Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Nasaha za Dini  

"Dini ni nasaha, wakauliza kwa nani ? Akasema Mtume : Kwa Allah, Mtume wake, kwa viongozi wa waislamu na watu wa kawaida" Hadith Tukufu

NJIA ZA KUFUATA ILI KUWEZA KUPATA WINGI WENYE NGUVU AMBALO NDILO SHABAHA YA UISLAMU.

 

Njia pekee ya kutuwezesha kulifikia lengo hili ni kuwa na mpango wa familia. Mipango huu utakuwa na dhima ya kuilinda nguvu na uwezo wa familia katika kusimamia na kutekeleza wajibu wake. Kwa janibu (upande) wa kizazi kinachopatikana, dhima ya mpango huu itakuwa ni kuzalisha kizazi chenye afya njema kitakachopata haki zake zote za malezi. Ama kwa upande wa jamii, mpango huu utakuwa na dhama ya kuhakikisha ustawi wa ukuaji wake na kujitegemea kwa mahitaji yake. Kwa kuzingatia kanuni na misingi ya sheria, lengo la mpango huu lifikiwe kupita njia zifuatazo:-

1.      Kuzuia kushika mimba kwa muda ili kumpa fursa mama kumnyonyesha mwanawe kwa kipindi kamili. Qur-ani tukufu imeufanya muda wa kunyonyesha kuwa ni miaka miwili kamili, tusome:- “NA WANAWAKE WALIOZAA WAWANYONYESHE WATOTO WAO MIAKA MIWILI KAMILI, KWA ANAYETAKA KUKAMILISHA KUNYONYESHA; NA NI JUU YA BABA (yake) CHAKULA CHAO (hao watoto na mama) NA NGUO ZAO KWA SHARIA WALA HAIKALIFISHWI NAFSI YOYOTE ILA KWA KADRI YA WASAA WAKE. MAMA ASITIWE TAABUNI KWA AJILI YA MTOTO WAKE, WALA BABA (asitiwe taabuni) KWA AJILI YA MTOTO WAKE NA JUU YA MRITHI (inapokuwa baba kafa) NI KAMA HIVYO - - - “ [2 : 233]

Katika aya hii tukufu kuna mambo kadhaa muhimu ya kuzingatia, miongoni mwake ni kama ifuatavyo:-

i.       Muda timilifu wa kunyonyesha.

Aya inataja muda timilifu wa kumnyonyesha mtoto kuwa ni miaka miwili kamili. Huu ndio muda uliowekwa na sheria wa kumnyonyesha mtoto kwa kuizingatia afya yake na ya mama yake. Muda huu wa kumnyonyesha ukichanganywa pamoja na ule muda ujauzito mpaka kujifungua, utakuta takriban kuna kipindi cha miaka mitatu baina ya mimba na mimba nyingine. Hiki ni kipindi kinachotosha kumfanya mtoto awe na siha njema na kukua vizuri.

ii.     Kutoikalifisha nafsi kuliko uweza (wasaa) wake.

“MWENYE WASAA AGHARIMU KADIRI YA WASAA WAKE; NA YULE AMBAYE AMEPUNGUKIWA RIZIKI YAKE, ATOE KATIKA KILE ALICHOPEWA NA ALLAH, ALLAH HAMKALIFISHI MTU YE YOTE ILA KWA KADIRI YA ALICHOMPA ---.” [65 : 7]

Aya hii inaashiria upande wa uchumi na umuhimu wake katika uwanja wa familia, kwani ni upande huu wa uchumi ndio unaoipa familia uwezo wa kuihudumia familia.

iii.  Taathira ya mimba, unyonyeshaji na malezi kwa afya ya mama.

Kipindi cha ujauzito ni kipindi amacho mama hupitia katika hali ngumu sana kimaumbile na kiakili (mawazo) “NA TUMEMUUSIA MWANAADAMU AFANYE WEMA KWA WAZAZI WAKE MAMA YAKE AMECHUKUA MIMBA YAKE KWA TAABU NA KAMZAA KWA TAABU – NA KUBEBA MIMBA YAKE HATA KUMWACHISHA ZIWA (uchache wake) NI MIEZI THELATHINI.” (46: 15).

Lishe ya mama, kinga dhidi ya maradhi hulazimika kushirikiana na mwanawe (mimba), unyonyeshaji na suala zima la ulezi huiathiri kwa kiasi kikubwa afya ya mama kimwili, kiakili na kitabia. Kwa mantiki hii mama anahitaji kupewa fursa ya kutosha kuweza kuijenga upya afya  yake, hivyo ndivyo inavyoashiriwa na aya: ……..MAMA ASITIWE TAABUNI KWA AJILI YA MTOTO WAKE………..”

