Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Dini ni nasaha, wakauliza kwa nani ? Akasema Mtume : Kwa Allah, Mtume wake, kwa viongozi wa waislamu na watu wa kawaida" Hadith Tukufu

WAKATI KATIKA MAISHA YA MUISLAMU

 

SIFA/TABIA (PROPERTIES) ZA WAKATI……..III

 

1. KUONDOKA/KUMALIZIKA HARAKA:

Hii ni sifa kuu ya wakati. Wakati unapita/unakwenda mwendo wa mawingu na unakimbia mbio za upepo. Hivi ndivyo unavyoweza kuimithilisha kasi ya mpito wa wakati bila ya kujali ni wakati wa furaha na raha au wakati wa huzuni na shida. Kimtazamo siku za furaha hupita haraka sana kuliko siku za huzuni na shida ambazo huonekana zikijikongoja taratibu sana. Hizi ni hisia na mtazamo wa mtu anayepita katika kipindi hicho kigumu, na si ukweli na hakika ya mambo ilivyo. Hakika itaendelea kubakia ilivyo kuwa wakati unapita haraka.

Umri wo wote atakaopewa mtu kuishi ulimwenguni hapa, urefuke utakavyorefuka hata ukapindukia miaka alfu, bado utakuwa ni mfupi. Ufupi huu unatokana na ukweli kuwa mauti/kifo ndio mwisho wa kila kilicho hai, katika ulimwengu huu. Allah amrehemu mshairi aliyenena: (Ikiwa kufa ndio mwisho wa umri basi ni sawasawa ufupi na urefu wa umri).

Siku mauti yatakapo muhudhuria mtu, miaka aliyoishi itajikunja na kuonekana kama ni vipindi vifupi vilivyopita kama umeta wa radi. Imepokelewa hekaya kwamba malaika wa mauti- Allah amshushie Amani – alipomjia Nabii Nuhu – Amani imshukie – ili amfishe baada ya kuishi zaidi ya miaka alfu moja. Alimuuliza akisema: Ewe mrefu wa umri kuliko Mitume wote, umeionaje dunia? Akajibu (Nuhu): Mithili ya nyumba yenye milango miwili, nimeingia (nyumbani humo) kupitia mmojawapo wa milango na kutoka kupitia mlango mwingine.

Mazingatio si usahihi wa kisa/hekaya hii bali mazingatio yako kwenye ukweli na hakika inayoelezwa na kisa chenyewe ambao ni ufupi wa umri wakati wa kufa. Anavyouona mwanadamu umri (wakati) wakati wa kufa ndivyo atavyouona wakati wa kusimama kiyama. Hivi ndivyo Allah Muumba wa wakati anavyolielezea hilo: “SIKU WATAKAPO KIOANA WATAKUWA KAMA KWAMBA HAWAKUKAA (ulimwenguni) ILA JIONI MOJA AU MCHANA WAKE (kutokana na kishindo kitakachowafika)”. (79:46)

“NA (wakumbushe) SIKU ATAKAYOWAKUSANYA (waone)KAMA KWAMBA HAWAKUKAA (akili zimewaruka hata hawajui kiasi cha wakati)….” (10:45)

 

2. KILICHOPITA KATIKA WAKATI KIMEPITA, HAKIRUDI NA WALA HAKINA BADALI.

 

Hii ni sifa na tabia nyingine ya wakati kwamba kila siku iliyopita, saa iliyomalizika na kila kipindi kinachopita ni muhali kujirudia tena kama ambavyo ni muhali kupata badala yake. Hii ndio maana na muradi wa kauli ya Sheykh Al-Hassan Al-Biswriy- Allah amrehemu: “Hapana siku yo yote inayochomoza alfajiri yake ila hulingana (hunadi) siku hiyo (na kusema): Ewe mwanadamu wee! Mimi ni kiumbe mpya, na ni shahidi juu ya amali zako (za leo, mbaya na njema). Basi jichukulie masurufu (ya akhera) kwangu kwani mimi nikiondoka sirudi tena mpaka siku ya Kiyama.”

