|
WAJIBU WA
MUISLAMU KUELEKEA WAKATI….IV
vi) KILA WAKATI NA
AMALI YAKE.
Inampasa muumini
kujua linalotakiwa kutendwa katika wakati alionao; aliomo hivi sasa ndani
yake. Je, ni wakati wa amali ya moyo, ulimi au viungo? Akishajua ni wakati
wa amali gani kati ya hizo tulizozitaja, aipanie na kujitahidi kuitenda
kiasi cha kuoana na makusudi yake na hivyo kuipa nafasi kubwa ya kuweza
kukubaliwa mbele ya Allah.
Imekuja katika wasia
wa Amirul-Muumini Abuu Bakri kwa Sayyidna Umar-Allah awawiye radhi-wakati
anamuachia ukhalifa: “Tambua kwamba Allah anazo amali (anazotaka
zitendwe) wakati wa mchana, hakubali (zitendwe) wakati wa usiku.”
Itakuwazikia basi,
kwamba suala si mtu kufanya cho chote wakati wo wote, bali muhimu ni mtu
kufanya amali munasibu katika wakati muafaka. Ni kutokana na ukweli huu
kwamba kila wakati una amali yake inayonasibu kufanywa ndani yake.
Tunamuona Allah ameziwekea nyakati maalum ibada nyingi, haijuzu kwa
muumini kuzitenda kabla au baada ya nyakati hizo. Mathalan haisihi kufunga
swaumu ya Ramadhani katika mwezi wa Dhul-Hijah kama ambavyo isivyosihi
kufanya ibada ya Hijah katika mwezi wa Ramadhani, kwa sababu sio wakati
wake uliowekwa na sheria. Allah ameyafanya haya kwa hekima na busara,
miongoni mwa hekima za kuziwekea nyakati maalum kathiri (nyingi) ya ibada.
Ni pamoja na kutufahamisha kwamba kitu/jambo/amali haikubaliwi kabla ya
kuingia wakati wake wala baada ya kupita wakati wake. Allah Mola Mwenyezi
amesema kuhusiana na suala la swala: “KWA HAKIKA SWALA KWA WAUMINI NI
FARDHI ILIYOWEKEWA NYAKATI MAKHSUSI.” (4:103)
Na akasema katika
swaumu: “…ATAKAYEKUWA KATIKA MJI KATIKA HUU MWEZI (wa Ramadhan) NA
AFUNGE…” (2:185)
Na katika Hijah
akasema: “HIJA NI MIEZI MAALUM….” (2: 197)
Na katika zakah
akasema: “…NA TOENI HAKI YAKE SIKU YA KUVUNWA KWAKE….” (6: 141)
Anasema mmoja
miongoni mwa waja wa Allah wenye kuzijua neema na ihsani zake – Allah
awarehemu: “Nyakati za mja ni nne hazina wa tano wake:
-Wakati wa neema,
-Wakati wa balaa
(mitihani ya maisha),
-Wakati wa twaa, na
-Wakati wa maasi.
Na ana Allah juu
yako katika kila wakati miongoni mwa nyakati hizi sehemu (hisa) ya
uja/utumwa ambao ni haki yake kwako kwa mujibu wa hukumu ya ubwana/ulezi
na uungu wake. Basi utakayekuwa wakati wake ni twaa, basi njia yake ni
kushuhudia neema kutoka kwa Allah kumshukia yeye kwa kumuongozea katika
twaa na kumuwafikisha kuitenda. Na utakayekuwa wakati wake ni neema, basi
njia yake (ya kuidumisha neema hiyo) ni shukrani, nayo ni furaha ya moyo
kwa Allah. Na
utakayekuwa wakati wake ni maasia, basi njia yake (ya kujinasua nayo) ni
toba na Istighfaari. Na utakayekuwa wakati wake ni balaa (majanga) basi
njia yake (ya kuyashinda) ni kuridhia (kuwa yanatoka kwa Allah) na
kusubiri (faraja kutoka kwake).”
