Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Akhlaaq-Tabia  

"Hakika si vingine nimetumwa kuja kutimiza TABIA NJEMA" Hadith Tukufu

7. HAKI ZA VIONGOZI NA HAKI ZA RAIA                                                               Inaendelea

 Faida

WAJIBU WA KIONGOZI/HAKI ZA RAIA.

IV/. KUGAWA MADARAKA KWA KUWATEUA VIONGOZI WA CHINI YAKE.

Kiongozi mkuu ndiye mwenye dhima na jukumu la kuongoza serikali sambamba na kupanga mipango endelevu ya jamii (raia). Ana wajibu mkuu wa kuhakikisha kuwa mipango na taratibu hizo zinahamishwa kutoka maandishini na kutiwa katika ulimwengu wa matendo kwa maslahi na manufaa ya jamii yake. Ni jukumu lake kuutumikia uma wake kwa uadilifu. Kutokana na ukubwa, uzito na ugumu wa majukumu haya ya kiongozi kama mtumishi mkuu wa uma, ni dhahiri kuwa hataweza kulibeba furushi hili la majukumu peke. Kutokana na ukweli huo usiokanushika ni haki ya msingi ya raia wake na ni wajibu wake wa lazima kuwateulia watu miongoni mwao watakaomsaidia katika majukumu ya utawala. Hii ndio njia aliyoitumia Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-wakati wa ustawi (kupanuka) wa dola ya Kiislamu zama za uhai wake. Ukizifungua kurasa za tarekh (history) hutoshindwa kuona kuwa Bwana Mtume aliwateua kwa vipindi maalumu mabwana Aliy Ibn Abuu Twaalib na Muaadh Ibn Jabal-Allah awawiye radhi-kuwa makhalifa wake katika nchi ya Yemen. Kama alivyomteua Abuu Musa na maswahaba wengine-Allah awawiye radhi-kuwa makadhi baadhi yao na wengine kuwa magavana na walinganiaji dini sehemu mbalimbali za ulimwengu ule wa Kiislamu. Bwana Mtume alipomteua mmojawapo wa maswahaba wake kuwa kiongozi wa uma katika ngazi fulani, hakumuachia kuongoza kwa maoni na matashi yake binafsi. Bali alimpa muongozo kamili wa kufuata katika kazi yake hiyo, sambamba na miiko na mipaka ya kazi. Na zaidi ya yote hayo alimuusia kumcha Allah na kuwa muadilifu katika kazi yake hiyo. Katika uteuzi huu wa viongozi (makhalifa) wa chini yake, Bwana Mtume alitumia vigezo maalumu. Aliangalia uaminifu, uwezo wa kazi (utawala), ucha-Mungu na baki ya sifa nyingine njema. Hakumteua katu mtu ajizi, dhaifu wala mwenye pupa ya kupata uongozi ili awe bwana mkubwa (muheshimiwa). Swahaba Abuu Dhari alimuomba Bwana Mtume-Rehema na Amani zimshukie-kumpa nafasi ya uongozi. Mtume akamwambia: “Wewe ni dhaifu (huuwezi uongozi) nao (huo uongozi) ni amana na siku ya kiyama ni fedheha na majuto. Ila kwa atakayeutwaa kwa haki yake na akayatekeleza yanayompasa katika huo uongozi”. Muslim

Utaratibu huu wa uteuzi ulirithiwa pia na makhalifa wa Mtume baada ya kufa kwake, na inatakikana urithiwe pia na viongozi wetu wakuu wa leo kwa maslahi ya uma.

 

V/. JIHADI KATIKA DINI YA ALLAH NA ULINZI (HIMAYA) WA DOLA.

Allah Mola Mwenyezi amemleta Mtume wake Muhammad-Rehema na Amani zimshukie-kwa watu wote: “NA HATUKUKUTUMA (hatukukuleta) ILA KWA WATU WOTE, UWE MTOAJI WA KHABARI NZURI NA MUONYAJI...” [34:28]

