|
3.
HAKI YA KUFANYA KAZI KULINGANA NA UWEZO:
Katika
jumla ya haki za mtumishi/mfanyakazi ni kuwa kazi anayopewa ilingane na
uwezo wake. Kwa maneno mengine mtumishi asikalifishwe kufanya kazi asiyo
na uwezo nayo. Hii ni kwa sababu: “ALLAH HAIKALIFISHI NAFSI YO YOTE
ILA YALIYO SAWA NA UWEZA WAKE...”. [2:286]
Ikiwa
Allah Mola Muumba na Bwana Mlezi mwenye kustahiki kutumikiwa na kuabudiwa
na kila kiumbe ukiwemo wewe muajiri, haikalifishi nafsi ila yaliyo katika
uweza wake. Ni dhahiri basi, kwamba hakuna mwenye haki ya kumkalifisha
mtumishi/muajiriwa kufanya kazi nzito na ngumu asiyoimudu. Au kumkalifisha
mtu mmoja kufanya kazi inayohitaji nguvukazi ya zaidi ya mtu mmoja hata
kama anamlipa. Huu si Uislamu na wala si ubinadamu kamwe, ni lazima kazi
husika iende sambamba na nguvukazi inayohitajika katika kuitekeleza kazi
hiyo. Hivi ndivyo Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-anavyoielezea
haki hii: “...Na wala msiwakalifishe (kufanya kazi) wasiyoiweza na
iwapo mtawakalifisha basi wasaidieni”. Bukhaariy & Muslim
Katika
kusaidia utekelezaji wa haki hii ni lazima uwepo muda maalumu wa kuanza na
kumaliza kazi. Muda huu ni wajibu uheshimiwe na pande zote mbili; mtumishi
na mtumikiwa (muajiri) ili kuwepo na ufanisi katika utendaji mzima wa kazi.
4.
DHAMANA YA MAHITAJI MUHIMU NA HIMAYA DHIDI YA MAJANGA YA KIMAUMBILE:
Uislamu
unampa mfanyakazi/mtumishi haki ya dhamana ya mahitaji yake muhimu kiasi
ya tosha ya maisha yake. Hivi ndivyo inavyofahamisha kauli ya Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie: “Atakayetawalishwa (atakayetawazwa)
kwetu sisi (kufanya) kazi fulani (kwa maslahi ya uma wa kiislamu) na (akawa)
hana nyumba, basi na ajifanyie nyumba (kutokana na mali ya waislamu). Au (akawa)
hana mnyama (kipando/gari), basi na ajitwalie mnyama (kwa mali hiyo)”.
Bukhaariy & wengineo
Kauli
hii ya Bwana Mtume kwa lugha ya leo inamaanisha dhamana (guarantee) ya
maisha bora kulingana na zama anazoishi mtumishi huyo wa uma. Dhamana hii
inahusisha:-
v
maskani (nyumba) bora na salama ya kuishi,
v
mke wa kumliwaza baada ya machovu yatokanayo na utumishi wa uma,
v
usafiri utakaomuwezesha kwenda katika utumishi wa uma na kurudi
nyumbani.
Ijapokuwa
hadithi hii imepokelewa katika kutaja na kubainisha haki za watumishi wa
dola/serikali ya kiislamu. Kwa yakini sababu iliyompelekea mtumishi huyu
wa dola kuyapata haya, ambayo ni kumuhakikishia na kumdhaminia tosha ya
maisha yake ili aweze kuifanya kazi aliyopewa kwa amani, utulivu na
ufanisi. Hapana shaka kwamba sababu hii inapelekea kuenea kwa hukumu kwa
wafanyakazi na watumishi wengine. Sherehe (ufafanuzi) hii ya kauli ya
Mtume haikusudii kusema kwamba kila muajiri analazimika kumpa muajiriwa
wake mahitaji yake yote ya lazima zaidi kuliko ujira anaoustahiki. Bali
maana yake ni kwamba dola ina wajibu wa kumtimizia mwananchi/raia wake
huyu kile asichoweza kukipata kutokana na kazi aifanyayo. Baadhi ya nchi
za Kiarabu na baadhi ya madola ya kimagharibi yamejaribu kwa kiwango
kikubwa kulitekeleza zoezi hili ambalo ni sehemu ya mfumo sahihi wa maisha
(Uislamu). Katika kulitekeleza zoezi hili nchi hizi zimefikia hatua ya
kumlipa mtoto mchanga aliyezaliwa, bila ya kumsahau mzee kikongwe
asiyejiweza. Huu ndio Uislamu, mfumo wa maisha waliochaguliwa wanadamu na
Mola Muumba wao: “...NA NIMEKUPENDELEENI (nimekuridhieni) UISLAMU UWE NI
DINI YENU...” [5:3]
Dola
ya kiislamu imdhaminie mwanadola haki ya tosha ya maisha yake na himaya ya
familia yake kutokana na maradhi, uzee au kifo. Hivi ndivyo ilivyokuja
katika hadithi ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie:
“Atakayeacha mali (baada ya kufa), basi mali hiyo ni (haki) ya warithi
wake. Na atakayeacha watoto walio dhaifu (hawana mali), basi na wanijie
kwani mimi ndio mlinzi/msimamizi wao”. Bukhaariy
Katika
hadithi hii, Bwana Mtume anawapa yatima walioachwa bila ya mali haki ya
kupata mali ya dola, kwa kiasi kitakachowahakikishia kupata mahitaji yao
ya msingi.
