|
Maana;
Wasia ni neno lenye asili ya
lugha ya Kiarabu ni neno ambalo limetumika ndani ya Qur-ani Tukufu,
hadithi za mtume na baki ya maandishi mengine ya kiarabu.
Neno
hili kama lilivyotumika ndani
ya Qur-ani na Sunah lina maana ya maneno
yenye maadili maonyo yanayolenga :-
Kunasihi/kuamrisha
juu ya ama kutenda au kutokutenda
jambo fulani.
Kuadabisha
na kutoa muongozo juu ya suala
zima la maisha.
Kuelekeza,
kukosoa na kurekebisha tabia .
CHIMBUKO
:
Asili na chimbuko la
darsa yetu hii ya wasia ni kauli yake
Allah Mola Mwenyezi ambayo ni
wasia wake kwa walimwengu wote: “...NA KWA YAKINI TULIWAUSIA (amri)
WALIOPEWA KITABU KABLA YENU, NA NYINYI (pia) KWAMBA MUMCHE ALLAH (wasia)…”
(4:131)
Na
inaeleweka wazi kwa kila mmoja wetu kwamba kumcha Allah (Taqwa) ni
kujiepusha na makatazo ya Allah na kuyatekeleza maamrisho yake.
LENGO/MADHUMUNI:
Darsa hizi za wasia zinalenga kumjenga musislamu kiutu na kitabia
ili:-
-
Maisha
yake yote yatoe taswira ya Uislamu, yaani awe ni Uislamu unaotembea.
-
Awe
ni kigezo cha utu na tabia njema katika jamii anayoishi nayo.
-
Afikie
daraja ya Ucha–Mungu (Taq-wa) kwa kutenda anayoamrishwa katika wasia
na kuacha anayokatazwa.
Mpenzi
msomaji wetu, darsa hizi za wasia ambazo ni sehemu ya somo la Akhlaaq
zitakujia katika mfululizo utakaokuwa chini ya anuani munasibu.
Ni matarajio yetu makubwa kwamba wasia huu
maridhawa utakunufaisha katika maisha yako binafsi, ya kijamii, ya
ulimwengu huu na ule ujao. Kwa
fadhila zake Allah ambaye ndiye aliyetuelekeza katika sula zima la wasia. Sasa kwa msaada wake Allah tuingie katika darsa zetu hali ya
kuwa tunakusudia kujiusia sisi nafsi zetu na wewe msomaji wetu.
WASIA
WA KWANZA.
a)
KUWA NA HURUMA.
Muislamu unausiwa na kuhimizwa kujipamba na tabia ya huruma kamili
kwa viumbe wote wa Allah; wanadamu wenzio na wasio wanadamu.
Ishi na wanadamu wenzio na changanyika nao kimaisha kwa kuwaonyesha
upole na huruma. Uwe mpole na
mwenye huruma hata kwa wale walio maadui zako na wanaokufanyia hasadi
katika neema ulizopewa na Mola wako.
Ni wajibu wako kutambua kwamba mwanadamu ikiwa ni pamoja na wewe
mwenyewe ni kiumbe dhaifu: “…MWANADAMU AMEUMBWA DHAIFU (hana nguvu
kubwa kabisa za kiwiliwili wala nguvu kubwa
za kupigana na moyo na shetani).”
(4:28). Ukiri udhaifu
huu wa mwanadamu ambao ni sehemu ya maumbile yake na umuhurumie.
Umuhurumie na umchukulie upole hata adui yako, kwani kwa yakini Allah Mola
Mwenye huruma huwaonea huruma waja wake wenye kuwaonea huruma wanadamu
wenzao. Hivi ndivyo unavyoambiwa na Mtume wako–Rehema na Amani zimshukie:
“Wenye huruma watahurumiwa na Mwingi wa rehema (Allah), wahurumieni
walioko ardhini (viumbe wenzenu) atakuoneeni huruma aliyeko
mbinguni (Mola muumba wenu)”. Ahmad, Abuu Daawaud, Tirmidhiy
& Al-Haakim
Ni
bora na ni kheri kwako ukamuhurumia mwanadamu mwenzio kwa udhaifu wake,
kwani kumbuka kwamba asiyehurumia ahurumiwi. Hebu jiulize, je wewe hutaki
huruma ya Allah Mola Mwenye huruma? Kama unaitaka, basi itafute huruma
hiyo kwa kuwahurumia viumbe wenzio kila unapowapata udhaifu wa kibinadamu.