Maneno haya yenye
thamani aliyoyasema mja huyu wa Allah aliyewafikiwa kuzijua neema na
ihsani za Mola wake. Yanayaeleza na kuyatafsiri yaliyotamkwa na Qur-ani na
Sunah katika safu (makamu) ya twaa, Allah Mola Mwenyezi
anasema: “SEMA:KWA
FADHILA ZA ALLAH NA KWA REHEMA YAKE (ndiyo mumepata haya) BASI NA WAFURAHI
KWA HAYO. HAYA NI BORA KULIKO HIVYO WANAVYOVIKUSANYA.” (10:58)
Na katika safu ya
maasia anasema: “SEMA: ENYI WAJA WANGU MLIOJIDHULUMU NAFSI ZENU (kwa
kutenda maasi)! MSIKATE TAMAA NA REHEMA YA ALLAH, BILA SHAKA ALLAH
HUSAMEHE DHAMBI ZOTE (kwa mwenye kutubia na kutubu na kuleta Istighfaari )
HAKIKA YEYE NI MWINGI WA KUSAMEHE (na) MWINGI WA KUREHEMU.” (39:53)
Na anasema katika
safu ya balaa (majanga/misiba): “NA TUTAKUTIENI KATIKA MSUKOSUKO WA
(baadhi ya mambo haya); KHOFU NA NJAA NA UPUNGUFU WA MALI NA WA WATU NA WA
MATUNDA NA WAPASHE KHABARI NJEMA WANAOSUBIRI AMBAO UWAPATAPO MSIBA HUSEMA:
HAKIKA SISI NI WAJAWA ALLAH NA KWAKE YEYE TUTAREJEA (atatupa jaza
yake).” (2:155-156)
Ama katika Sunah,
imepokelewa kwamba Mtume wa Allah– Rehema na Amani zimshukie–amesema:
“Ajabu iliyoje kwa jambo la muumini, hakika jambo lake lote ni kheri na
hilo halipatikani kwa ye yote ila kwa muumini tu. Ikimpata raha (la
kufurahisha) hushukuru na ikawa ni kheri kwake na ikimpata taabu (la
kuhuzunisha) husubiri na ikawa ni kheri kwake.” Muslim
vii). KUZENGEA
NYAKATI BORA; ZENYE FADHILA.
Linalotakikana
kufanywa na muislamu mwenye pupa ya kushindana katika mambo ya kheri ni
kuzizengea nyakati bora. Nyakati ambazo Allah amezipendelea kuliko nyakati
nyingine kwa kuzipa hadhi na heshima ya pekee ya
kiroho. Heshima na
hadhi inayoainisha ubora na fadhila zake, kama ilivyopokewa katika
hadithi: “Hakika yuna Mola wenu katika zama zenu vipawa, basi vizengeeni
(vipawa hivyo)” Twabaraaniy
Ukhusishaji huu wa
nyakati fulani kwa ubora na fadhila ni suala la kimungu, kwani Allah
humkhusu (humtemshia) kwa rehema zake amtakaye na kwa akitakacho. Kama
ambavyo Allah alivyowaboresha (alivyowafanya bora) baadhi ya waja wake
zaidi kuliko wengine: “MITUME HAO TUME WAFADHILISHA (tumewaboresha)
BAADHI YAO ZAIDI KULIKO WENGINE MIONGONI MWAO WAKO AMBAO ALLAH
ALISEMA NAO NA
WENGINE AKAWAPANDISHA KATIKA VYEO
VIKUBWA KABISA…”
(2:253)
Na akaziboresha
baadhi ya sehemu katika ardhi yake zaidi kuliko sehemu nyingine. Kadhalika
ameziboresha na kuzifadhilisha zaidi baadhi ya nyakati kuliko nyingine:
“NA MOLA WAKO HUUMBA ATAKAVYO NA HUCHAGUA (atakavyo) HAWANA (viumbe)
KHIYARI…..” (28:68)
Allah Mola Mwenyezi
ameyafadhilisha katika usiku masaa (nyakati) ya maladaku (nyakati za kabla
ya alfajiri). Haya ni masaa ya theluthi ya mwisho ya usiku, ambamo Allah
hujidhihirisha kwa waja wake kila usiku kwa kuwashukia ushukaji
unaolingana na dhati yake tukufu. Basi hunadi (hulingana): “Je, yuko
mwenye kutaka maghfira (msamaha) nimghufirie? Je, yuko mwenye kutubu
nimpokelee toba yake? Je, yuko mwenye kuomba (nimpe ambacho). Je, yuko
mwenye haja (nimkidhie)? (Huendelea kunadi hivyo) mpaka
kuchimbuka
(kuchomoza) kwa alfajiri”. Ahmad & Muslim
Kwa ajili hiyo Allah
amewasifia waja wake wema wamchao kwa kusema: “KWA YAKINI WAMCHAO ALLAH
WATAKUWA KATIKA MABUSTANI NA CHEMCHEM WANAPOKEA ALIYOWAPA MOLA WAO KWA
HAKIKA WAO WALIKUWA WAKIFANYA WEMA KABLA YA HAYA. WALIKUWA WAKILALA KIDOGO
TU USKU NA WAKIOMBA MAGHUFIRA (msamaha)
NYAKATI ZA KABLA YA
ALFAJIRI.” (51:15-18) Nae Bwana Mtume-Rehema na Amani
zimshukie–anasema: “Wakati ambao Bwana Mlezi anakuwa karibu mno na mja
wake ni ndani ya sehemu ya mwisho ya usiku. Basi ukiweza kuwa miongoni mwa
wanaomdhukuru Allah katika nyakati hizo, basi kuwa (miongoni mwao).”
