|
Allah Sub-haana wa taala – kwa hekima zake tukufu
zisizohojiwa: “HAULIZWI (Allah) ANAYOYAFANYA (kwani yote ni ya haki) LAKINI
WAO (Viumbe) WATAULIZWA” (21:23). Humfanya huyu tajiri na yule fukara, humpa nguvu
huyu na yule kumfanya mnyonge/dhaifu. Humfanya huyu kuwa mwerevu na yule kuwa
mpumbavu, huyu humfanya mweupe na yule mweusi. “NA KAMA MOLA WAKO
ANGALIPENDA, ANGALIWAFANYA WATU WOTE KUWA UMATI MMOJA. KWA HIVYO WATAENDELEA
TU KUHITILAFIANA.” (11:118).
Lakini kumbe kuhitilafiana kwa viumbe katika lugha
rangi, maumbile, hali za kiafya na kimaisha…….na…….ni alama/ishara ionyeshayo
uweza wa Allah: “NA KATIKA ISHARA ZAKE (za kuonyesha uweza wake) NI KUUMBA
MBINGU NA ARDHI, NA KUHITILAFIANA LUGHA ZENU NA RANGI ZENU NA (mengine yenu,
na il-hali Muumbaji ndiye huyo huyo mmoja). KWA YAKINI KATIKA HAYA ZIMO
ISHARA KWA WENYE UJUZI” (30:22).
Ni
kutokana na na hekima hizi hizi,
Allah humfanya huyu kuwa ni mzai na yule kuwa ni tasa, huyu humpa watoto wa
kike tu. Hivyo ndivyo tunavyosoma
ndani ya kitabu kisicho na shaka na kilicho muongozo kwa watu wote” UFALME WA
MBINGU NA ARDHI NI WA ALLAH, ANAUMBA APENDAYO, ANAMPA AMTAKAYE WATOTO WA KIKE
NA ANAMPA AMTAKAYE WATOTO WA KIUME, AU HUWACHANGAYA (watoto) WA KIUME NA WA
KIKE (Kwa mtu mmoja) NA HUMFANYA TASA
AMTAKAYE, HAKIKA YEYE NI MJUZI, MUWEZA” (42:49-50)
Aya zinabainisha bayana kwamba anayetoa uzazi au
utasa ni Allah pekee. Suala linajitokeza. Je, ni halali kwa wawili (mke na mume) waliopewa mtihani wa utasa
na Allah kutafuta mtoto kwa kutumia njia za kitaalamu kamavile “Upandikizaji
wa mbegu za uzazi katika tumbo la uzazi”?!.
Tunasema hali ya kuwa tunalitarajia sana msaada wa
Allah aliye Mjuzi mno: Upandikizaji tunaoukusudia hapa ni ule ukutanaji wa
mbegu za uzazi za mwanamume na yai la mwanamke bila ya maingiliano ya moja
kwa moja ya kimwili kwa lengo la kupata mtoto. Huu ndio upandikizaji
tunaouzungumzia hapa. Tafadhali elewa hivyo.
Suala hili la upandikizaji wa mimba si muuujiza
wala suala geni ulimwenguni hapa. Asili ya mwanadamu iligundua uwezekano wa
jambo hili miongo kadhaa ya miaka iliyopita. Historia iantuonyesha kwamba
Waarabu waliitumia njia hii ya upandikizaji katika kupandikiza mitende katika
karne ya kumi na nne (14thC A.D). Nazo nchi za Magharibi zikaigundua njia hii katika karne ya kumi na nane
(18thC AD) karne nne baada ya Waarabu. Mtu wa kwanza kufanya jaribio hilila
upandikizaji kwa binadamu alikuwa ni daktari wa Kiingereza, John Hunter mnamo mwaka 1899 miladia, na
jaribio hili lilihusisha mbegu za mwanamume (manii) kwa mkewe. Ama huu
upandikizaji wa mimba kwa mwanamke bila ya kutumia bmegu za mumewe bali kwa
kutumia mbegu za mtu mwingine, huu ulifanywa kwa mara ya kwanza nchini
Ufaransa mnamo mwaka 1918 Miladia. Kutoka hapo ndipo ulipoenea katika pande
mbalimbali za ulimwengu ulioendelea kisayansi na teknolojia mpaka wakafikia
kuanzisha benki ya mbegu za kiume (manii) kwa lengo hili la upandikizaji.
Utaalamu huu ukaendelea mpaka ukafikia hatua ya kupandikiza mbegu nje ya
tumbo la uzazi, zikapandikizwa ndani ya chupa iliyoandaliwa maalumu kwa
kazi hiyo. Chupa hii huwa mithili ya
kitaru cha miche ambapo ikikua huenda kupandikizwa shambani. Hivyo ndivyo
ilivyo kwa chupa hii, baada ya muda fulani kupita tangu kupandikizwa kwa yai,
yai hilo hurejeshwa tena katika tumbo la mwanamke lililotwaliwa kwake yai
hilo au kwa mwanamke mwingine yeyote. Na pengine huwekwa katika tumbo la hayawani mwingine asiye mwanadamu ili
aibebe mimba hiyo aliyopandikizwa badala ya binadamu (mwanamke). Hapa ndipo
ulipofumuka upinzani dhidi ya upandikizaji huu wa mimba kutoka katika
majukwaa ya kidini na ya kisiasa. Khasa khasa pale upandikizaji
unapowahusisha watu wasiokuwa mke na mume, au ulezi wa mimba anapopewa
mwanamke mwingine au mnyama.
