|
WASIA
WA SABA: JIEPUSHE NA GHURURI (MADANGANYO) ZA DUNIA.
Ewe
ndugu mpenzi katika imani-Allah akurehemu. Ninamuomba Allah atuwafikishe
kufahamu kuwa miongoni mwa mambo yenye kuhilikisha ni “ghururi”.
Pengine utataka kuniuliza ghururi ni nini? Ikiwa hivyo ndivyo, basi
ninakusihi uniazime sikio la usikivu. Ninasema, ghururi: ni kitendo cha
mtu kuichanganya nafsi yake kwa kuionyesha mambo/vitu kinyume na uhalisia
wake. Kwa mantiki hii, tunaweza kusema kuwa ghururi ni madanganyo
ya nafsi yanayotokana na uoni dhaifu (ujuzi duni) katika dhana nzima ya
dini. Pia kutokana na maarifa lemavu juu ya uhalisia wa dini ambao
husababishwa na kujikingikiwa (kutokujua) athari ya amali mbaya na vitimbi
vya adui shetani. Ghururi huchangiwa kwa kiasi kikubwa na matamanio ya
nafsi yanayomtawala na kumpeleka hovyo mwanadamu. Allah Mola Mtukufu
anatutahadharisha waja wake na ghururi, anatuambia: “ENYI WATU! BILA
SHAKA AHADI YA ALLAH NI HAKI. BASI YASIKUGHURINI (yasikudanganyeni)
MAISHA YA DUNIA. WALA YULE GHARURI (mdanganyaji mkubwa; Iblisi)
ASIKUGHURUNI JUU YA ALLAH. KWA YAKINI SHETANI NI ADUI YENU, BASI
MFANYENI ADUI (yenu, kwa hivyo msimtii) KWA ANALIITA KUNDI LAKE LIWE
KATIKA WATU WA MOTONI”. [35:5-6]
Allah
anatutajia baadhi ya wasifu wa watu walioghurika kupitia kauli yake:
“SEMA: JE! TUKUJULISHENI WENYE KHASARA KATIKA VITENDO (vyao)? HAO AMBAO
BIDII YAO (hapa duniani) IMEPOTEA BURE KATIKA MAISHA YA DUNIA, NAO
WANAFIKIRI KWAMBA WANAFANYA AMALI NJEMA! HAO NI WALE WALIOZIKATAA
(waliozikanusha) ISHARA ZA MOLA WAO NA (wakakataa) KUKUTANA NAE. KWA HIVYO
VITENDO VYAO VIMERUKA PATUPU, WALA HATUTAWASIMAMISHIA MIZANI SIKU YA
KIYAMA. HIVYO JAHANAMU NI MALIPO YAO KWA SABABU WALIKUFURU NA KUZIFANYIA
MZAHA AYA ZANGU NA MITUME YANGU”. [18:103-106] Bwana Mtume-Rehema na
Amani zimshukie-anatubainishia ni nani mwenye akili na nani hamnazo,
anasema: “Mtu mwenye busara (akili) ni yule aliyeihifadhi nafsi yake na
akafanya amali njema kwa ajili ya maisha baada ya kufa. Na mtu ajizi
(mlemavu wa akili) ni yule aliyeifuatishia nafsi yake matamanio yake (hiyo
nafsi) na akatamani kwa Allah matamanio (matarajio) matupu (yasiyo na
amali njema)”. Tirmidhiy
Ewe
ndugu yangu uliyemuamini Allah na Mtume wake, fahamu na uelewe kuwa kuna
aina nyingi za ghururi. Kama ambavyo zilivyo mbeya (sampuli) za wenye
kughurika katika janibu (pande) zote mbili; janibu ya twaa na ile ya
maasi. Hebu nipe nafasi nikupigie mfano wa ghururi kwa janibu ya wana twaa
(watu walio katika twaa ya Allah) ili tupate kwenda sambamba katika darsa
yetu hii. Sote tunatambua fika kwamba kutafuta elimu ni fardhi ya lazima
kwa kila muislamu; mwanamume na mwanamke. Mja akachagua kumtii Mola wake,
akajiingiza katika harakati za kuitafuta elimu. Allah akambariki katika
jitihada zake hizo akamruzuku elimu, lakini yeye baada ya kuipata hiyo
elimu akawa anafanya ngojangoja kutenda amali kwa mujibu wa elimu
aliyoipata. Kisha akaghurika na kauli zilizopokewa katika kutaja ubora wa
elimu na na fadhila za kuitafuta. Huku akighafilika na kauli zilizopokewa
katika kutaja makamio makali kwa upande wa mtu asiyetenda kwa mujibu wa
elimu yake. Fahamu ewe ndugu yangu mwanachuoni, mwanafunzi, msikilizaji wa
elimu na mpenzi wa elimu kwamba elimu uliyoruzukiwa na Mola wako inaweza
kuwa ni hoja ama ya kukuokoa au kukuangamiza. Elimu itakayokunufaisha na
kukuokoa leo hapa duniani na kesho kule akhera ni ile iambatanayo na amali
(matendo). Ama elimu bila ya amali, haya ni maangamivu tu na si vinginevyo
na ghururi tupu. Mfano mwingine, sote tunakongamana kwamba ni wajibu wa
mwenye kujua kukifundisha alichokijua kwa wenzake wasiojua. Huku akiamini
kuwa elimu aliyonayo ni amana na ni neema ya Allah, kwa hivyo ataulizwa
aliitumiaje: “KISHA KWA HAKIKA MTAULIZWA SIKU HIYO JUU YA NEEMA
(mlizopewa mlizitumiaje)”. [102:8]
Mtu
akijitua dhima hii kwa kuamua kufundisha, lakini akafundisha kwa malengo
fulani. Akafundisha ili apate uongozi na vilivyo mikononi mwa watu na huku
akidhania na kuitakidi kwamba yeye amesoma na anasomesha kwa ajili tu ya
Allah. Hii pia si cho chote bali ni miongoni mwa aina za ghururi. Fahamu
ewe ndugu yangu kwamba fahari, kiburi na majivuno ni sumu kali na ni adui
mkubwa wa amali njema, kwani huzipomosha na kumrusha patupu mtendaji wa
amali hizo zilizochanganyika na sifa mbaya hizo. Au mtu akafanya ibada kwa
ajili ya kuwaonyesha watu (ria) na kutafuta daraja/utukufu kwao. Huku yeye
mwenyewe akijiona kuwa anafanya amali hizo kwa ajili ya Allah (Ikhlaaswi)
na kwa ajili ya kujikurubisha kwake. Huyu ni maghururi anaidangaya nafsi
yake, kwani hana atakachokipata mbele ya Allah kwa amali yake hiyo. Ama
daraja, utukufu na kuonwa na watu haya atayahodhi tu bila ya shaka kwa
sababu ndio aliyoyakusudia. Mtendaji twaa wa namna hii tunamnasihi amtegee
sikio swahaba wa mtume; Abuu Dardaai-Allah amuwiye radhi-asemaye: (Uzuri
ulioje/wema ulioje wa usingizi na kula kwa watu wale wenye akili.
Jinsi/namna wanavyoishinda kesha na funga ya watu wajinga. Amali ya uzani
wa mdudu chungu ya mtu mwenye yakini na taqwa ni bora zaidi amali hiyo
kuliko amali mfano wa majabali za watu walioghurika).
Hii
ni baadhi tu ya mifano ya ghururi katika twaa, nakuomba ewe ndugu yangu
usinitupe mkono katika darsa ijayo ili nikupigie mifano ya ghururi katka
janibu ya maasi.
|