|
Allah mola mtukufu
ametukuza na kumfadhilisha mwanadamu kuliko viumbe vingine
alivyoumba:"NA HAKIKA TUMEWATUKUZA WANADAMU NA TUMEWAPA VYA KUPANDA
BARANI NA BAHARINI, NA TUMEWARUZUKU VITU VIZURI NA TUMEWAFANYA BORA KULIKO
WENGI KATIKA WALE TILIOWAUMBA KWA UTUKUFU ULIO MKUBWA (kabisa)"
(17:70)
Tena Allah amemuhalalishia mwanadamu huyu
vyote vilivyo vizuri vizuri na venye manufaa kwake na akamuharamishia
vyote vilivyo vibaya vibaya na vyenye madhara kwake. Na akampa mwanadamu
mwanaume mke wa jinsi yake, yaani mwanadamu mwenzie na akamruzuku kutokana
na mke huyu kizazi (watoto):"NA ALLAH AMEKUUMBIENI WAKE KATIKA JINSI
YENU, NA AKAKUJALIENI KUTOKA KWA WAKE ZENU WATOTO NA WAJUKUU, NA
AKAKURUZUKUNI VITU VIZURI. BASI JE, WANAAMINI YASIYOKUWA YA HAKI NA
KUZIKATAA NEEMA ZA ALLAH ?" (16:72)
hii ndiyo suna (kawaida/dasturi) ya Allah
mola mwenye hekima aliyoiweka katika umbile la mwanadamu. kuiheshimu
kawaida hii ya kimaumbile, bila ya kuichezea kwa kuizuia kutekeleza jukumu
iliyoumbiwa ni kuiheshimu haki ya Allah mola mmiliki wa ulimwengu na vyote
vilivyomo ni pamoja na viungo vyako vya uzazi "HIYO NDIYO KAWAIDA (suna)
YA ALLAH ILIYOTANGULIA ZAMANI; WALA HUTAPATA MABADILIKO KATIKA KAWAIDA YA
ALLAH" (48:23)
Hebu sasa tujaribu kuangalia neno "TA’AQIYM"-
(sterilization). "ta'aqiym" hali ni neno la kiarabu lenya
kumaanisha tendo cha kufanya mwanamke au mwanamume kuwa tasa. Kitendo hiki
kina lengo la kumfanya muhusika (mwanamume/mwanammke) asiweze kuzaa ili
kupunguza ongezeko la kasi ya idadi ya watu kama wanavyodai waasisi wa
mpango huu. Tendo hili la kumtia mtu utasa ambao hakuumbwa nao hutekelezwa
kwa kutumia njia mbali mbali (vasectomies) miongoni mwa njia zilizokuwa
zikitumika zamani ni kuvunja na kupasua pumbu (testicles) za mwanamume
sawa na ifanyikavyo kwa ngo'mbe (maksai) leo hutumika njia kwa kukata
nrija unaosafisha mbegu za uzazi (manii) kadhalika hutumika njia za kumeza
dawa au kudunga sindano ambayo huwa au kudhoofisha nguvu za vihayawani vya
manii (spermatozoon) ama kwa upande wa mwanamke hufungwa mfereji wa mayai
(fallopian tube) ili usiweze kusafisha na kuyapeleka mayai pahala ambapo
yatarutubisha na kukuzwa kutokana na kukutana na mbegu za mwanamume.