Huu ndio ukweli usiopingika kuhusiana na wakati. Baada ya kutunga mimba, mwanadamu hukua kadri siku (wakati) zinavyopita kutoka hali moja kwenda nyingine, mpaka akawa kiumbe kamili akazaliwa. Baada ya kuzaliwa na kuanza kuvuta hewa ya ulimwengu huu akiwa katika kipindi cha uchanga. Kuja na kuondoka kwa siku (wakati) humchukua kutoka katika kipindi hiki cha uchanga na kumfikisha katika kipindi cha utoto. Kisha kutoka utotoni hadi ujanani, safari hii ya ujana humfikisha katika kituo cha utu-uzima. Kutokea hapo mpaka uzeeni na ukogweni, halafu hapo ndipo siku (wakati) huikhitimishia safari yake hii kaburini. Kwa mlolongo huu ni muhali kwa mzee kutamani kurudi ujanani na akaweza kuurufia ujana. Umuhali huu unatokna na ukweli kwamba siku (wakati) za ujana zimekwishakwenda na kupita na kwa tabia ya wakati, haziwezi kurudi tena. Kwa mantiki utafahamikiwa kuwa wakati una sifa na kanuni ya mbele kwa mbele, yaani kuja na kuondoka haraka bila ya kurudi tena. Sifa hii ya wakati inakhalifiana na maumbile ya mwanadamu ya kutamani kurudia yaliyopita. Kuhusiana na maumbile haya ya mwanadamu, tunasoma: “HATA YANAPOMFIKIA MMOJA WAO MAUTI, HUSEMA MOLA WANGU! NIRUDISHE (Ulimwenguni) ILI NIFANYE MEMA SASA BADALA YA YALE NILIYOYAACHA….” (23: 99-100)

Ukweli huu pia unadhihirishwa na kauli ya mshahiri:-

Ee laiti ujana ungerudi siku moja, Nikapata kuueleza yaliyofanywa na uzee.

 

3. WAKATI NDIO KITU CHA THAMANI KULIKO VYOTE ANAVYOVIMILIKI MWANADAMU (WAKATI NDIO RASILIMALI KUU YA MWANADAMU).

Kwa kuwa imekuwa ni tabia ya wakati kuondoka haraka na kwamba kilichopita katika wakati ndio kimepita, hakirudi na wala hakina badali. Kwa tabia na sifa hii ya wakati, inaufanya wakati kuwa ndio kitu ghali na cha thamani kuliko vyote vinavyomilikiwa na mwanadamu. Ughali na thamani hii ya wakati unatokana na ukweli kwamba wakati ndio chombo na mahala pa kazi na uzalishaji wote uanompatia milki mwanadamu. Kwa mantiki hii sote tutakubaliana kwamba wakati ndio rasilimali ya kweli ya mtu/jamii. Rasilimali hii haimilikiwi na mwanadamu na wala haimfuati mwanadamu anavyotaka. Bali mwanadamu ndio analazimika kuifuata na kuichunga ili aweze kuchuma na kumiliki kupitia rasilimali hii kuu. Kwa hivyo thamani ya wakati haiwezi kumithilishwa na dhahabu wala jiwe lo lote la thamani ulijualo, kwa sababu wakati ndio uhai/umri wa mtu. Hivi ndivyo alivyouona wakati Hassan Al-Bana – Allah amrehemu: “Huo (wakati) ndio uhai (wenyewe)! Haukuwa uhai wa mwanadamu ila ni ule wakati ambao anaoupitisha tangu saa ya kuzaliwa mpaka ya kufa.”

Kauli hii ya Hassan Al-Banaa inashabihiana na ile ya Al-Hassan Al-Biswriy- Allah awarehemu wote: “Ewe mwanadamu wee! Hakika wewe si chochote ila ni siku zilizojumuishwa pamoja, kila inapokwenda zake siku moja huwa imeondoka baadhi yako.”

