Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Akhlaaq-Tabia  

"Hakika si vingine nimetumwa kuja kutimiza TABIA NJEMA" Hadith Tukufu

7. HAKI ZA VIONGOZI NA HAKI ZA RAIA                                                               Inaendelea

 Faida

2- WAJIBU WA RAIA/HAKI ZA VIONGOZI.

Utakapofungamana uongozi kwa mtu ambaye waislamu wamemridhia kwa nafsi zao, dini na dunia yao. Atakuwa tayari ana dhima na wajibu ambao ni haki ya Allah na haki ya uma (raia) wake. Sasa basi ili aweze kuutekeleza wajibu wake huu ipasavyo na kwa ukamilifu, Uislamu umempa haki kadhaa juu ya raia wake. Haki hizi zimsaidie katika kumtumikia Allah na uma wake. Miongoni mwa haki hizi za kiongozi katika Uislamu ni kama zifuatavyo:-

KUSIKILIZWA NA KUTIIWA:

Miongoni mwa haki za kiongozi ambazo ni wajibu wa uma (raia) kumtekelezea kama mtumishi wao ni kumsikiliza na kumtii katika hali zote maadam hakuamrisha maasi. Haki hii anapewa na mwenyewe Allah, hebu na tuitegee siko Qur-ani Tukufu: “ENYI MLIOAMINI! MTIINI ALLAH NA MTIINI MTUME NA WENYE MAMLAKA JUU YENU (viongozi) WALIO KATIKA NYIE (waislamu wenzenu)...” [4:59]

Hii ni nukuu ya Qur-ani inayowafaradhishia waumini kwanza kumtii Allah Mola Muumba wao na kadhalika kumtii Mtume wake. Na muislamu anapaswa kutambua kwamba kumtii Mtume ni kumtii Allah aliyemtuma kutuletea sheria hii: “MWENYE KUMTII MTUME AMEMTII ALLAH (kwani anayoyaamrisha Mtume yametoka kwa Allah)...” [4:80]

Na suna ya Mtume ni sehemu ya sheria ya Allah (sheria mama), kazi yake ni kubainisha mujmali (ujumla) wa sheria mama. Kwa mantiki hii suna ya Mtume inakuwa ni sheria shereheshi. Baada ya aya kuwaamrisha waumini kumtii Allah daraja la kwanza, kumtii Mtume wa Allah daraja la pili, ndipo ikawaamrisha kumtii kiongozi daraja la tatu. Utaratibu huu wa twaa unaonyesha kuwa twaa ya kiongozi inaiandamia twaa ya Mtume ambayo nayo inaiandamia twaa ya Allah Mola Mwenyezi. Kwa utaratibu huu ni muhali kumtii Mtume bila ya kumtii kiongozi na hivyo hivyo ni muhali kumtii Allah bila ya kumtii Mtume wake. Kadhalika utaratibu huu unafahamisha kuwa raia hawawajibiki kumtii kiongozi wao mpaka kwanza naye awe anamtii Allah na Mtume wake sambamba na kusimamisha sheria ya Allah. Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-anasema kuhusiana na haki hii ya kiongozi: “Sikilizeni na kumtii hata kama atakutawalieni (mambo yenu) mtumwa wa kihabeshi mwenye kichwa mithili ya zabibu”. Bukhaariy. Akasema tena: “Ni juu ya mtu muislamu kusikiza na kumtii (kiongozi) katika alipendalo na alichukialo maadam hakuamrishwa maasi. Ikiwa ataamrishwa maasi, basi (hapo) hakuna kusikiliza wala kutii”. Bukhaariy & Muslim.

Uislamu siku zote unapupia mshikamno na umoja wa uma na kuepusha njia za migongano na fitna. Kwa kulizingatia na kulichunga hili, Uislamu umewatahadharisha na kuwaonya waislamu dhidi ya kujitoa katika twaa ya kiongozi na kumuasi. Eti kwa sababu tu ya maasi na ufasiki unaotendwa na kiongozi huyo kama binadamu mwingine ye yote. Si haki kumuasi muda wa kuwa hajatenda ukafiri wa waziwazi kabisa. Isieleweke kuwa Uislamu unamlea na kumlinda kiongozi fasiki, la hasha. Uislamu unaangalia uzito na athari ya mambo mawili haya kwa jamii; uasi/ufasiki wa kiongozi na fitna/shari ya kumuasi kiongozi fasiki. Uislamu ukaona kuwa fitna/athari ya ufasiki wa kiongozi kwa jamii si kubwa zaidi kuliko athari ya kumuasi kiongozi huyo. Fitna hii ya kujitoa katika twaa ya kiongozi ni shari yenye kuendelea, kwani itaugawa uma katika matapo (makundi) mawili. Tapo la kiongozi fasiki mwenye dola (nguvu) na tapo la hawa raia waliojitoa wasio na nguvu za kuwahami dhidi ya nguvu za dola watakazoshushiwa na kiongozi fasiki ili kuwarejesha katika twaa yake na kukomesha uasi wao kwake. Katika hali hii ya mgawanyiko ni lazima patazuka vita ya wenyewe kwa wenyewe vitakavyozichukua muhanga roho za watu wengi wasio na hatia. Kwa kulichelea hili ndio Uislamu ukautaka uma kusubiri na kustahamili juu ya ufasiki huu wa kiongozi wao huku ukiitumia haki yao ya kumuelekeza na kumnasihi kwa utaratibu wa kiislamu. Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-anatuambia: “Atakayeung’oa mkono katika twaa (ya kiongozi), atakutana na Allah na ilhali hana hoja. Na atakayekufa na ilhali hana shingoni mwake kiapo cha utii (kwa kiongozi) atakufa mauti ya kijahilia”. Muslim. Akazidi kutuambia: “Atakayelichukia kwa kiongozi wake jambo/tabia fulani, basi na asubiri. Kwani atakayejitoa katika twaa ya kiongozi kwa (kiasi cha) shubiri moja (tu), atakufa mauti ya kijahilia”. Bukhaariy & Muslim. Mukhtasari wa kauli, hakumuhalalikii muislamu ye yote kumuasi kiongozi aliye muislamu mwenziwe kwa kisingizio cha uasi/ufasiki wa kiongozi huyo. Ni wajibu wake kuendelea kumtii pamoja na uasi wake huo maadam uasi huo haujafikia kiwango cha kufuru ya wazi isiyo na tafsiri nyingine ila kufru tu.

