Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Dini ni nasaha, wakauliza kwa nani ? Akasema Mtume : Kwa Allah, Mtume wake, kwa viongozi wa waislamu na watu wa kawaida" Hadith Tukufu

MTIZAMO WA UISLAMU KATIKA SUALA LA UTOAJI WA MIMBA (ABORTION).

Faida

Utoaji mimba ni kitendo cha kuikatisha bila ya ridha wala khiyari yake safari ya mwanadamu mtarajiwa kuja katika ulimwengu huu kuishi kama alivyotaka  mola wake. Kitendo hiki humfanya katika kituo cha mwanzo cha safari hii, ambacho ni tumbo la mama, na huweza kufanya kabla ya mwanadamu huyu kuviviziwa/kupuliziwa roho yaani kabla ya mimba kutimiza umri wa miezi minne na kuendelea.

Kuhusiana na swala la umri wa kuviviziwa roho, huyu hapa mwanasayansi mahiri, Mtume wa Allah Rehema na Amani zimshukie-anatuambia: "Hakika  mmoja wenu hukusanywa umbo/umbile lake tumboni mwa mama yake hali ya kuwa ni tone la manii kwa muda wa siku 40.kisha huwa pande la damu kwa mfano wa muda huo (yaani siku 40) kisha huwa pande la nyama kwa mfano wa muda huo, kisha (hapo ndipo) hupelekewa malaika akamviviza roho (katika umri huo wa siku 120 ambazo ni sawa na miezi minne).........Bukhariy na Muslim.

Utoaji wa mimba ni swala lililoenea ulimwenguni kote hivi sasa na kujaribu kukemewa na taasisi na madhehebu mbalimbali za kidini na hata baadhi ya wanasiasa. hili ni suala ambalo linashughulisha akili ya wanawake wengi wajawazito. hasa pale wanapojikuta njia pande, ama waendelee kubeba mimba mpaka kujifungua au waitoe. Kwa kuwa tunaamini kuwa uislamu ni dini na mfumo wa maisha unaokwenda sambamba na maumbile ya mwanadamu : "BASI UELEKEZE USO WAKO KATIKA DINI ILIYO SAWASAWA, NDILO UMBILE LA ALLAH ALILOWAUMBIA WATU (yaani hii dini ya kiislamu inafikiana barabara na umbo la binadamu). HAKUNA MABADILIKO KATIKA MAUMBILE YA VIUMBE VYA ALLAH. HIYO NDIYO DINI ILIYO HAKI, LAKINI WATU WENGI HAWAJUII". (30:30)

Ni nini mtazamo wa dini hii ya maumbile kuhusiana na suala zima la utoaji wa mimba?

Uislamu kama dini au mfumo sahihi wa maisha unalitazama swala hili kwa mitazamo miwili tofauti. uislamu unaliangalia suala la  utoaji wa mimba :

1) Baada ya kiumbe kuviviziwa roho  na

2) Kabla ya kiumbe kuviviziwa roho

Mitazamo hii miwili iliyosimama kwa kigezo cha kuviviziwa ama kutokuviviziwa roho iniatufikisha katika hukumu mbili tofauti kama zifuatavyo:- 

 

1)  HUUMU ZA KUTOA MIMBA BAADA YA KIUMBE KUVIVIZIWA\KUPULIZWA ROHO:

Uislamu unakitizama kitendo cha kutoa mimba baada ya mimba kufikishwa umri wa kuviviziwa roho, yaani miezi minne kama tulivyo kwishwa bainisha kuwa ni kitendo cha haramu na ni jarima (crime/offence). Kwa mtazamo huu sii halali kwa muislamu yoyote kushiriki ama kukifanya kitendo hiki dhalimu kinachomnyima mwanadamu na mtarajiwa haki ya kuishi na kufurahia maisha. Hili ni  kosa la jinai dhidi ya kiumbe hai aliyekamilika inalompelekea mtendaji wake diyah (Indemnity) ikiwa mimba itatoka na kiumbe akawa hai au adhabu nyingine inayohusika mali chini ya kiwango cha  diyah ikiwa mimba itatoka na kiumbe akawa tayari ashakufa tangu tumboni. Utoaji mimba katika hali na mazingira haya utakua ni kosa la jinai hata kama utafanywa na mama wa mwanamimba huyo au baba yake. Wote hawa watakuwa na hatia mbele ya sheria na watastahiki kuadhibiwa kwa mujibu wa sheria.