5.
HAKI YA KUTENDEWA VEMA (KIBINADAMU):
Tabia
na umbile la Uislamu ni umbile la sawa linalowaweka watu wote katika
daraja moja la usawa. Mkubwa na mdogo, tajiri na masikini, mtumishi na
mtumikiwa wote hawa ni sawa mbele ya macho ya Uislamu. Dhana hii ya usawa
katika Uislamu haikinzani na ukweli wa utukufu na ubora waliopewa baadhi
ya watu na Allah kwa hekima na busara azijuazo yeye mwenyewe. Haikanushi
kuwaweka watu kulingana na daraja zao mbele ya Allah na mbele ya jamii.
Kwa tabia na umbile hili la Uislamu ndio Bwana Mtume-Rehema na Amani
zimshukie-alivyoishi na watumishi wake. Tukimchulia Sayyidina Anas-Allah
amuwiye radhi-kama kigezo chetu, Bwana Mtume hakupata kumkaripia, wala
kumtolea maneno yenye kuumiza hisia zake au kumvunjia heshima. Huyu hapa
Anas mwenyewe anaelezea namna ulivyokuwa utumishi wake kwa Mtume wa Allah:
“Nilimtumikia Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-kwa kipindi cha
miaka kumi. Basi (katika kipindi chote hicho) hakupata
kuniambia japo ‘ah!’ au ‘kwa nini umefanya?’ au ‘kwa nini
hukufanya’. Muslim
Chini
ya kivuli cha hali hii ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-kuelekea watumishi wake. Tunagundua kosa baya kabisa
linalotendwa na wengi wetu leo. Ni ukweli uonekanao kwamba matajiri au
waajiri walio wengi leo hawawatendei vema watumishi/waajiriwa wao, hili li
bayana mbele ya macho ya kila mmoja wetu. Watumishi leo wanadharauliwa,
wananyanyaswa, wanapuuzwa, wanapunjwa na kudhulumiwa haki zao na pengine
hupigwa. Haya yanapingana na misingi ya sheria ya Uislamu. Katika hadithi
iliyopokelewa na swahaba Abuu Hurayrah-Allah amuwiye radhi-Mtume wa Allah-Rehema
na Amani zimshukie-amesema: “Inatosha (kabisa)
shari mtu kumdharau nduguye muislamu”.
Muslim
Imepokelewa
kutoka kwa Ibn Masoud-Allah amuwiye radhi-amesema: “Nilikuwa nikimpiga
bakora mtumwa wangu, nikasikia sauti nyuma yangu (ikisema): Tambua ewe Ibn
Masoud. Sikuweza kuitambua sauti ile kutokana na ghadhabu (niliyokuwa nayo).
Alipokurubia (mwenye sauti) tahamaki ni Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-naye akiniambia: “Tambua kwamba ewe Ibn
Masoud Allah ana uwezo zaidi juu yako kuliko uwezo ulio nao wewe juu ya
mtumwa huyu”. Nikasema
sitampiga tena mtumwa ye yote baada ya leo.
Katika
riwaya nyingine: “Bakora ile ilinianguka mkononi kutoka na khofu ya (maneno
yale ya) Mtume”. Na katika riwaya nyingine: “Nikasema: Ewe Mtume wa
Allah, nimemuacha huru kwa ajili ya Allah. Mtume akasema: “Ama
lau usingelifanya hivyo, ungeliunguzwa na moto (wa Allah)”. Muslim
|