Mtu asiyeiona thamani ya wakati leo, hapana shaka kuwa ataiona na kuijua thamani hiyo kesho wakati ambapo tayari wakati huo utakuwa umepita na hautarudi tena. Kuhusiana na hili la kutokuiona thamani ya wakati ila bada ya kupita. Kisha tena ndipo mwanadamu ajute majuto yasiyomfalia kitu ila uchungu. Qur-ani inatukumbusha sehemu mbili ambazo mwanadamu ataujutia wakati alioupoteza

WAKATI WA KUTOKA ROHO:

Wakati mwanadamu anapoipa mgongo dunia bila ya khiyari yake na

kuikabili akhera, atatamani apewe muda kidogo tu. Ajali (mauti) yake iakhirishwe kidogo ili apate fursa ya kutengeneza aliyoyaharibu na kuyadiriki yaliyomfutu/yaliyompita. Tuitegee sikio Qur-ani tukufu: “ENYI MLIOAMINI! YASIKUSAHAULISHENI MALI YENU WALA WATOTO WENU KUMKUMBUKA ALLAH, NA WAFANYAO HAYO, HAO NDIO WENYE KUKHASIRIKA. NA TOENI KATIKA YALE TULIYOKUPENI, KABLA MMOJA WENU HAYAJAMTIA MAUTI, KISHA AKASEMA: MOLA WANGU! HUNIAKHIRISHI MUDA KIDOGO (tu) NIKATOA SADAKA NA NIKAWA MIONGONI MWA WATENDA MEMA?” (63: 9-10)

Na jawabu la matamanio haya matupu litakuwa ni la kukatisha tamaa kabisa kuonyesha kuwa kilichopita kimepita na wala hakidirikiwi: “LAKINI ALLAH HATAIAKHIRISHA NAFSI YOYOTE INAPOKUJA AJALI YAKE NA ALLAH ANAZO KHABARI ZA MNAYOYATENDA (yote).” (63:11)

AKHERA:

Hapa ndipo mahala ambapo kila nafsi italipwa kwa ukamilifu kila iliyochuma na kisha watu wa peponi waingie pepini na wale wa motoni waingie motoni. Hapo ndipo watakapotamani watu wa motoni kurudi kwa mara nyingine tena katika maisha haya ya majukumu (taklifu). Warudi duniani ili waanze upya kutenda amali njema zitakazowanufaisha akhera. Haiyawi, hayawi ng’o hayo wayatakayo, kwani kipindi cha kufanya amali tayari kimepita na sasa ni wakati wa kipindi cha jazaa/malipo ya amali zilizotendwa katika kipindi kilichomalizika. Kuhusiana na hili Qur-ani Tukufu inatuambia: “NA WALE WALIOKUFURU WATAKUWA NA MOTO WA JAHANAMU, HAWATAHUKUMIWA KUFA, WALA HAWATAPUNGUZIWA ADHABU YAKE HIVI NDIVYO TUNAVYOMLIPA KILA ASIYE NA SHUKRANI. NAO HUMO WATAPIGA MAKELELE (watalia wanasema): MOLA WETU! TUTOE (motoni uturejeze duniani) TUTAFANYA VITENDO VIZURI VISIVYOKUWA VILE TULIVYOKUWA TUKIFANYA (Allah awaambie) HATUKUKUPENI UMRI WA (kuweza) KUKUMBUKA MWENYE KUKUMBUKA? NA AKAKUJIENI MUONYAJI, BASI ONJENI (adhabu) MADHALIMU HAWANA WA KUWANUSURU.” (35: 36-37)

Hoja yao hiyo ya kutaka kurudisha nyuma kilichopita mbali ya kuwa inapingana na kanuni ya wakati itakatiliwa mbali na swali kemeo/karipio: “HATUKUKUPENI UMRI WA (kuweza) KUKUMBUKA MWENYE KUKUMBUKA NA AKAKUJIENI MUONYAJI?……”

Hawatapata jawabu ya swali hili, kwa sababu Allah tayari alishaukata mzizi mkuu wa mti wa udhuru pale alipompa kila mwenye dhima (mukalafu) umri (wakati) unaotosha kutenda kila alilokalifishwa nalo. Na akamuwekea ada ya kumkumbusha kila anapoghafilika na kujisahau khasa kwa mtu aliyebahatika kuishi miaka sitini. Umri huu unatosha kabisa kumzindua aliyeghafilika na kumpa fursa ya kutubu. Hili ndilo eleweko la kauli ya Bwana Mtume – Rehema na Amani zimshukie – “Allah amemuondoshea udhuru mtu aliyemngojea (asimfishe) mpaka akafikia umri wa miaka sitini.”

Bukhaariy



Forum | Guestbook | Tuandikie |