatenda). Wakauliza (tena): Je, kama hakufanya hivyo? Akawajibu: “Basi na ajizuie na shari (uovu), kwani hakika (kufanya hivyo) ni sadaka”. Bukhaariy & Muslim

Sadaka hii au tuseme kodi hii ya kijamii ni fardhi ya kila siku kwa kila muislamu. Kwa kuitekeleza sadaka hii iliyofaradhishwa na Mtume wake, anakuwa ni chemchem inayobubujisha kheri, manufaa na salama kwa jamii inayomzunguka.

Kadhalika imepokelewa katika hadithi iliyotajwa na Abuu Hurayrah-Allah amuwiye radhi-amesema: Amesema Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie: “ Kila mfupa/maungio/kiungo cha watu kinalazimikiwa na sadaka katika kila siku ichomozewayo na jua:

Kufanya uadilifu baina ya wawili ni sadaka, na

Kumsaidia mtu katika kipando chake (mnyama/gari n.k.) ukampandisha au ukampakilia mzigo wake juu ya mnyama huyo ni sadaka, na

Neno jema (zuri) ni sadaka, na

Kila khatua unayopiga kwenda kuswali ni sadaka, na

Kuondosha adha (chupa, jiwe, kinyesi n.k.) njiani ni sadaka”. Bukhaariy & Muslim

 

Kwa kuyafanyia kazi maneno haya matukufu ya Mtukufu Mtume wetu kunampasa kila muislamu kumshukuru Allah kwa neema hii ya mifupa na viungo alivyopewa. Aishukuru neema hii kwa kuvitumia viungo na mifupa yake hiyo katika kumtii Mola wake na kuwanufaisha waja wake kwa kuwatendea wema ulio ndani ya uweza wake.

 

MCHANA:

Sasa tayari ni mchana na adhana ya adhuhuri inasikika na masikio ya kila muumini. Muislamu anasimamisha kazi, anatika mbio kwenda kuitekeleza fardhi ya swala kwani kaambiwa katika adhana (ALLAAHU AKBAR) yaani Allah ni Mkubwa kuliko kila kitu, ikiwa ni pamoja kazi yake hiyo. Anajitahidi upeo wa juhudi yake kuitekeleza fardhi ya swala kwa wakati wake uliowekwa na sheria tena kwa jamaa. Muislamu anatakiwa kutambua kuwa wakati wa mwanzo wa swala ni radhi za Allah na Allah ametuamrisha kushindana katika mambo ya kheri. Ili kuusisitiza umuhimu wa swala ya jamaa, Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-alikusudia kuzichoma moto nyumba za watu wanaochelewa kuhudhuria swala za jamaa pamoja nae msikitini. Na katika kuonyesha ubora na fadhila za swala ya jamaa, Bwana Mtume akasema kwamba swala ya jamaa ni bora kuishinda swala ya mtu pweke kwa daraja ishirini na saba. Baada ya swala, muislamu huenda kupata chakula chake cha mchana kabla ya kurejea tena kazini. Chakula kitokanacho na vizuri vizuri alivyoruzukiwa na Allah Mola Mwenye kuruzuku wema na waovu bila ya kubagua. Hula bila ya israfu kiasi cha kuvimbiwa na kumfanya ashindwe kufanya kazi na badala yake alale na kukoroma. Pia katika ulaji wake huu, muislamu hajidhiki kwa kula chakula kidogo mno kisichokidhi mahitaji ya mwili wake na hivyo kumfanya kukosa nguvu na nishati itakayomuwezesha kufanya kazi. Au akajidhiki kwa kula chakula cha aina moja tu siku hata siku na kumfanya akose viinilishe muhimu vinavyohitajiwa na mwili wake. Muislamu anatakiwa kufanya kazi kwa juhudi, maarifa na ufanisi na ale, anywe, avae na aishi mahala pazuri maadam tu hafanyi israfu na ubadhirifu anaouchukia Allah. Hebu na tuitegee sikio la uzingativu kauli hii tukufu ya Allah: “ENYI WANADAMU! CHUKUENI MAPAMBO YENU (vaeni nguo zenu nzuri mzipendazo) WAKATI WA KILA SWALA, NA KULENI (vizuri) NA KUNYWENI (vizuri). LAKINI MSIPITE KIASI TU, HAKIKA YEYE (Allah) HAWAPENDI WAPITAO KIASI (wabadhirifu). SEMA: NI NANI ALIYEHARIMISHA MAPAMBO YA ALLAH AMBAYO AMEWATOLEA WAJA WAKE. NA (nani aliyeharimisha) VITU VIZURI KATIKA VYAKULA? SEMA: VITU HIVYO VIMEWAHALALIKIA WAISLAMU (hapa) KATIKA MAISHA YA DUNIA (na) VITAKUWA VYAO PEKE YAO SIKU YA KIYAMA...” [7: 31-32]

Katika nchi za joto au katika majira ya joto, watu huweza kuhitajia mapumziko kidogo ya mchana. Mapumziko haya yanajulikana katika Uislamu kama ‘Qailuulah’-(siesta). Mapumziko haya yana msaada mkubwa katika kusimama usiku kuswali na katika kuamka mapema. Qur-ani Tukufu imeyaashiria mapumziko haya katika kauli tukufu ya Allah: “...NA MNAPOVUA NGO ZENU ADHUHURI...” [24:58]



Forum | Guestbook | Tuandikie |