Kwa kauli na tangazo hili la Allah, Bwana Mtume akabeba amana hii ya kuwa mjumbe wa Allah kwa ulimwengu mzima. Akaitekeleza haki ya amana hii kwa kuufikisha ujumbe wa Allah kwa walimwengu wote kwa kipindi kisichotindika miaka kumi na tatu. Hapo ndipo akatunukiwa shahada ya ustahiki iliyopigwa muhuri wa kukamilisha na kukhitimisha kazi kwa kauli yake Allah: “...LEO NIMEKUKAMILISHIENI DINI YENU NA KUKUTIMIZIENI NEEMA YANGU NA NIMEKUPENDELEENI UISLAMU UWE DINI YENU...” [5:3] Kutokana na vikwazo alivyokumbana navyo katika kuitekeleza kazi hii ya Mola wake, wakati mwingine kulimlazimu Mtume kujitoa muhanga kwa mali na nafsi yake ili kuipigania dini ya Allah. Akapanga katika uhai wake mikakati ya kuwaandaa maswahaba wake kuchukua na kuiendeleza kazi aliyoianza. Baada ya kufa Mtume, maswahaba-Allah awaridhie-wakaibeba mabegani mwao bendera ya da’awah na kuufikisha Uislamu kule usikofika bado. Wakashika hatamu za kuwaongoza watu katika mfumo sahihi wa maisha uliofumwa na Mola wao (Uislamu), mpaka sheria ya Allah ikatawala zaidi ya robo tatu ya dunia. Elewa na ufahamu ewe ndugu muislamu khususan kiongozi, kuwa jihadi hii ya kuipigania dini ya Allah iliyoasisiwa na mtume wako na kuendelezwa na maswahaba wake watukufu. Jihadi hii inaendelea muda wa kuwepo/kupatikana sababu zinazoiwajibisha mpaka kutoweka kwa mbingu, ardhi na vyote vilivyomo (kiyama). Jihadi hii ni kwa ajili ya kulinda, kutetea na kuchunga heshima, uhai, mali na haki ya waislamu kama jamii. Sambamba na haki yao ya kuabudu kwa mujibu wa mafundisho ya Uislamu na kuutangaza Uislamu ulimwenguni kote bila ya kizuizi cha aina yo yote ile. Nafasi ya Mtume katika kuuongoza uma katika jihadi unayo wewe ambaye ndio kiongozi wa waislamu leo. Hii ni dhima isiyoepukika iliyo shingoni mwako, ni wajibu wako bali ni sehemu ya dini khasa kuwaongoza raia wako katika jihadi iwapo hali na mazingira yanalazimisha hivyo. Na kunawawajibikia raia wako wote wenye kumuamini Allah na siku ya mwisho kukutii katika hilo.

 

VI/. USIMAMIZI, UENDELEZAJI NA ULINZI WA RASILIMALI YA DOLA NA KUHAKIKISHA MGAWANYO ADILIFU WA MALI HIZO MIONGONI MWA RAIA.

Mali ndio kano (mshipa) na zana ya maisha haya na pengine ndio sababu ya mafanikio ya maisha ya ulimwengu huu na ule ujao (akhera). Mali pia ni mojawapo ya nguzo za nguvu inayoamrishwa katika kauli tukufu ya Allah: “BASI WAANDALIENI (wawakeeni tayari) NGUVU MZIWEZAZO (silaha) NA MAFARASI (vifaru, madege, manowari) TAYARI TAYARI (mipakani). ILI KWAZO (nguvu hizi) MUWAOGOPESHE MAADUI WA ALLAH NA MAADUI WENU...” [8:60] Kadhalika mali ni uti wa mgongo wa maisha ya uma, kwa ukweli huu ni haki ya msingi ya raia na ni wajibu wa kiongozi kuwaratibia raia wake mipango mizuri ya kiuchumi. Mipango itakayowashirikisha katika kuendeleza rasilimali za dola na kunufaika nazo katika nyanja za maisha yote ya kijamii. Mipango itakayowahakikishia kupata mahitaji yao ya msingi kwa njia halali na rahisi. Ni wajibu wa kiongozi kuanzisha ‘Baytul-Maali’-(Public Treasury) itakayokuwa na vyanzo vya mapato ili iweze kujitegema katika kutoa huduma kwa uma. Kiongozi atakuwa na wajibu wa kusimamia mapato na matumizi ya Baytul-Maali moja kwa moja au kupitia kwa atakayemteua kwa kazi hiyo. Miongoni mwa haki za raia kwa kiongozi wao ni kupata mgawanyo sawa wa rasilimali za dola na huduma sawa za kijamii bila ya upendeleo wa mahala fulani kwa sababu tu ndiko anakotoka kiongozi huyo. Ahakikishe kuwa mali ya uma haihujumiwi na na kuibiwa na watu wa nje. Wanawazuoni wa kale na hawa wa sasa-Allah awarehemu-wameandika mengi katika ukumbi huu wa kisiasa khususan katika jukwaa hili la uongozi. Sheikh Al-Maawardiy-Allah amrehemu-ni mmoja wa wanazuoni walioshika kalamu katika fani hii na kueleza kwa ufafanuzi wa kina. Yeye ameukusanya wajibu wa kiongozi katika vifungu kumi, kama ifuatavyo:-

KULINDA MISINGI YA DINI:

Ni wajibu wa kiongozi kulinda misingi ya dini na Ijmaa ya salafu. Akitokeza mzuzi (mzushi) au mpinzani wa misingi hiyo, ni wajibu wake yeye mwenyewe au kupitia mteule wake kumuwekea wazi mzuzi huyo hoja na kumbainishia ilivyo ndivyo. Ayafanye yote haya ili kuilinda dini dhidi ya kombokombo na kuulinda uma na mgawanyiko usio wa lazima.

