|
WAJIBU WA
MUISLAMU KUELEKEA WAKATI….IV
III/. KUYAENDEA
HARAKA MAMBO YA KHERI.
Linalofaa na
kunasibu kutendwa na muumini baada ya kujua thamani na umuhimu wa wakati
ni pamoja na kuutumia wakati wake katika kufanya mambo mbali mbali ya
kheri (mema). Ahakikishe kuwa wakati wake unatumika katika mambo yote
ambayo manufaa na maslahi yake yatamrejea yeye binafsi kama mtendaji. Bila
ya kuinyima manufaa hayo familia na jamii yake kwa ujmla leo ulimwenguni
na kesho mbele ya Allah Mola Mwenye khabari za yote tuyatendayo ya dhahiri
na siri. Muislamu ayatende mambo ya kheri bila ya kuhitaji msukumo utokao
nje yake bali ajitume yeye mwenyewe kutokana na manufaa ya mambo hayo.
Autupilie mbali uvivu na ajizi ya kuakhirisha jambo la leo ili alifanye
kesho au kufanya mambo nusunusu bila ya ukamilifu. Miongoni mwa dua na
dhikri ambazo Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-ameufundisha umati
wake kuzisoma asubuhi na jioni ni pamoja na: “Ewe Mola wa haki wee!
Hakika mimi ninakuomba unikinge na wasiwasi wa moyo (hammu) na huzuni na
unikinge na ajizi na uvivu”. Kuyaendea haraka mambo ya kheri ni amri ya
Allah kama ilivyokuja ndani aya Qur-ani Tukufu: “NA KILA UMA ULIKUWA NA
QIBLAH WALICHOKIELEKEA. BASI JITAHIDINI KUFANYA MEMA...” [2:148]
Kadhalika Allah
anawaambia watu wa kitabu: “...NA KAMA ALLAH ANGALITAKA ANGEKUFANYENI
KUNDI MOJA (la kufuata sharia moja), LAKINI ANATAKA KUKUJARIBUNI KWA HAYO
ALIYOKUPENI. BASI SHINDANENI KATIKA KUYAFIKILIA MAMBO YA KHERI. NYINYI
NYOTE MARUDIO YENU NI KWA ALLAH...” [5:48]
Allah Mola mwenye
shani akaendelea kusema katika kuraghibisha pepo na neema zake zilizomo
humo: “NA YAENDEENI UPESI UPESI MAGHUFIRA YA MOLA WENU NA PEPO (yake)
AMBAYO UPANA WAKE (tu) NI (sawa na) MBINGU NA ARDHI. (Pepo) ILIYOWEKEWA
WAMCHAO ALLAH”. [3:133]
Katika aya hizi na
zenye kushabihiana nazo, Allah anawaamrisha waja wake kuyashindania na
kuyaendea haraka maghufira (msamaha wa dhambi) yake na pepo yake. Yaani
washindane na kuharakia kuziendea sababu zitakazowadhaminia kupata
maghufira na pepo ya Mola wao. Na sababu hizi si nyingine bali ni imani
thabiti, ucha-Mungu na amali njema, na kushindana katika mambo haya ni
jambo jema linalotakiwa kuazimiwa na kila muislamu: “...NA KATIKA
(kupata) HAYA WASHINDANE WENYE KUSHINDANA”. [83:26]
Katika ushindani huu
wa kheri, Allah amewasifia baadhi ya mitume wake kwa kauli yake:
“...BILA SHAKA WAO WALIKUWA WEPESI WA KUFANYA MEMA NA KUTUOMBA KWA
SHAUKU NA KHOFU NAO WALIKUWA WAKITUNYENYEKEA”. [21:90]
Na akawasifia watu
wema katika Ahlul-Kitaab kwamba wao: “WANAMUAMINI ALLAH NA SIKU YA
MWISHO NA WANAAMRISHA MEMA NA WANAKATAZA MAOVU NA WANAYAENDEA MBIO MAMBO
MEMA. NA HAO NDIO MIONGONI MWA HAO WATENDAO MEMA (kweli kweli)”. [3:114]
Kwa janibu yake
Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-hakuacha kuuamrisha umati wake
kutenda amali njema haraka haraka kabla ya kukosa nafasi kutokana na
kushughulika mno, akasema: “Hamngojei nyinyi ila utajiri unaomfanya mtu
kuwa jeuri, au ufakiri unaomsahaulisha mtu, au maradhi yenye kumfisidi au
ukongwe unaomaliza. Au mauti yenye kuandalia au Dajjaal basi (huyo) ni
shari ghaibu yenye kungojewa au kiyama basi (hicho) ni kizito sana na
kichungu kabisa”. Tirmidhiy
IV/. KUCHUKUA
MAZINGATIO KUTOKANA NA KUJA NA KUPITA KWA SIKU.