 

KUMSAIDIA NA KUSIMAMA NAE KATIKA JIHADI:

Ni wajibu wa raia (uma) kumuunga mkono na kumsaidia kiongozi wao katika kuwatumikia. Na hii ni haki inayokwenda sambamba na haki ile ya twaa. Kila atakalolifaradhisha au kuliamrisha kiongozi ndani ya mipaka ya sheria kwa maslahi ya uma, dini ya Allah na kulinda heshima ya waislamu na dini yao. Ni wajibu wa kila muislamu (raia) kuitekeleza amri hiyo ya kiongozi wake hata kama itagharimu uhai wake. Hili linatokana na ukweli kwamba kiongozi kama binadamu hawezi kubeba dhima hii kuu ya kuutumikia uma mpaka raia wasimame upande wake na kumsaidia kwa mali na nafsi zao. Kiongozi akitangaza jihadi dhidi ya maadui wa Uislamu, jihadi hii haitasimama ila kwa msaada na uungaji mkono wa raia. Kama tulivyotangulia kueleza kuwa haki ya msaada na kusimama na kiongozi katika jihadi inaandamana na haki ya twaa. Kadhi Abuu Ya’alaa-Allah amrehemu-anasema: “Imamu (kiongozi) atapotekeleza haki za uma (raia), zitamuwajibikia yeye juu yao (raia) haki mbili: (Haki ya) twaa na (haki ya) msaada (kuungwa mkono), muda wa kuwa halipatikani upande wake jambo litakalomtoa katika amana/uaminifu”.

 

TOSHA YA MAISHA YAKE:

Kiongozi wa kiislamu huutumia muda wake mwingi pengine hata ule wa mapumziko binafsi katika kuhakikisha kuwa anayatekeleza vema na ipasavyo majukumu yake kama mtumishi wa uma. Huutumia muda wake huu kwa ajili ya maslahi na manufaa ya uma wake. Kwa kuuzingatia ukweli huu na kuuthamini mchango huu wa kiongozi, Uislamu unampa haki ya kuchukua tosha ya maisha yake katika mali ya waislamu. Kiasi anachoruhusiwa kuchukua ni kile kinachoweza kukidhi mahitaji yake na familia yake kwa wema bila ya ubadhirifu. Zama alipotawazwa Sayyidna Abuu bakri-Allah amuwiye radhi-kuwa Amirul-Muuminina kushika nafasi iliyoachwa wazi kwa kufariki kwa Bwana Mtume, maswahaba wa Mtume wakaambizana: Mkadirieni khalifa wa Mtume kitakachomkwasia (kitakachomtoshelaza) Wakasema: Naam, nguo mbili atakapozichakaza atazivua na kuchukua nyingine mithili ya hizo. Kipando (usafiri) anapotaka kusafiri na matumizi ya nyumbani kwake (outlay) kama alivyokuwa akitumia kabla ya kutawazwa khalifa. Abuu bakri akasema: Nimeridhia.

Yatizame haya katika “TWABAQAAT” ya Ibn Sa’ad juzuu ya tatu, sahifa 184 na 185. Kadhalika amepokea Ibn Sa’ad kutoka kwa Bi. Aysha-Allah amuwiye radhi-amesema: Alipotawazwa Abuu Bakri alisema: Kaumu yangu inatambua fika kwamba kazi yangu haikushindwa kuilisha familia yangu. Na hivi sasa nimeshughulika na mambo ya waislamu na nitachuma katika mali yao na familia ya Abuu Bakri itakula kutokana na mali hiyo. (Twabaqaat).

Na wakati alipotawalia ukhalifa Sayyidna Umar Ibn Al-Khatwaab-Allah amuwiye radhi-waliulizana baadhi ya maswahaba waliokuwa katika baraza ya Umar kuhusiana na kinachomuhalalikia katika mali ya Allah. Umar akawaambia: Mimi nitakuelezeni kinachonihalalikia katika mali hiyo. Zinanihalalikia nguo mbili; nguo ya kiangazi (joto) na nguo ya kipindi cha baridi. Mnyama wa kuendea Hijjah na Umrah, chakula changu na familia yangu kama chakula cha mtu wa kawaida katika Makurayshi ambaye si tajiri wala fakiri wao. Kisha mimi nichukuliwe kama ye yote miongoni mwa waislamu, yananifika yanayowafika.

Riwaya hizi za tarekh na mithili ya hizi zinafahamisha kuwa kiongozi (Amirul-Muuminina) ana haki katika Baytul-Maali (khazina) ya waislamu. Achukue/apewe katika mali hiyo kadri ya haja yake na familia yake ili asishughulike na kazi nyingine itakayomfanya ashindwe kutimiza majukumu kama kiongozi na mtumishi wa uma.

 


TUJIFUNZE NA TUKUBALI: kuwa waislamu: “...WANASHAURIANA KATIKA MAMBO YAO...” [42:38]

Bwana Mtume anaagizwa: “...NA USHAURIANE NAO KATIKA MAMBO...” [3:159]


Forum | Guestbook | Tuandikie |