 

KUSIMAMIA UTEKELEZAJI WA SHERIA:

Kunamlazimu kiongozi kama mtumishi wa uma kuhakikisha kuwa sheria ya Allah ndio inayotumika katika kuwahukumu mahasimu wawili na kukata magomvi baina ya wagombanao. Ni wajibu wake kuhakikisha kuwa sheria inampa haki kila aistahikie mpaka mwenye nguvu asiweze kumuonea mnyonge kwa sababu tu ya nguvu zake.

KUIMARISHA NGUVU ZA DOLA:

Ni wajibu wakiongozi kuunda serikali imara na yenye nguvu itakayowahakikishia raia wake amani, salama na utulivu. Vitu ambavyo vitawawezesha kuendesha shughuli zao za kimaisha kwa uhuru na bila ya khofu wala bughudha. Watu waweze kusafiri wakiwa hawana khofu juu ya nafsi au mali zao.

 

KUWEKA MIPAKA:

Aweke mipaka itakayochunga maharamisho ya Allah yasitendwe na kulinda haki za waja wake zisivunjwe.

KUWEKA ULINZI IMARA KATIKA MIPAKA YA NCHI:

Kunampasa kuhakikisha kuwa kuna ulinzi wa kutosha na imara kuzunguka mipaka yote ya nchi. Ili kuilinda nchi dhidi ya uvamizi wa ghafla kutoka kwa maadui wa nje.

JIHADI DHIDI YA MPINZANI WA UISLAMU:

Kiongozi ana wajibu wa kumpiga vita mtu uliomfikia ujumbe wa Uislamu na akaupinga bila ya kuwa na hoja yenye kuzingatiwa. Ampige vita mpaka ima aukubali Uislamu (asilimu) au awe chini ya dhima ya Uislamu (awe Dhimiyu).

 

KUSIMAMIA MATUMIZI YA FEI NA SADAKA/ZAKAH KWA MUJIBU WA SHERIA:

Fei ni ile mali inayopatikana bila ya vita baada ya maadui kukimbia, mali hii na ile itokanayo na sadaka/zakah ni dhima na amana iliyo mikononi mwa kiongozi. Kwa hivyo basi ni jukumu lake kuhakikisha kuwa mali hiyo inatumika kwa namna ilivyoagizwa na sheria.

MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI:

Kiongozi anapaswa kukadiria mapato na matumizi ya Baytul-Maali na kutoa kasimu (fungu) panapostahiki kwa wakati muafaka bila ya ubadhirifu au kuchelewa.

KUTEUA WATU STAHIKI WAAMINIFU NA WENYE SIFA STAHIKI KUENDESHA MAMBO:

Kunamuwajikia kiongozi kuwateua watu watakaomsaidia katika kuendesha shughuli mbalimbali za kiutawala. Vigezo vya uteuzi huo viwe ni uaminifu na sifa stahiki kwa kazi husika ili huduma za kijamii ziendeshwe vema na mali ya uma iwe katika udhibiti wa watu waaminifu.

KUONGOZA NA KUSIMAMIA IDARA ZOTE ZA UTAWALA:

Kiongozi anawajibika kutoa muongozo wa uendeshaji wa shughuli za utawala katika idara/wizara mbalimbali za serikali yake. Na kusimamia na kufuatilia kwa karibu utendaji wa watendaji aliowateua kushika nyadhifa hizo.

Ili kuyaona haya na mengi mengineyo yahusuyo mambo ya utawala na sheria, rejea kitabu “AL-AHKAAMUS-SULTWAANIYYAH” cha Al-Maawardiy.

 

 


TUJIFUNZE NA TUKUBALI: kuwa waislamu: “...WANASHAURIANA KATIKA MAMBO YAO...” [42:38]

Bwana Mtume anaagizwa: “...NA USHAURIANE NAO KATIKA MAMBO...” [3:159]


Forum | Guestbook | Tuandikie |