Ama akithibiti kutokana na kauli ya matatibu bingwa katika fanii hii ya uzazi kutokana na uzoefu, elimu na utafiti wao kwamba mama kuendelea kubeba husika katika kipindi hiki ni kuhatarisha maisha yake.

Hali ilivyo inaonyesha lazima tu mama atakufa aidha katika kipindi hiki cha ujazito, au wakati wa kujifungua au mara tu baada ya kujifungua kutokana na sababu mbalimbali.

Katika hali na mazingira kama haya uislamu unatoa nafasi itumike kanuni ya kuiondosha lenye madhara kidogo kati ya mambo mawili yenye madhara. Itaangalia ikiwa matabibu watasema kuwa kuendelea kuishi kwa mimba hiyo hakumaanishi kingine zaidi ya kifo kwa mama mjazito na ikawa hakuna njia nyingine ya kuyaokowa maisha yake ila ni kuitoa mimba hiyo. Utoaji mimba katika hali hii na mazingira haya utakua ni jambo la lazima lisiloepukika. Kufa mama ni madhara na hali kadhalika kufa mwanamimba pia ni madhara . Lakini madhara haya ya kufa mwanamimba si makubwa sana ukilinganisha na madhara ya kufa mama. Kwa mantiki hii mama huyu hatokuwa muhanga kwa sababu ya kutoa maisha tya mwanamimba, kwani mama ndiye asili na shina halingolewi kwa sababu ya tawi. Mama huyu tayari ana sehemu ya wajibu ya kuitekeleza katika maisha haya, ambayo mwanamimba huyu hana, na isistoshe yeye mama ndiyo msingi na nguzo kuu ya familia.

Ni jambo lisiloingia akilini kuutoa muhanga uhai wake kwa ajili ya huyu mwanamimba ambaye uhai ake haujathibiti bado; atazaliwa hai au atafia tumboni:".... MAMA ASITIWE TAABUNI KWA AJILI YA MTOTO WAKE ....(2:233)

 

2. HUKUMU YA KUTOA MIMBA KABLA YA KIUMBE KUVIVIZIWA ROHO.

Utoaji mimba kabla ya mimba hajatimiza umri wa siku 120- yaani miezi minne ambayo ndio umri wa kuviviziwa roho kiumbe. Ni halali kuitoa mimba iliyo chini ya miezi minne kama kuna haja/sababu ya kupelekea kufanya hivyo. Na kama hakuna haja ipelekeayo kutoa, basi itakua haramu kisheria kuitoa kauli jumla, wanazuoni wa fiqhi wamekongamana na kuwafikiana kwamba utoaji mimba ni kitendo haramu kisichokubalika katika umri wowote wa mimba/uajzito ila kwa dharura iliyithibitisha na matabibu bingwa wa masuala ya uzazi.

 

NYONGEZA/FAIDA:

JE, AIBU/KASORO (Defect/Blemish) YA JANINI/MWANAMIMBA (Embroy/Foetus) NI UDHURU (Excuse) UNAOHALALISHA KUTOA MIMBA?

Ni jambo lililo wazi kwa kila mmoja wetu kwamba baadhi ya mimba huwa na mapungufu ya kimaumbile (ulemavu-deformities). Kutokana na hatua ya maendeleo iliyofikia katika elimu ya sayansi na teknologia. Mapungufu/ulemavu huu huweza kuonekana kupitia vyombo vya kisasa na il-hali mtoto angali tumboni. Pia utaalamu huu huweza kuonyesha uwezekano wa mtoto mtarajiwa kurithi aibu/ulemavu au maradhi aliyo nayo baba au mama yake. Na suala la mtoto kurithi tabia, maumbile au maradhi kutoka kwa mmaja wa wazazi wake ni suala linalozingatia na sheria, yaani uislamu unalikubali sasa tujiulize:-

 

  • Je inajuzu kutoa mimba pindipo itakapokundulika mapungufu/aibu/ulemavu mabaya utakaomfanya mtoto mtarajiwa kushindwa kuishi maisha ya kawaida?
  • Je inajuzu kuitoa mimba hayo hata kama anaweza kuishi maisha ya kawaida baada ya kuzaliwa pamoja na ulemavu/mapungufu hayo?