Tirmidhiy, Nasaai,
Al-Haakim & wengineo
Na Allah ameichagua
na kuifadhilisha zaidi siku ya Ijumaa miongoni mwa siku saba za juma. Siku
hii ya Ijumaa ni Idi (siku kuu) ya juma kwa waislamu na ndani ya siku hii
kuna fardhi ya swala ya Ijumaa. Swala ambayo kuwakusanya pamoja waislamu
wa kitongoji fulani mahala pamoja. Ndani ya siku hii kuna muda maalumu (wa
upendeleo) ambao hujibiwa maombi ya waombaji. Muislamu hausadifu muda huo
akimuomba Mola wake jambo la kheri ila humpa. Imekuja katika hadithi:
“Bora ya siku iliyochomozewa na jua ni siku ya Ijumaa…” Na ndani
yake kuna muda ambao hausadifu mja muumini na il-hali yu ndani ya swala
akimuomba Allah cho chote ila humpa kitu hicho.” Ahmad
Na katika siku za
mwaka mzima, Allah ameyafadhilisha masiku kumi ya mwezi wa Dhul-Hijah
(Mfunguo tatu) kiasi cha kuyaapia: “NAAPA KWA ALFAJIRI. NA MASIKU KUMI
(ya mwanzo ya Dhul-Hijah)”. [89:1-2]. Na bora ya masiku kumi haya ni ile
siku ya Arafah (mwezi tisaa-Dhul-Hijah). Imepokewa kutoka kwa Ibn
Abbas–Allah awawiye radhi: “Hapana miongoni mwa masiku (ya mwaka
mzima) yapendezayo zaidi kwa Allah kufanya amali ndani yake kuliko masiku
haya (kumi).” Maswahaba wakauliza: Ewe Mtume wa Allah wala kuliko
kupigana jihadi katika dini ya Allah? Mtume akawajibu: “Wala jihadi
katika dini ya Allah (hailingani na amali inayotendwa katika masiku haya
kumi). Ila mtu atoke (katika njia ya Allah) kwa nafsi na mali yake
(mwenyewe), na kisirejee cho chote katika hivyo (yaani afe shahidi)”.
Bukhaariy.
Na katika miezi kumi
na mbili inayofanya mwaka mmoja, Allah ameukhitari na kuufadhilisha mwezi
wa Ramadhan. Huu ni mwezi ambao imeteremshwa Qur-ani Tukufu ndani yake ili
iwe ni muongozo kwa watu wote na upambanuzi wa baina ya haki na batili.