Huruma yako hii isikomelee tu kwa wanadamu wenzio bali iwaenee hata
wanyama ambao Allah amewaumba kwa ajili ya manufaa yako.
Imepokelewa kutoka kwa Abuu Hurayrah–Allah amuwiye radhi–kwamba
Mtume wa Allah-Rehma na Amani zimshukie amesema: “Wakati ambapo mtu
mmoja akienda njiani, kikamshika kiu kikali kabisa akashuka kisimani
akanywa maji humo, kisha akatoka (kuendelea na safari yake). Tahamaki huyo
mbele yake ni mbwa anahema na kula mchanga kutokana na ukali wa kiu.
Akajisemea: Bila ya shaka kimempata (mbwa) huyu kiu kama kilichonipata
mimi (hivi punde tu). Akakijaza
maji kiatu chake kisha akakiuma kwa mdomo wake, akapanda (kutoka kisimani
mle). Akaja akamnywesha maji mbwa yule, Allah akakishukuru kitendo chake
kile cha huruma, akamsamehe dhambi zake kwa sababu hiyo. (Maswahaba)
wakauliza: Ewe Mtume wa Allah, hivi sisi tuna ujira kwa (kuwatendea huruma
hata) wanyama! Mtume akawajibu: “Katika kila ini bichi (kilicho hai)
kuna ujira.” Bukhaariy
Hebu
ndugu muislamu na tuienzi kauli hii ya Mtume wetu–Rehema na Amani
zimshukie-kwa kuwaonea huruma wanyama: “Mwenye kukihurumia walau
kichinjwa cha ndege, Allah atamuonea huruma siku ya kiyama.”
Bukhaariy, Twabaraaniy & Dhwiyaa
Elewa
kumuhurumia kiumbe dhaifu mithili ya ndege unayetaka kumchinja kwa ajili
ya kitoweo chako si kuacha kumchinja.
Bali ni kutokumtesa au kumchinja kikatili.
WASIA
WA PILI.
b)
WAEPUSHIE WENGINE SHARI ZAKO:
Muislamu unausiwa uishi na wanadamu wenzio na ujitahidi upeo wa
jitihada zako shari zako zisiwafikie kwa namna yote ile iwayo. Kwani kwa
kufanya hivyo, Allah atakukinga na kukulinda na shari na maudhi yao.
Tambua kwamba imethibiti kutoka kwa Bwana Mtume– Rehema na Amani
zimshukie: “Mwenye kutaka salama, basi na aitafute katika salama ya
mwenziwe kutoka kwake.”
Wanuwilie
kheri wanadamu wote khususan waislamu na wala usiwadhamirie shari. Wala
usimfanyie undani na chuki muislamu mwenzio, bali muislamu mwema ni yule
asemaye: “…MOLA WETU! TUSAMEHE SISI NA NDUGU ZETU WALIOTUTANGULIA (kufa)
KATIKA USILAMU WALA USIJAALIE KATIKA NYOYO ZETU UNDANI KUWAFANYIA WISLAMU
( wenzetu) MOLA WETU! …” (59:10)
Ukiwa
una sifa hii, huna undani wala mfundo kwa waislamu wenzako utakuwa
umejijengea ngome imara dhidi ya shari zao na Allah atakuvika taji la Ucha–Mungu.