        

Inabainika kutokana na kauli za mafaqihi kwamba mimba ikishakaa katika fuko/tumbo la uzazi kwa muda wa siku 120 au miezi minne. Imethibiti kwa ushahidi wa Quran na sunnah kuviviziwa roho kwa kiumbe hicho katika kipindi hicho. Kutokana  na kuviviziwa roho huku, kiumbe huyu anatambulika na sheria kuwa ni mwanadanmu mwenye kustahiki kapata haki zote za kimsingi kama wanadamu wengine. Ni kwa sababu ya kuzotambua na kuzikubali haki za mtoto huyu aliye tumboni ndio sheria ikajuzisha kumuekea wasiyah (Bequests), waqfu (Endowment) na kustahiki kurithi (Inheritance). Kwa mantiki hii, mwanamimba huyu anazingatia kisheria kuwa ni miongoni mwa nafsi ambazo Allah ameharamisha kuuliwa ila kwa haki :...." WALA MSIMUUE MTU AMBAYE ALLAH AMEHARAMISHA (kuuawa) ILA IKIWA (Imetokea) HAKI(ya kuuawa)...."(6:151)

 Kwa hali hii ni haramu kuitoa mimba hiyo ila kama sababu ya msingi inayohitajisha jambo hilo. Hata ulemavu/mapungufu ya kimwili yawe yatakavyokua hayawezi kuwa ni sababu ya msingi ya kuhalalisha tendo hili ovu. Hii ni kutokana na kuwa maendeleo ya elimu ya tiba yameonyesha kwamba baadhi ya maradhi/ulelemavu huwa hautibiki kwa kipindi fulani na baadae ukapatikana ufumbuzi wake yakatibika.Utakasifu ni milki yake Allah ambae aliyefundisha mwanadamu chungu ya mambo aliyokua hayajui

NANYI HAMKUOEWA KATIKA ILIMU (ujuzi) ILA KIDOGO KABISA (17:85)

Kwa hivyo suala la kusema kuwa mimba hii ikizaliwa mtoto huyu atashindwa kiishi maisha ya kawaida, kwa sababu hii ni bora kuitoa mimba , halikubaliki.

Ama ikiwa kasoro/mapungufu haya ni ya kurithi kutoka kwa mmoja wa wazazi, inamkiniki kuyazuia yasienee kwa kizazi chao kwa kuizuia mimba kwa muda. Na jambo hili linajuzu kama dawa/tiba ambayo imeamrisha na sheria. Kama haikumkinika kuzuia mimba baina ya mke na mume ambao imedhihirika kuwa wote wawili au mmoja wao ana maradhi hatari ya kuambukiza ambayo mtoto hawezi kusalimika nayo kama vile ukimwi (AIDS) na ikathibiti kwa vipimo kwamba mtoto ameathirika na hatoweza kuishi, inajuzu kisheria kuitoa mimba hii mida wa kuwa hajatimiza umri wa siku 120 yaani miezi minee tumboni.

Ama wanamimba ambao wana kasoro/mapungufu ambayo inamkinika kutibika tumboni kwa dawa atakazotumia mama yake au kwa njia ya operesheni (upasuaji) baada ya kuzaliwa. Na wale wenye ulemavu ambao haiwazuilii kuishi maisha ya kawaida. hata zote hizi hazizingatii na sheria kuwa ni udhuru unaohalalisha kutolewa kwa mimba hizo. Kipimo kinachozingatia katika kujuzisha utoaji wa mimba hizi ni kuthibiti kielimu kwa hatari ya kasoro/mapungufu hayo na kwamba hayana tiba. Ama kasoro za kimaumbile kama vile, upungufu wa mkono au mguu mmoja, hizi hazizingatiwi kuwa ni mapungufu (udhuru) unaohalalisha utoaji wa mimba husika.Kwani maendeleo ya kielimu yameonyesha uwezekano wa mtu kuwekewa viungo bandia na vikafanya kazi bila ya tofauti kubwa na viungo halisi.

Haya ndiyo tunayoweza kuyaelezea kuhusiana na suala zima la utoaji wa mimba.

 

USHAURI WA BURE:

Ewe daktari muisalmu wee, unayeshughulika na utoaji mimba. Elewa sheria haikuruhusu kufanya kitendo hiki kiovu ila kwa dharura ambazo tumezibainisha humu. Kinyume na hivi utakua umejitumbukiza katika hatia na midhambi ya kuwa nafsi ambayo Allah kaharamisha kuuliwa. Tena usifikie uamuzi wa haraka kabla ya kuthibitisha na vipimo na kashauriana na jopo la madaktari wenzio.

 


TUJIFUNZE NA TUKUBALI:"......YA KWAMBA ATAKAYEMUUA MTU BILA YA YEYE KUUA MTU AU BILA YA KUFANYA FISADI KATIKA NCHI BASI NI KAMA AMEWAUWA WATU WOTE......." QURAN: (5:32)

 


Forum | Guestbook | Tuandikie |