Mafaqihi (Wataalamu mabingwa wa sheria ya Kiislamu
wamesema kwa sura ya jumla kwama.
·
Utapokuwa upandikizaji wa mimba ni kwa manii ya mume kwa mkewe,
hapana kizuizi iwapo kutakuwa na uhakika na uthibitifu wa hilo.
·
Ama upandikizaji utakapohusisha manii ya mtu mwingine asiye mume,
hapa itakuwa hairuhusiwi kisheria.
Baada ya kutolewa fatua hii, maswali mengi
yakachimbuka kutokana nayo, yakaelekezwa katika Baraza la Fatwa, la Misri.
Baraza likayajibu maswali hayo mwezi 6 mfunguo 8, mwaka 1400 Hijiria sawa na
tarehe 23 Machi, mwaka 1980 Miladia, chini ya Mufthi Shaykh Jaadul –haq Aliy
jaadul-Haq.
Ufuatao ni mukhtasari wa fatwa hiyo kwa
utaratibu wa swali na jawabu:
SWALI 1: Kuna
hukumu gani iwapo yatatwaliwa manii ya mume na kupandikizwa mkewe aliye tasa
(asiyeshika mimba) wakiwepo wote wawili (mume na mke)?
JAWABU: kwa kuwa lengo kuu la mafungamano na mahusiano ya kimaumbile
baina ya mume na mke ni kupata watoto ili kuendeleza jamii ya wanadamu. Na
kukawa kuna matatizo ya kimaumbile au maradhi baina ya mke na mume au mmoja
wao. Matatizo yanayopelekea kushindikana kutunga mimba katika njia ya kawaida
ya kimaumbile kama alivyotaka Allah. hapo anaruhusiwa kisheria kutumia njia hii ya upandikizaji
iwapo wawili hao (mke na Mume) wataona kuna haja ya kufanya hivyo. Kwa sharti
kwamba upandikizaji mimba huu uwe ni
kwa dhati ya mani ya mume kwa mkewe, bila ya kubadilishwa au kuchanganywa na
manii ya mwanamume mwingine au mnyama.
SWALI 2: Vipi, iwapo manii ya mume hayana uwezo katika upandikizaji,
yakatwaliwa manii ya mwanamume mwingine na kupandikizwa kwa mkwe.
JAWABU: Kupandikizwa mke manii ya mwanamume mwingine asiye mumewe kwa
kigezo cha kutokufaa manii ya mumewe katika suala zima la upandikizaji mimba
ni jambo lililohalalishwa kisheria. Uharamu huu unatokana na kuchanganyika
kwa nasabu na kumnasibisha mtoto na baba ambaye hatokani na manii yake manii
ya mtu mwingine, kisha mtoto awe wa mtu mwingine?
SWALI 3: Vipi, ikiwa yatachukuliwa manii ya mume na kupandikizwa na yai la mwanamke asiye mkewe. Kisha
yai hili lilopandikizwa likahamishwa
na kwenda kuwekwa katika tumbo la uzazi la mwanamke ambaye mumewe ndiye
mwenye manii yale.
JAWABU: Sura hii hatofautiani sana na ile sura ya kwanza, inaingia chini ya maana ya zinaa. Mtoto
atakayeumbwa na kuzaliwa kupitia utaratibu huu atahesabika kisheria kuwa ni
mtoto wa haramu (wa nje ya ndoa) kwa yakini. Hata kama manii haya ni ya mume
lakini kama ijulikanavyo ni kwamba mimba haitungi ila kwa idhini na mapenzi
ya Allah wakati manii ya mume yanapokutana na yai la mkewe. Katika sura hii
yai la mke linakosekana na badala yake linatumika yai la mke linakosekana na badala yake linatumika
yai la mwanamke mwingine asiye mke wa mwanamume mwenye manii husika. Hili linamfanya mke asiwe konde
kama alivyokusudia Allah iwe:” WAKE ZENU NI KAMA KONDE ZENU. BASI ZIENDENI KONDE
ZENU MPENDAVYO……..” (2:223).
Katika sura hii mke hakuwa konde kwa sababu zao
(mtoto) limezalishwa na konde nyingine (mwanamke asiye mke). Mimba anayoibeba
mwanamke ni lazima iwe ni natija ya maingiliano ya kisheria ya kimaumbile
baina ya mke na mume. Iwe ni kwa njia ya kawaida ya kukutana katika tendo la
ndoa au kwa upandikizaji wa yai na kisha kurudishwa katika tumbo la uzazi ili
likue na kisha kuzaliwa mtoto kama
alivyosema Allah: “….HUKUUMBENI MATUMBONI MWA MAMA ZENU – UMBO BAADA YA UMBO
– KATIKA VIZA VITATU……..” (39:6)
Fatwa hii ni ndefu lakini sisi tumeifupisha kwa
kiasi ambacho kitakusaidia kukupa mwangaza katika suala zima la upandikizaji
wa mimba ambao leo umeenea ulimwenguni kote khasa ulimwengu wa Magharibi. Kwa
ufahamu zaidi juu ya suala hili ikiwa hukutoshelezwa na maelezo yetu, unaweza
kuwauliza masheikh waliokuzunguka hapo ulipo.
|