4).
Kuonewa/kuliliwa wivu.
Ni haki ya
mke na ni wajibu wa mume kisheria kumuonea wivu wa kisheria mkewe. Mume
awe na wivu kwa mkewe, wivu utakaokuwa wigo wa kulinda na kuhifadhi utu,
cheo, nafasi na utukufu wa mkewe. Mume anatakiwa asighafilike na kutoa
mwanya ambao unaweza kuwa ni sababu ya fisadi itakayopelekea kulegalega
au pengine kuvunjika kwa ndoa yao. Naam, ni kweli mume anatakiwa kuwa na
wivu kwa mkewe, lakini si haki wala sheria kupindukia katika wivu. Wivu
utakaomtumbukiza katika lindi la dhana mbaya dhidi ya mkewe. Dhana hizi
zikamgeuza kuwa kachero na jasusi wa kuchunguza nyendo na pengine mambo
ya ndani kabisa ya mkewe. Huku si kuutekeleza wajibu wako kwa mkeo, wala
huambiwi kuwa ndio unampenda sana mkeo. Wivu huu wa kupindukia ni
ugonjwa unaoweza kuondosha masikilizano na maelewano ndani ya nyumba. Na
mahala pake kutawaliwa na mizozo na gubu lisilokwisha. Pengine wivu wa
namna hii unaweza kuwa kichocheo na kumuamshia mke ari ya kufanya uchafu
anaoshukiwa kuufanya na kumbe masikini hana khabari nao kabisa. Ni kwa
kuyazingatia madhara haya na kama haya ndio tunamuona Bwana Mtume-Rehema
na Amani zimshukie-akiuukataza wivu huu wa kupindukia. Makatazo hayo
yamekuja katika hadithi sahihi iliyopokelewa na swahaba Jaabir-Allah
amuwiye radhi: “Kwamba Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-amekataza mwanamume kumgongea mlango mkewe wakati wa usiku.
Akimdhania kufanya khiyana au (kwa lengo la) kutafuta kunguwao (makosa
ya kuteleza) zao.” Muslim
5). Mahitaji
ya lazima.
Ni katika
jumla ya haki za mke zilizo katika dhima ya mumewe kupata mahitaji yake
yote ya lazima. Mume anawajibika kutoa gharama zote za mahitaji ya lazima
ya mkewe, ikiwa ni pamoja na chakula bora cha kulinda, kujenga na kutia
mwili nguvu. Ni wajibu wa mume kuhakikisha kuwa mkewe anapata maji safi na
salama ya kunywa. Ampatie mavazi yatakayomfaa katika vipindi/majira yote
ya mwaka; nguo za masika na kiangazi. Ni haki ya mke kupatiwa maskani
yatakayomsitiri na kumpa amani na usalama wa nafsi, mali na akili.
Kadhalika ni wajibu wa mume kumpa matibabu mkewe anapougua na kushirikiana
nae kwa kumliwaza katika kipindi kigumu cha maradhi au ujauzito. Haya yote
yamo katika agizo tukufu la Allah Mtukufu: “...NA NI JUU YA BABA (yake)
CHAKULA CHAO (hao watoto na mama) NA NGUO ZAO KWA SHARIA. WALA
HAIKALIFISHWI NAFSI YO YOTE ILA KWA KADRI YA WASAA WAKE...” [2:223]
Nae Bwana
mtume-Rehema na Amani zimshukie-amesema katika kuuonyesha wajibu huu wa
mume ambao kwa mkewe ni haki: “Wana (hao wanawake) juu yenu (haki ya)
chakula chao na nguo zao kwa wema (sharia)”. Tirmidhiy
Siku moja Bwana
Mtume-Rehema na Amani zimshukie-aliulizwa ni ipi haki ya mke wa mmoja wetu
juu yake, akasema: “Ni kumlisha utakapokula na kumvisha utakapovaa. Na
wala usiupige uso (wake), wala usimtolee maneno machafu na wala usimuhame
ila ndani ya nyumba (yenu)”. Ahmad,
Abuu Daawoud & Ibn Maajah.