Kadhalika hutumika pia njia ya kuling'olea mbali fuko la uzazi
(hysterectomy). Wakati mwingine hutumika njia ya kumeza vidonge kadunga
sindano na kadhalika. Kumtia utasa mwanamume ni kitendo haramu kwa mtazamo
wa uislamu, uharamu huu unatokana na kuzuia kazi yake maalumu (function)
aliyoumbiwa na kumfanya ashabiane na mwanmke katika baadhi ya tabia
(properties) zake. na tendo hili linapingana na hekima (wisdom) ya Allah
katika kuumba jozi mbili; ya kiume na ya kike:"ENYI WATU! MCHENI MOLA
WENU AMBAYE AMEKUUMBENI KATIKA NAFSI (asili) MOJA. NA AKAMUUMBA MKWE
KATIKA NAFSI ILE ILE. NA AKAENEZA WANAUME WENGI NA WANAWAKE KUTOKA KATIKA
WAWILI HAO.....". (4:1)
Hali kadhalika utaona kuwa ni haramu
kumfanya tasa mwanamke kwa hekima hii. Utasa ni haramu kwa sababu
unamaanisha kukata sababu ya kuzaliana, kuongezeka na kujaza ulimwengu
kama alivyokusudia Allah mola muumba wa ulimwengu. Ni kutokana na sababu
hii na nyinginezo ndio tinamuona Bwana Mtume rehema na amani zimshukie
akilikemea na kuharamisha tendo hili la kujitia utasa.
Imepokelewa katika sahihi al Bukhariy
kwamba Abu Hurayrah Allah amuwie radhi alimuomba Mtume rehma na amani
zimshukie ruhusa ya kujihasi (awe tasa) kwa sababu ya kukosa gharama za
kuolea naye (Abu Hurayrah) alikuwa kijana anachelea kutumbukia katika
zinaa. Mtume akampa mgongo bila ya kumjibu mpaka (Abu Hurayrah) akayakiri
maneno yake haya mara tatu, ndipo akamuambia:" ewe Abu Hurayrah
kalamu imekwisha kauka kwa hayo yanayokukuta, basi ishi mpweke (bachelor)
au acha (kuishi mpweke, yani oa)".
Imekuja katika riwaya nyingi zilizopokewa
na Imam Ahmad kwamba baadhi ya masahaba walimuomba Bwana Mtume awape
idhini ya kujihasi, akawakataza na kawambia: kujihasi kwa umati wangu ni
kwa kufunga na kusimama usiku(kuswali). Imam Nawawiy pia ametaja katika
sherehe ya Muslim (juzuu ya 9 sahifa77) kwamba kujihasi ni haramu kwa
mwanadamu awe ni mkubwa au mtoto.
kwa hiyo basi suala la mtu kujifanya tasa,
awe ni mwanamume au mwnamke ni haramu kisheria ikiwa anakusudia kuondosha
uzazi moja kwa moja. Hii ni kwa sababu tendo hili linatishia kumaliza
uzazi cha jamii ya mwanadamu ambacho ndicho lengo kluu la ndoa na kuumba
kwa jinsi ya kike au kiume.
Ama ikiwa utasa huo ni wa muda maalum, kwa
sababu maalumu inayokubalika kisheria. Tunakusudia kwa neno "utasa wa
muda" kuzuia uzazi kwa kipindi fulani bila ya kuuathiri mfumo mzima
wa uzazi yaani mtu anabakia na uwezo wake wa kuzaa pindi akitaka kufanya
hivyo. Aina hii ya utasa inajuzu kisheria ikiwa iko sababu inayohitajika
kifanya hivyo inazingatia/inakubalika katika msingi wa sheria. Udhuru/sababu
hiyo inaweza kuwa kama ni kuondoa/kuzuia madhara yanayoweza kuhatarisha
maisha ya muhusika iwapo atashika mimba. Au utasa huu wa muda utakusudiwa
kuwa ni njia ya kutoa nafsi baina ya mimba na mimba ila kumpa mama fursa
ya kuinyonyesha na kuijenga upya afya ya mama na mtoto.
Amenukuu Imam Bujayramiy kwamba ni haramu
kutumia kitu/njia inayoweza kuzuia mimba kabisa (milele) ama njia
inayochelewesha tu, ujauzito kwa muda fulani bila ya kuathiri uwezo wa mtu
kuzaa si haramu. Na isitoshe ikawa ni udhuru/sababu inayozingatia kama
vile ulezi wa mtoto si haramu na kama ikiwa bila ya udhuru, inakuwa ni
haramu. (Hashiyatul-Khatwib, juzuu 4 sahifa 40)
|