|
Uaminifu/Amana tunayokusudia hapa ni kule kuzihifadhi haki za MwenyeziMungu
Mtukufu zilizotupasa sambamba na haki za binadamu wenzetu. Mtu akizichunga na kuzihifadhi
haki za Mola wake na za wanadamu wenziwe huyo ataitwa mwaminifu mwenye amana mbele ya
hadhara tukufu ya MwenyeziMungu na machoni mwa binadamu wenziwe. Kwa kupitia uaminfu wake
mali na heshima za watu zitahifadhika.
Tunaposema uaminifu/amana ni kuhifadhi haki za MwenyziMungu tunamaanisha nini ?
Kuhifadhi haki za MwenyeziMungu hupatikana kwa kutekeleza amri na maagizo yake yote bila
ya kuwa na khiyari ya kuchagua lipi utende na lipi usitende. Umeamrishwa kuswali, basi ni
lazima uswali, umeamrishwa kuwatendea wema wazazi wako basi inakulazimu kuwatendea wema.
Kadhalika kuhifadhi haki za MwenyeziMungu ni kujiepusha na kuyaacha yote aliyokataza.
Umekatazwa ulevi, basi ni wajibu usilewe, umeharamishwa zinaa basi usizini. Kwa ujumla
utakapofikia daraja ya kutenda tu lile uliloamrishwa na kuacha kila ulilokatazwa, hapo
utahesabiwa mbele ya Mola wako umezihifadhi haki zake zilizokulazimu.
Ama kuhifadhi haki za binadamu, waja wa MwenyeziMungu ni pamoja na kurudisha amana
za watu kwa wenyewe, zikiwa kama ulivyopewa bila kupunguza chochote wala kudai ujira.
Kutozifichua siri za watu, kutokuvunja ahadi ulizozifunga kwa uliowaahidi. Kutokumfanyia
gushi/udanganyifu/utapeli mtu yeyote. Kuvitumia viungo vyako vya mwili kwa malengo
vilivyoumbiwa. Iwe kazi ya jicho lako kwenye kutizama vilivyo vya halali, ulimi utumike
kusema kweli na maneno mazuri yenye nasaha. Moyo wako usimdhanie mtu kwa jambo lenye
kumdhuru. Utupu (uchi) wako usitumike katika uzinifu/ulawiti na kama hivi kwa baki ya
viungo vingine vya mwili. Hii ndio maana ya kuhifadhi haki za binadamu. Iwapo watu
watazifasiri maana hizi za kuhifadhi haki za MwenyeziMungu na za waja wake katika maisha
yao ya kila siku, hapana shaka dunia yetu hii itakuwa ni kisiwa cha amani. Kisiwa ambacho
mali na heshima za watu zina dhamana. MwenyeziMungu Mtukufu anatuagiza :
"HAKIKA ALLAH ANAKUAMRISHENI KUZIRUDISHA AMANA KWA WENYEWE (wanaozistahiki) NA
MNAPOHUKUMU BAINA YA WATU MHUKUMU KWA HAKI [4:58]
Uaminifu ni kielelezo cha imani ya mja. Haya yanathibitishwa na kauli ya Bwana
Mtume - Rehma na amani zimshukie aliposema :
"Hana imani mtu asiye na amana na wala hana dini mtu asiye na ahadi" Ahmad,
Ibn Hibban na Albayhaqi kutoka kwa Anas-Allah amwiye radhi.
Kadhalika uaminifu/amana ni chanzo cha riziki maridhawa kwa mja. Bwana Mtume
Rehma na Amani zimshukie anatuambia :
"Amana/Uaminifu huvuta/huleta riziki na khiyana huleta ufakiri" Al-Dailamy
kutoka kwa Jabir kwa Imam Ally awawiye radhi.
Khiyana iliyoelezwa katika hadithi kuwa ni mojawapo ya sababu za ufakiri ni
kutohifadhi haki za MwenyeziMungu Mtukufu na waja wake. Hapana shaka kuwa khiyana ni
miongoni mwa sifa na tabia mbaya ambayo mwislamu hapaswi kujipamba nazo. Miongoni mwa
athari na sifa mbaya hizi ni :
Kwanza : Mwenye khiyana husifika na sifa ya udanganyifu/utapeli na upungufu wa
dini. Sifa hizi humuweka katika nafasi mbaya katika jamii aishimo. Jamii humtazama kwa
jicho la tahadhari kubwa, ktokana na madhara anayoweza kuwasababishia wakati wowote.
Pili : Mwenye Khiyana ana nafasi kubwa ya kutengwa na jamii, hana thamani machoni
mwa wanajamii na huonekana ni mtu duni asiye na maana. Hizi ni baadhi tu ya athari za
tabia hii mbaya ya khiyana. Tunasoma ndani ya Qur-ani :
"ENYI MLIOAMINI ! MSIMFANYIE KHIYANA ALLAH NA MTUME WAKE (mkaacha kufuata
mliyoamrishwa) WALA MSIKHINI AMANA ZENU (mnazoaminiana wenyewe kwa wenyewe) NA HALI MNAJUA
(kuwa ni vibaya hivyo)"
|