|
WAJIBU WA
MUISLAMU KUELEKEA WAKATI….IV
Ikiwa wakati una
thamani na umuhimu mkubwa sana kama tulivyokwishaona, kiasi cha
kuchukuliwa/kuhesabiwa kuwa ndio uhai au maisha yenyewe kabisa. Basi ni
lazima muislamu atakuwa anao wajibu mkubwa kuelekea wakati ambao ndio
rasilimali yake kuu anayoitegemea katika maisha haya na hata yale yajayo
pia. Inatakikana mno kwa muislamu huyu kuichunga, kuitunza, kuihifadhi na
kuiweka mbele ya macho yake rasilimali yake hii yenye thamani
isiyolinganishika na cho chote. Kinachompasa muislamu baada ya kuifahamu
thamani na kuutambua umuhimu huu wa wakati. Ni kuihamisha thamani hii
kutoka katika daira (mzunguko) ya maarifa na utambuzi kuitia katika daira
ya imani na matashi/matakwa. Kisha kutoka katika daira hiyo mpaka katika
daira ya amali na utendaji/utekelezaji.
- PUPA YA KUSTAFIDI (KUFAIDIKA)
NA WAKATI.
Wajibu wa
kwanza wa muislamu kuelekea wakati ni kuuhifadhi mithili ya
anavyoihifadhi mali yake bali zaidi kuliko hivyo. Awe na pupa ya kutaka
kustafidi na wakati wake wote kwa ajili ya manufaa yake katika dini yake
na dunia yake. Kadhalika ahakikishe kuwa jamii yake nayo inafaidika
kutokana na wakati wake katika ustawi wa kiroho na kimaada. Kwa janibu
(upande) hii ya kuujali na kuuhifadhi wakati, wahenga wetu wema
(salafu)-Allah awawiye radhi-walikuwa na pupa kubwa sana na wakati wao.
Hili lilitokana na kuijua kwao thamani na umuhimu wa wakati. Mwanachuoni
Al-Hassan Al-Biswriy-Allah amrehemu-anauelezea ukweli huu, anasema:
“Niliwadiriki watu walioupupia wakati wao kuliko mnavyozipupia nyinyi
dirham na dinari (pesa) zenu leo!”
Kwa utambuzi
wao huu wa thamani na umuhimu wa wakati, salafu waliuratibia wakati wao,
nini cha kufanya na kifanywe wakati gani na waliiheshimu ratiba yao
hiyo. Hivyo amali zao zikafanywa kama zilivyopangwa na kwa wakati
ziliopangiwa bila ya kupunguza au kuongeza. Kwa utaratibu wao huu mzuri
wakawa hawana wakati unaopotea bure bila ya kufaidika nao. Umar Ibn
Abdul-Aziz-Allah amuwiye radhi-anatuasa juu ya wakati, anasema:
“Hakika usiku na mchana (wakati) vinafanya kazi ndani yako, basi nawe
fanya kazi ndani yake (viwili hivyo)”.
Ufafanuzi wa
maneno haya ni kwamba kila mchana na usiku vinapopita na kwenda zao huwa
vimepunguza sehemu ya umri wako. Na kuondoka na fursa yako ya kufanya
amali ndani yake. Kwa hivyo basi utumie mchana na usiku wa leo kwa
kufanya amali itakayokunufaisha katika mchana na usiku wa kesho. Kwani
mchana na usiku wa leo ni shamba litakalokupa mavuno katika mchana na
usiku wa kesho sambamba na maisha ya milele ya akhera.
Katika
kuielezea thamani ya wakati, salafu walikuwa na msemo: Wakati ni upanga,
kama hukuutumia kukatia, utakukata wewe (kwa sababu kazi yake ni kukata
na haustahamili kukaa bila ya kukata). Na siku zote waliufanya wakati
kuwa ni chombo chao cha kusafiria kutoka katika hali duni kwenda katika
hali iliyo bora. Kwa mtindo huu waliifanya leo kuwa ni bora kuliko jana
na kesho kuwa ni bora kuliko leo. Hata mmoja wao akafikia kusema: Mtu
itakayekuwa leo yake ni kama jana yake (hakuna tofauti), basi mtu huyo
amepunjika (amekula khasara). Na mtu ambaye leo yake itakuwa mbaya
kuliko jana yake, basi mtu huyo amelaaniwa.
Salafu
walipupia kwa pupa kuu kuona kuwa siku, sehemu ya siku au hata kitambo
kidogo cha wakati hakipiti bila ya kufaidika nacho ama kwa kutafuta
elimu yenye manufaa. Au kwa kutenda amali njema au kwa kuisaidia jamii
na kadhalika. Walifanya hivi ili kuhakikisha kuwa umri wao haupotei
bure. Swahaba Ibn Masoud-Allah amuwiye radhi-alikuwa akisema:
“Sikupata kukijutia kitu cho chote mithili ya nilivyoijutia siku
iliyozama jua lake ukapungua umri wangu na isizidi amali yangu ndani
yake (siku hiyo)”. Naye swahaba mwingine alisema: Kila siku
inayonipitia nikawa sizidishi ndani yake elimu itakayoni kurubisha kwa
Allah Mtukufu, basi nisibarikiwe katika uchomozaji wa jua la siku hiyo.
- KUUFANYA NGAWIRA (NYARA)
WAKATI WA FARAGHA.