Kisha ninakuusia tuuzingatie kwa pamoja wasia wa Luqmaan kwa mwanawe kama
alivyousajili Allah ndani ya Qur-ani Tukufu “…EWE MWANANGU! USIMSHIRIKISHE
ALLAH, MAANA SHIRKI NDIYO DHULUMA KUBWA.” (31:13) Akaendelea
kumuusia: “EWE MWANANGU! KWA HAKIKA JAMBO LO LOTE LIJAPOKUWA NA UZITO WA
CHEMBE YA HARDALI, LIKAWA NDANI YA JABALI AU MBINGUNI AU KATIKA ARDHI,
ALLAH ATALILETA (amlipe aliyefanya) BILA SHAKA ALLAH NI MJUZI WA MAMBO
YALIYOFICHIKANA (na) MJUZI WA MAMBO YALIYO DHAHIRI. EWE MWANANGU! SIMAMISHA
SWALA, NA UAMRISHE MEMA NA UKATAZE MABAYA, NA USUBIRI JUU YA YALE
YATAYOKUSIBU (kwani mwenye kuamrisha mema na kukataza mabaya lazima
zitamfika tu taabu) HAKIKA HAYO NI KATIKA MAMBO YANAYOSTAHIKI KUAZIMIWA (na
kila mtu) WALA USIWATAZAME (usiwafanyie watu jeuri) KWA UPANDE MMOJA WA
USO, WALA USENDE KATIKA NCHI KWA MARINGO, HAKIKA ALLAH HAMPENDI KILA
AJIVUNAE, AJIFAKHIRISHAYE NA USHIKE MWENDO WA KATIKATI, NA UTEREMSHE
SAUTI YAKO, BILA SHAKA SAUTI YA PUNDA NI MBAYA KULIKO SAUTI ZOTE (kwa
makelele yake bure)” (3:16-19)
Ninazidi
kukuusia ewe ndugu yangu mpenzi pamoja na kuiusia nafsi yangu ya kwamba
tuwe miongoni mwa waja wa Rahmaani–Allah mwingi wa rehema: “….AMBAO
WANAOKWENDA (na kurejea) ULIMWENGUNI KWA UNYENYEKEVU, NA WAJINGA WAKISEMA
NAO (maneno mabaya) HUWAJIBU (maneno ya) SALAMA NA WALE WANAOPITISHA
BAADHI YA SAA ZA USIKU KWA AJILI YA MOLA WAO KWA KUSUJUDU NA KUSIMAMA NA
WALE WANOSEMA MOLA WETU! TUONDOLEE ADHABU YA JAHANAMU, BILA SHAKA ADHABU
YAKE NI YENYE KUENDELEA NA WALE AMBAO WANAPOTUMIA HAWATIMII KWA FUJO WALA
HAWAFANYI UBAKHILI, BALI WANAKUWA KATIKATI BAINA YA HAYO. NA WALE
WASIOMUOMBA MUNGU MWINGINE PAMOJA NA ALLAH, WALA HAWAUI NAFSI
ALIYOIHARIMISHA ALLHA ISIPOKUWA KWA HAKI, WALA HAWAZINI, NA ATAKAYEFANYA
HAYO ATAPATA MADHARA (papa hapa ulimwenguni kabla ya Akhera).”
(25:63–68)
Na
tuwe katika: “…WALE AMBAO HAWASHUHUDII SHAHADA ZA UWONGO, NA
WANAPOPITA PENYE UPUUZI, HUPITA KWA HISHIMA (yao) NA WALE AMBAO
WANAPOKUMBUSHWA AYA ZA MOLA WAO HAWAZIANGUKII KWA UZIWI NA UPOFU. NA WALE
WANAOSEMA: MAOLA WETU! TUPE KATIKA WAKE ZETU NA WATOTO WETU YABURUDISHAYO
MACHO (yetu, nyoyo zetu) NA UTUJAALIE KUWA WAONGOZI KWA WAMCHAO ALLAH”.
(25:72-74)
Ewe
ndugu yangu katika imani-Allah akurehemu-elewa na ufahamu kwamba
tukiushika wasia huu na tukajipamba na sifa hizi. Basi hapana shaka kwamba
tutakuwa ni malaika watembeao katika ardhi na ujira adhimu unatungojea
kesho mbele ya Allah: “…HAO (wenye sifa hizo) NDIO WATAKAOLIPWA
GHOROFA (za peponi) KWA KUWA WALISUBIRI, NA WATAKUTA HUMO HISHIMA NA AMANI.
WAKAE HUMO MILELE, KITUO KIZURI NA MAHALA PAZURI (kabisa) PA KUKAA”.
(25:75–76)
Tuusiane
na tutambue kuwa gharama na thamani ya kununulia hizo ghorofa za peponi
ambazo ni mahala pazuri mno pa kukaa mja ni kuishi katika ulimwengu huu
kwa kujipamba na sifa tulizozitaja. Mola
wetu Mtukufu tunamuomba atujaalie kwa fadhila zake kuwa ni miongoni mwa
“WAJA WA RAHMAANI” – Aamiyn!
|