Allah akurehemu
ewe mume ikiwa utajua kwamba juhudi na uchovu wako katika kuhangaika
kumpatia mkeo mahiataji yake haya. Hazipotei bure bali Allah anakulipa
thawabu na ujira mkubwa. Imekuja katika hadithi ya Sa’ad Ibn Abiy
Waqaasw-Allah amuwiye radhi-kwamba Mtume wa Allah-Rehema na Amani
zimshukie-alimwambia: “Na hakika wewe hutotoa matumizi/gharama zo zote
ukiikusudia dhati ya Allah ila utalipwa kwayo (gharama hizo). Hata
(gharama za) kile unachokitia katika kinywa cha mkeo (yaani chakula)”.
Bukhaariy & Muslim
6). Mahari.
Ni haki ya mke na
ni wajibu wa mume kwa mujibu wa sheria kumpa mke mahari yake kamili. Kwa
kuwa hiyo ni haki yake aliyopewa na Allah Mola Muumba wake. Tusome na
tukubali: “NA WAPENI WANAWAKE MAHARI YAO, HALI YA KUWA NI HADIYA
(aliyowapa Allah). (Lakini hao wake zenu) WAKIKUPENI KWA RADHI YA NAFSI
ZAO KITU KATIKA HAYO (mahari) BASI KULENI KWA FURAHA NA KUNUFAIKA”.
[4:4]
Mahari ni haki ya
mke hata kama ulimpa nyumba, gari, shamba na...na....kuwa ndio mahari
yake. Ukimtaliki na kuoa mke mwingine huna rukhsa kuchukua cho chote
katika hiyo mali uliyompa. Hebu tuitegee pamoja sikio la usikivu na
uzingativu kauli hii tukufu ya Allah: “NA KAMA MKITAKA KUBADILISHA MKE
MAHALA PA MKE (yaani kumuoa mke mwingine na kumuacha huyo wa zamani), NA
HALI MMOJA WAO (naye ndio huyo unayemuacha) MMEMPA MRUNDI WA MALI, BASI
,MSICHUKUE CHO CHOTE. JE, MNACHUKUA KWA DHULMA NA KWA KHATIA ILIYO WAZI?
NA MTACHUKUAJE, NA HALI NYINYI KWA NYINYI MMEINGILIANA?...” [4: 20-21]
7). Uadilifu
baina ya wake wenza.
Ni haki ya wake
wenza na ni wajibu wa mume kuwafanyia uadilifu wakeze hawa katika haki na
mahitaji yao ya lazima. Awalinganishe sawa katika matumizi, malazi, zamu
za kulala na kila ambacho kinamkinika kugawika. Ni vema mume akakumbuka
kuwa kumpendelea mmoja wa wakeze na kumili (kuelemea) zaidi kwake ni
miongoni mwa madhambi makubwa. Bwana Mtume-Rehema na Amani
zimshukie-anatutahadharisha na dhambi hii, aliposema: “Atakayekuwa na
wake wawili akamili kwa mmoja wao, atakuja (atafufuliwa) siku ya kiyama na
ilhali bega (upande) lake moja limeshuka”. Ahmad
& Ahli Sunan.
Ama yale mambo
yasiyokubali kugawika kama vile mapenzi na raha ya nafsi. Haya hayamo
katika uweza wa mwanadamu, kwa hivyo hana dhambi kwa hilo maadam yale
yanayogawika anayatekeleza kwa usawa. Ukweli wa hili umo katika kauli ya
Allah, tuisome sote: “NANYI HAMUWEZI KUFANYA UADILIFU (kweli kweli)
BAINA YA WAKE, IJAPOKUWA MTATAKA KUFANYA HIVYO. KWA HIVYO MSIELEKEE
(upande mmoja) KABISA KABISA; MSIJE KUMUACHA (huyo mwingine msiyempenda)
KAMA ALIYEANGIKWA (hajijui kuwa ana mume au mjane)...” [4:129]
Alikuwa Mtume wa
Allah-Rehema na Amani zimshukie-akigawa siku sawa baina ya wakeze na
akisema: Ewe Mola wa haki, hii ndio sehemu/fungu langu katika kile
nikimilikicho. Basi usinilaumu katika kile ukimilikicho wewe na wala mimi
sikimiliki”. Abuu Daawoud,
Tirmidhiy, Nasaai & Ibn Maajah.