Miongoni mwa
neema ambazo watu wameghafilika nazo na kujingikiwa thamani yake na
wala hawaishukuru ni neema ya wakati wa faragha. Wakati ambao mtu huwa
amepumzika na hana la kumshughulisha wakati huo katika mambo ya lazima
ya kila siku. Imepokelewa na Ibn Abas-Allah awawiye radhi-kwamba Mtume
wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-amesema: “Neema mbili miongoni
mwa neema za Allah wamepunjwa katika neema mbili hizo wengi miongoni
mwa watu (neema hizo ni neema ya) siha (afya) na (neema ya) wakati wa
faragha”.
Bukhaariy
Wakati wa
faragha alioukusudia Bwana mtume ni ule wakati ambao mtu hana shughuli
za kimaisha ambazo kwa namna moja au nyingine humnyima fursa ya
kutenda amali njema zenye sura ya kiakhera. Kauli hii ya Bwana Mtume
haigongani na hadithi nyingine nyingi zinazohimiza kuchuma na kutafuta
maisha. Maadam hili la kutafuta maisha halimtumbukizi na kumzamisha
mtu katika bahari kina ya maisha kiasi cha kumfanya ashindwe
kuitekeleza haki ya Allah. Asili ya neno alilolitumia Bwana Mtume
“kupunja” na mahala linapotumika ni katika sekta ya biashara na
uchuuzi. Na hapa katika hadithi hii kama anavyosema mwanachuoni mkubwa
Al-Manaawiy-Allah amrehemu-anamshabihisha mtu mkalafu na mfanya
biashara. Na anaishabihisha siha (afya njema) na faragha na rasilimali
ya mkalafu huyo. Hii ni kwa sababu siha na faragha ni katika jumla ya
sababu za kupatia faida na ni zana za mafanikio. Basi ye yote
atakayeamiliana na Allah kwa kutekeleza maamrisho yake atapata faida.
Na atakayeamiliana na shetani kwa kufuata nyayo zake, huyo ataipoteza
rasilimali yake hii na kupata khasara kubwa. Katika hadithi nyingine
Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-anasema: “Itumie fursa ya
mambo matano kabla hayajakufika mambo matano...(katika jumla ya hayo):
“Itumie faragha yako kabla ya kushughulika kwako”.
Fursa hii ya
faragha haisalikii daima kuwa ni faragha isiyo na jambo la kutendwa
ndani yake. Uzoefu na hali ilivyo inaonyesha kuwa ni lazima faragha
iwe na jambo ama la kheri au la shari linalotendeka ndani yake. Ukweli
wa hili unaonekana katika maisha yetu ya kila siku, hebu waangalie
watu wanapotoka kazini na katika shughuli zao mbali mbali za mchana
kutwa, wanaitumiaje fursa yao ya faragha? Utaona wako wanaorudi
nyumbani na kujipumzisha na familia zao. Na pia wako ambao huunganisha
wakaenda katika mabaa na vilabu vya usiku mpaka usiku wa manane. Kwa
hivyo basi utagundua kwamba mtu ambaye hakuishughulisha nafsi yake na
mambo ya haki na kheri. Hapana shaka nafsi hiyo itamuendesha yeye na
kumshughulisha na mambo ya batili na upotofu. Anasema mmoja wa watu
wema: “Kufaraghika wakati (ukawa huna) shughuli (ya kufanya wakati
huo), hiyo ni neema adhimu (kubwa sana). Mja atakapoikufuru neema hii
kwa kuifungulia nafsi yake mlango wa matamanio na akavutwa nayo. Allah
atampindulia neema ya moyo wake na atampokonya usafi wa moyo aliokuwa
nao (na hapo ndipo hukosa haya/soni na akatenda lo lote bila ya kubali
(kujali)”.
Salafu wetu
wema-Allah awarehemu-walikuwa hawapendezwi mtu kuwa amefaraghika hana
la kumshughulisha si katika dini yake wala dunia yake, akawa yupo tu
hana alitendalo. Kwani hapo ndio hugeuka neema hiyo ya faragha na kuwa
nakama (adhabu/mateso/maangamivu). Ndipo pakasemwa: “Faragha kwa
wanamume ni mghafala (kujisahau) na kwa wanawake ni kiamshi/kichocheo
cha matamanio/ashki”. Ukweli wa hili unajidhihirisha katika kisa cha
Nabii Yusuf na Bi. Zuleikhah mke wa waziri kama kilivyotajwa ndani ya
Qur-ani Tukufu. Bibi Zuleikhah asingegubikwa na kufunikwa na penzi
zito la Nabii Yusuf kiasi cha kupanga vitimbi vitakavyomtia mtegoni
Nabii Yusuf. Haya yote ni natija ya faragha kubwa aliyokuwa nayo bibi
huyu katika maisha yake. Na khatari hii ya faragha ikazidi pale
ilipochanganyika na kijana mwenye uzuri uliopindukia na uwezo wa mali
unaomuwezesha mtu kupata anachokihitaji.
Yatakikana
kwa kila muislamu; mwanamume au mwanamke kuiona fursa ya faragha
aliyonayo kuwa ni neema aliyopewa na Allah. Kwani muono huu ndio
utakaompelekea kuitumia vema fursa hiyo katika mambo yenye maslahi na
manufaa naye katika ulimwengu huu wa leo na ule wa kesho. Mola wetu
Mtukufu tunamuomba atuwafikishe kuitumia vema fursa ya faragha
tunayoipata.
|