Kunampasa muumini
kuchukua mazingatio kutokana na siku zinazomjia na kupita, kwani usiku na
mchana hukichakaza kila kilicho kipya na vinakisogeza karibu kila kilicho
mbali. Kama ambavyo vinavyoupunguza umri wa kila kilicho hai na
vinamzeesha kila aliye kijana/mdogo. Hakika kupita kwa zama, na
kuandamizana kwa usiku na mchana bila ya kuwa na mazingatio sio sifa ya
muumini. Kwani katika kila siku inayopita, bali kila saa inayomalizika na
kila kipindi (kitambo) kinachopita hutokea ulimwenguni na katika mwili wa
binadamu mabadiliko na matukio mbali mbali. Yako miongoni mwa mabadiliko
hayo yanayoonekana kwa macho na yasiyoonekana ila kwa hisia tu kadhalika
yako yanayojulikana na yasiyojulikana. Katika mabadiliko na matukio yote
hayo kuna dalili na uwezo wa Allah kwa kila mwenye akili. Kama ambavyo
kuna ukumbusho kwa kila mwenye moyo na mazingatio kwa kila mwenye busara.
Hivi ndivyo Allah anavyotuambia ndani ya Qur-ani Tukufu: “BILA SHAKA
KATIKA KUUMBWA MBINGU NA ARDHI NA MFUATANO WA USIKU NA MCHANA, ZIKO HOJA
(za kuonyesha kuwepo kwa Allah) KWA WENYE AKILI”. [3:190]
Na akasema tena:
“ALLAH HUBADILISHA USIKU NA MCHANA (baada ya mchana ukaja usiku na baada
ya usiku ukaja mchana). BILA SHAKA KATIKA HAYO IMO DALILI KWA WENYE
BUSARA”. [24:44]
V/. KUUPANGIA RATIBA
WAKATI.
Kunamuwajibikia
muumini wa kweli kuupangia ratiba wakati wake na kuhakikisha kuwa
anaifuata na kuiheshimu ratiba yake hiyo. Apange katika ratiba hiyo nini
cha kufanya, kifanyweje na wakati gani na kwa muda gani. Ratiba hiyo
iyachanganye pamoja mambo yote yenye sura ya dini na yale yenye sura ya
dunia. Ayapange kulingana na umuhimu, akianzia na lile lenye umuhimu
mkubwa na kushuka chini. Alitangulize lenye kuhitaji haraka na
alicheleweshe lisilo la haraka na lenye wakati maalumu litendwe ndani ya
wakati wake huo. Miongoni mwa aliyoyapokea Bwana Mtume-Rehema na Amani
zimshukie-kutoka katika vitabu (mbao) vya Nabii Ibrahimu ni pamoja na:
“Yatakikana kwa mwenye akili kama hakushindwa na akili yake awe na mida
minne (nyakati nne):-
Muda wa
kumnong’oneza Mola wake,
Muda wa kuikagua
nafsi yake,
Muda wa kutafakari
sanaa (uumbaji) ya Allah, na
Muda wa kutafuta
haja zake (kazi) za kimaisha (chakula, maji, nguo n.k.)” Ibn Hibbaan na
Al-Haakim
Ratiba hii ya
muislamu isisahau kuweka na kutenga muda wa kupumzika, hili linatokana na
ukweli kwamba binadamu ni kiumbe anayechoka. Na hivyo kuhitajia mapumziko
yatakayomrejeshea nguvu mpya ya mwili na akili. Imamu Aliy Ibn Abiy
Twaalib-Allah amuwiye radhi-anayaelezea maumbile na udhaifu huu wa
mwanadamu, anasema: “Zipumzisheni nyoyo muda baada ya muda kwani hakika
moyo ukilazimishwa hupofua (huingia upofu ukatenda bila ya mazingatio na
kufikiria)”.
