Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Akhlaaq-Tabia  

"Hakika si vingine nimetumwa kuja kutimiza TABIA NJEMA" Hadith Tukufu

WASIA MARIDHAWA KWA KILA MUISLAMU .....VI

 

G/. JIEPUSHE NA GHURURI (kutoka darsa iliyopita) 

Ewe ndugu yangu Allah-akuongoze katika kuyafuata ayaridhiayo na kuyapenda. Naam, sasa naomba uniazime fikra, moyo na usikivu wako nikupigie mifano ya ghururi kwa  janibu ya watu maasi. Kukosea na kufanya madhambi iwe ni kwa bahati mbaya au kwa makusudi ni sehemu ya maumbile ya mwanadamu, hili halipingiki. Sasa basi mtu anapoasi kisha akatubu na kumuomba maghfira Mola wake kwa ulimi tu, bila ya kujua sharti za toba na uhakika wake. Kisha kwa huku kutamka kwake: “ASTAGHFIRULLAH” kwa ulimi tu, akadhania na kuitakidi kabisa kwamba amekwishatubia na Allah amemghufiria. Huyu ni maghururi na hicho akifanyacho ni ghururi tu.

Hii nayo ni ghururi, mtu kukithirisha kufanya maasi na akaendelea na maovu hayo huku akizembea kutekeleza wajibu wake katika twaa. Halafu akawa anajihalalishia uovu wake huo kwa hoja kwamba hiyo ndiyo ‘Qadari’ ya Allah kwake. Na kwamba yeye hana khiyari ya kutenda ama kutokutenda, kwani yote ayatendayo au kuacha kuyatenda ameandikiwa na Allah Mola Muumba wake. Katika aina zote za ghururi hii ndio kubwa yao na mwenye kuifuata ghururi hii ni mzushi na si vinginevyo.

Kadhalika miongoni mwa ghururi kwa janibu hii ya watu maasi ni mtu kuwa na matumaini ya kupata maghfira huku akizembea kutekeleza maamrisho na kujiepusha ma maharimisho. Baadhi ya watu maasi wasiofanya ibada hupata kusema: (Hakika Allah hana haja nasi wala amali zetu, madhambi yetu hayamdhuru wala twaa zetu hazimnufaishi). Maneno yao haya ni haki iliyolengwa batili ambayo shetani ameitia moyoni mwa huyu maghururi. Kisha akayapitisha ulimini kwake ili apate kumkata na kumtenga na maghfira na aache kuyahangaikia, jambo ambalo ni amri ya Mola wake. Hii nayo haipungui kwa cho chote katika mizani ya ghururi.

Ndugu yangu katika imani-Allah aithubutishe imani yako-nakusihi uendelee kunitegea sikio katika mifano hii hai ya ghururi ili uepuke kutumbukia humo kwa msaada wa Allah. Utawaona baadhi ya watu wakibweteka kufanya amali njema zitakazowanufaisha mbele ya Allah, wakijinasibisha na kutegemea wema na uongofu wa baba zao. Wanafanya hivyo bila ya kuwaiga katika mazuri yao hayo waliyoyafanya, hii ni ghururi mbaya na isitoshe ni upumbavu muovu. Ingelikuwa wema na uongofu wa wazee unawafaa watoto wao  bila ya wao kushirikiana nao katika wema na uongofu huo. Basi mwanawe Nabii Nuhu-Amani imshukie-angelinufaika na utume na amali za baba yake, lakini ilikuwaje, hii hapa Qur-ani Tukufu itegee sikio mwenyewe: “NA NUHU ALIMUOMBA MOLA WAKE (alipomuona mwanawe anaangamia) AKASEMA: EWE MOLA WANGU! MWANANGU NI KATIKA WATU WA NYUMBANI KWANGU (mbona anaangamia)? NA HAKIKA AHADI YAKO NI HAKI, NAWE NI MWENYE HAKI KULIKO MAHAKIMU (wote). AKASEMA (Allah): EWE NUHU! HUYU SI MIONGONI MWA WATU WAKO. YEYE NI (mwenye) MWENDO USIOKUWA MZURI. BASI USINIOMBE AMBAYO HUYAJUI. MIMI NAKUNASIHI USIWE MIONGONI MWA WAJINGA” [11:45-46]

Utaona kwa mujibu wa aya kwamba wema wa mzazi bila ya wewe mwenyewe kuwa mwema hautakunufaisha kwa cho chote mbele ya Allah ila kama utamfuata kwenye wema huo. Hivi ndivyo isemavyo Qur-ani: “NA WALE WALIOAMINI NA WAKAFUATWA NA VIZAZI VYAO NA WATOTO WAO KATIKA IMANI. TUTAWAKUTANISHA NAO HAO JAMAA ZAO, WALA HATUTAWAPUNJA KITU KATIKA (thawabu za) VITENDO VYAO, KILA MTU ATALIPWA KWA KILE ALICHOKICHUMA”. [52:21]

Hii nayo haiachi kuwa ni aina ya ghururi, mtu kukutana na waja wema, akawatumikia kwa dhana njema kabisa. Lakini akajiepusha na kujitenga na mwendo wao mwema na kulazimikiana kwao na twaa ya Allah. Kisha akataraji kwa kuwatumikia tu mabwana hawa bila ya kuwaiga katika mema yao ataipata tu pepo ya Allah kwa baraka zao. Hii ni ghururi na wazimu mtupu tu.

Aina za ghururi ni nyingi mno kuliko tulivyowafikiwa kuzitaja na wala mja hataokoka na ghururi hizi ila ni kwa kurejea kwa Allah na kutegemea fadhila na ukarimu wake. Kurejea huko kuwe ni pamoja na kutinda na kupania katika kumtii na kujitahidi katika kumuabudu. Yote haya yaende sambamba na kujiepusha pamoja na kujitenga na maasi na kumshukuru kwa kukuwezesha kuwa katika twaa yake. Huku ukidumisha unyenyekevu, dua na istighfari mchana na usiku.

 



Forum | Guestbook | Tuandikie |