Mwezi ambao Allah amewafaradishia waja wake ibada ya funga (swaumu) na
Mtume wake akawasunishia kisimamo cha usiku (tarawehe). Ndani ya mwezi huu
kumependekezwa kukithirisha amali njema, za kheri. Kwa hivyo, basi mwezi
huu ambao ni chaguo la Allah kwa waja wake waumini ni musimu wa kushindana
katika mambo ya kheri kwa ajili tu ya kutaraji radhi za Allah. Imepokelewa
kutoka kwa Ubaadah Ibn As-swaamit–Allah amuwiye radhi–kwamba Mtume wa
Allah–Rehema na Amani zimshukie siku moja alisema wakati ulipoingia
mwezi wa Ramadhani: “Imekujieni Ramadhan, mwezi wa baraka, Allah
anakufunikeni ndani yake na kwa sababu hiyo rehema yake hukushushieni na
madhambi huyapomosha (huyafuta). Huyajibu maombi yenu, Allah huyaangalia
mashindano yenu (katika kheri na wema) ndani yake (mwezi huu) na
hujifakharisha nanyi kwa malaika wake. Basi muonesheni Allah kheri katika
nafsi zenu (kwa kutenda amali njema), kwani kwa yakini mtu muovu ni yule
aliyenyimwa rehema za Allah Mtukufu ndani yake (mwezi huu).” Imani
Suyuutw (Al-Jaamiul-Kabiyr). Mwezi mzima wa Ramadhan ni mwezi muhimu kwa
muislamu, lakini sehemu yenye umuhimu zaidi kwa muislamu, kuliko nyingine
ni ile theluthi yake ya mwisho, yaani kumi lake la mwisho. Umuhimu mkubwa
wa kumi hili unatokana na mambo mawili ya msingi:-
-Kumi hili ndio
mwisho wa mwezi huu mtukufu na kwa yakini amali zote huzingatiwa mwishoni
na sio mwanzoni. Hili linatokana na imkani ya kuanza vema na kumaliza
vibaya, kwa mantiki hii ndio ikawa mazingatio ya mambo/amali ni mwisho
wake. Ni kwa kulizingatia na kulijua hili ndio ikawa katika jumla ya dua
za Bwana Mtume–Rehema na Amani zimshukie-ni kauli yake: “Ewe Mola wa
haki wee! Ninakuomba ujaalie bora (kheri) ya umri wangu mwisho wake, na
bora ya amali zangu mwisho wake na bora ya siku zangu siku ya kukutana
nawe.”
Kumi hili ndilo
linalodhaniwa kuwemo ndani yake “Laylatul-Qadri.” Huu ni usiku ambao
Allah Mola Mwenyezi ameufadhilisha zaidi kuliko miezi alfu moja na
kutokana na ubora wake ukapewa sura kamili ndani ya Qur-ani Tukufu:
“HAKIKA TUMEITEREMSHA (Qur-ani) KATIKA LAYLATUL– QADRI (usiku wenye
heshima kubwa, usiku mwa mwezi wa Ramadhan). NA JAMBO GANI
LITAKALOKUJULISHA (hata ukajua) NI NINI HUO USIKU WA LAYLATUL-QADRI? HUO
USIKU WA HISHIMA (huo) NI BORA KULIKO MIEZI ELFU. HUTEREMKA MALAIKA NA
ROHO (za viumbe watakatifu) KATIKA (usiku) HUO KWA IDHINI YA MOLA WAO KWA
KILA JAMBO. NI AMANI (usiku) HUO MPAKA MAPAMBAZUKO YA ALFAJIRI.”
(97:1-5)
Bwana Mtume–Rehema
na Amani zimshukie-alikuwa akifunga kibwewe linapoingia kumi la mwisho (la
Ramadhan) na kuuhuisha usiku wake. Na akiwaamsha wakeze (kufanya ibada) na
alilikhusisha (kumi hili) na ibada ya Itikafu.
Na katika miezi kumi
na mbili ya mwaka, Allah ameifadhilisha miezi mine mitukufu baada ya
Ramadhan. Miezi minne hiyo ni Rajab, Dhul Qa’adah, Dhul-Hijah na
Muharam. Tusome: “IDADI YA MEZI (ya mwaka mmoja) MBELE YA ALLAH NI MIEZI
KUMI NA MBILI KATIKA ILIMU YA ALLAH (mwenyewe tangu) SIKU ALIPOUMBA MBINGU
NA ARDHI KATIKA HIYO IMO MINNE ILIYO MITUKUFU KABISA (nayo ni Rajabu,
Mfunguo pili, Mfunguo tatu na Mfunguo nne)…” (9:36)
|