Si vema kwa muislamu
kuisonga na kuitaabisha mno nafsi yake kwa amali kiasi cha kumdhoofisha na
kumfanya kutoendelea tena na amali hiyo. Hata kama kusonga na kutaabisha
huku kutakuwa ni kwa ajili ya ibada kama swaumu za suna, kuswali usiku na
kadhalika. Siku zote muislamu anatakiwa kuwa mkatikati wa mambo, ni kwa
sababu hii ndio Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-alipowaona maswahaba
wake wamekithiri kuswali suna nyuma yake usiku, akawaambia: “Chukueni
(fanyeni) katika amali hizi (za kheri) kiasi mkiwezacho, kwani Allah
hachoki (kulipa) mpaka mchoke nyinyi (kutenda amali). Na kwa hakika amali
ipendezayo zaidi mbele ya Allah ni ile yenye kudumu hata kama ni
chache”. Bukhaariy & Muslim
Na mahala pengine
Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alisema: “Hakika dini hii ni
nyepesi, hataitilia mikazo dini hii ye yote ila itamshinda. Basi fanyeni
amali kwa ukatikati, na (kama hamuwezi kufanya kwa ukamilifu) basi fanyeni
kiasi cha kuukaribia (huo ukamilifu). Na zifurahieni thawabu (za amali
yenye kudumu hata kama ni chache)”. Bukhaariy & Nasaai
Na katika kauli yake
nyingine, Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-anampa ushauri nasaha mtu
anayebalighisha (anayezidisha kupita kiasi) kusoma Qur-ani, kuamka usiku
kuswali, na kufunga swaumu za suna. Anamnasihi kufanya amali hizo kwa
ukatikati, anasema: “Hakika mwili wako una haki juu yako, familia (mkeo)
yako ina haki juu yako na mgeni wako pia anayo haki juu yako”. Bukhaariy
Na mahala pengine
Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-aliwaasa maswahaba wake waliosema
kuwa wao sasa watazama katika twaa ya Allah na kuipa mgongo dunia. Kwa
hivyo basi hawatalala usiku bali watakesha kufanya ibada, hawatakula
mchana na kamwe hawataoa, akawaambia: “Hakika si vinginevyo, mimi
ninamchelea zaidi Allah na kumcha kuliko nyinyi. Lakini (pamoja na hivyo)
ninasimama usiku kuswali na ninalala, ninafunga na kufuturu (kula) na
ninaoa wanawake. Basi ye yote yule atakayejitenga na mwendo wangu huu si
katika mimi”. Bukhaariy
Hii ndio suna ya
Mtume wa Allah na huu ndio utaratibu wake, utaratibu na njia ya ukatikati
katika ufanyaji wa amali. Utaratibu unaoweka mizani baina ya haki ya nafsi
na haki ya Allah Mola wa nafsi. Si katika sehemu ya mafundisho ya Uislamu
muislamu kuutumia muda wake wote katika kazi, anatoka nyumbani alfajiri na
mapema na kurudi usiku wa manane. Kwa utaratibu wake huu unaoukhalifu
Uislamu anaidhulumu familia yake usimamizi, ushauri na nasaha zake na
kuwaacha watoto kulelewa na mama pekee. Kadhalika si Uislamu mume kukesha
usiku kucha kuswali kila siku, kwani kufanya hivyo ni kumnyima mke haki
yake ya kimaumbile na ni kuidhoofisha afya yake. Uislamu haujamkataza
muumini wake kujitengea muda wa kujipumzisha na kujiburudisha kwa burudani
na michezo halali itakayomjenga kiafya.
|