2.      Kufunga uzazi kabisa.

Iwapo mke na mume, wote wawili au mmoja wao ana gonjwa sugu la kuambukiza. Gonjwa ambalo mtoto atakayezaliwa hatasalimika nalo, ni lazima tu litamkumba. Katika hali kama hii ni vema kwa wanandoa hawa wakakubaliana kufunga uzazi kabisa ili kumuepusha mtoto atakayezaliwa na maambukizo yatakayowagharimu wao na kumnyima furaha mtoto. Kwa ufafanuzi wa kina kuhusiana na mas-ala haya  unaweza kurejea kitabu (NIHAYATUL – MUHTAAJ) Juzuu ya nane (8) ukurasa 240, cha Imam Ramliy.

Njia mbili hizi ndizo tiba ya mpango wa uzazi inayomkinga na kumuepusha mtoto na udhaifu unaoweza kumpata kutokana na kunyonyeshwa katika kipindi cha ujauzito. Pia ndio kinga  ya maradhi ya kuambukiza kama ukimwi, ukoma (Leprosy) na kifua kikuu (tuberculosis) ambayo anaweza kuambukizwa na wazazi wake. Kadhalika hizi ndizo njia salama zitakazomuepusha mama na udhaifu wa mwili kutokana na kushika mimba zito baada ya mwimba bila ya kupata muda wa kutosha kupumzika na kujenga afya yake.

3.      Uwezo wa familia.

Uwezo wa familia katika kuwakimu na kuwahudumia watoto wao na kuwalea ni kigezo kingine kinachoweza kuhalalisha mpango wa uzazi ikiwa familia itachelea kujitia hatiani kwa kushindwa kuwapa watoto wao watakaowazaa haki yao ya  malezi na hivyo kusababisha kuharibika kwa maisha ya watoto  hao baadaye. Baasi ni bora na inajuzu kwa familia hiyo kujihusisha na mpango nwa uzazi kwa kutumia njia zinazokubalika kisheria. Uislam hauzui mpango huu wa uzazi bali unauhimiza kwa ajili tu ya kuondosha madhara yanayoweza kumpata mtu katika maisha yake. Ruhusa hii iantokana na kanuni ya Uislamu isemayo.” Madhara huondoshwa/huzuiwa kwa kiasi imkinikavyo”……………………..

TANBIHI:         Uislamu haukuruhusu kufunga/kuzuia uzazi kwa kile kinachoitwa – Mripuko/ongezeko la watu duniani. Naam, wachumi wanasema kuna ongezeko kubwa la watu duniani, ukilinganisha na ukuaji wa uchumi wa dunia. Ni kweli, kutokana na sensa zinazofanywa kwa kuzingatia idadi ya watoto watakaozaliwa baada ya miaka kadhaa. Lakini sensa na tafiti hizi hazikukadiria eneo la ardhi litakalokaliwa na idadi hiyo na chakula kitakachokidhi haja yake!. Tumefanya juhudi zipi za makusudi za kiuchumi na kijamii sisi tuliokadiria idadi hiyo ya watu katika kukabiliana na ongezeko hilo? Unaposema tupunguze idadi ya watu tu bila ya kusema tukuze uchumi maradufu ili kukabiliana na idadi hiyo, utakuwa na mtazamo hasi mtazamo dhaifu/lemavu. Uislamu unakutaka uwe na mtazamo chanya/mtazamo hai utuambie mathalan, kufikia mwaka 2010 idadi ya watu itakuwa imeongezeka kwa asilimia kumi (10%) ongezeko hili litahitaji eneo la ardhi za mita mraba kadhaa, chakula tani kadhaa na huduma za kijamii (shule, hospitali) kiasi kadhaa. Kisha uhimize kufanyakazi ili kufikia makadirio hayo ili kulingana na ongezeko  kadirio hilo. Ni lazima tuwe na mitazamo yote miwili, hasi na chanya ili tuwe na mizani na kusimama sawa bila ya kuyumba huku au kule. Kwa nini tukimbilie dhana ya upunguzaji wa watu na hatuikimbilii dhana ya kuongeza uzalishaji na kuboresha huduma za kijamii?? Kwa kuikimbilia dhana hii hasi ya upunguzaji idadi ya watu kwa kuzuia mimba, utakuwa umeelekea upande kiasi ambao unakusaidia kuwa mvivu na kuridhika na hatua ya maendeleo uliyofikia. Kwa nini tusiikimbilie dhana chanya ya uongezaji wa uzalishaji, dhana ambayo itatusukuma kuongeza nguvu kazi za makusudi ili kukuza hali ya uchumi? Tuukiri kukweli huu:”……NA AKABARIKIA HUMO NA AKAKADIRIA HUMO CHAKULA CHAKE (cha kuwatosha watakaokaa humo, ameyafanya haya) KATIKA SIKU NNE (mida minne). HAYA NI SAWA  KABISA KWA HAO WANAOULIZA (mambo wakataka kuyajua).” (41:10)

Rasilimali ya kututosha sisi leo na hao watakaokuja kesho tayari ipo, kinachohitajika tu ni nguvu kazi iambatanayo na juhudi, maarifa na  matumizi sahihi ya rasilimali hiyo, sambamba na kuilinda kwa faida yetu na faida ya vizazi vijavyo.



Forum | Guestbook | Tuandikie |