Lakini lau mume
atampendelea mmoja wa wake zake katika zamu ya kulala, akampa siku nyingi
zaidi kuliko mwenziwe. Lakini akafanya hivyo kwa radhi yake mwenyewe (huyo
mwenziwe) hakuna ubaya. Kwani hivyo ni kama alivyokuwa akifanya Bwana
Mtume, alikuwa akimpa Bi. Aysha siku yake na siku ya Bi. Saudah-Allah
awawiye radhi- ambayo mwenyewe Bi. Saudah alimpa hadiya (mke mwenziwe) Bi.
Aysha. Hivi ndivyo ilivyokuja katika riwaya ya Bukhaariy na Muslim.
Bwana
Mtume-Rehema na Amani zimshukie-kwa kuchunga uadilifu baina ya wakeze
katika zamu zao za kulala. Alikuwa akiuliza wakati akiwa ni mgonjwa
kitandani kwa maradhi yaliyokuwa sababu ya kifo chake, akisema: Kesho niko
wapi (ni zamu ya nani), kesho niko wapi mimi. Wakeze wakampa idhini
augulie po pote apatakapo, nae akakhitari kuwa katika nyumba ya Bi. Aysha,
akaugulia hapo mpaka akafa. Huu ni upokezi wa Bukhaariy na Muslim.
8). Haki ya
kupata elimu.
Mke ana haki
ya kupata elimu ambayo ni wajibu wa mumewe kuhakikisha kuwa anaipata.
Ikiwa mke hakupata elimu ya msingi ya dini yake huko kwao atokako, basi ni
jukumu la mume kuhakikisha kuwa mkewe anapata elimu hiyo muhimu.
Amfundishe yeye mwenyewe au amtafutie mtu/mahala ambapo ataipata elimu
hiyo. Aanze kufundishwa mambo ya msingi kama vile nguzo za imani na baki
ya mambo mengine yanayohusiana na akida (itikadi). Kisha afundishwe hukumu
za mambo ya kisheria yanayomtokea katika maisha yake ya kila siku. Yaani
hukumu za twahara, hedhi, swala, swaumu na kadhalika. Pia si vibaya
akipata elimu na taaluma ya ziada itakayoisadia familia kujikimu kimaisha,
taaluma itakayomuwezesha kufanya kazi na kuchangia kuongeza pato la
familia. Afanye kazi kwa ridhaa ya mumewe na chini ya mazingira
yanayokubaliwa na sheria. Kumbuka mama (mke) ni shule ya familia,
kumuelimisha mama ni kuielimisha familia.
Kadhalika ni
jukumu na wajibu wa mume kumuhimiza mkewe swala na mambo mengine ya kheri,
hii ni amri ya Allah tuamrike: “NA WAAMRISHE WATU WAKO (familia yako)
KUSWALI NA UENDELEE MWENYEWE KWA HAYO...” [20:132]
Ni vema mume
akakumbuka kuwa familia aliyonayo ni amana na dhima iliyo shingoni mwake.
Yeye ni mchunga na anawajibika kwa familia yake na atakwenda kuulizwa
mbele ya Allah aliichunga vipi familia yake. Kwa hivyo ni wajibu wa mume
(baba) kuhakikisha kuwa anakuwa kiwanda cha kuzalisha familia njema ya
kiislamu ili hatimaye tuwe na jamii njema ya kiislamu. Familia itakayoishi
katika maadili, mila, utamaduni na sheria ya Allah: “ENYI MLIOAMINI!
JIOKOENI NAFSI ZENU NA WATU WENU NA MOTO AMBAO KUNI ZAKE NI WATU NA
MAWE...” [66:6]
Ni dhahiri kuwa
hatuwezi kujiokoa sisi na kuziokoa familia zetu kutokana na adhabu kali ya
moto kama hatukuandaa mazingira mema tangu mapema. Mazingira
yatakayopelekea kuishi chini ya twaa ya Allah na Mtume wake kwa kufuata
muongozo wa Qur-ani Tukufu.
9). Heshima na
kuthaminiwa.
Ni haki ya
mke na ni wajibu wa mume kumthamini na kumpa mkewe heshima zote
anazostahiki kama mke, mwandani na msaidizi wa karibu katika maisha kwa
mujibu wa sheria. Mume anatakiwa kumuangalia mkewe kama sehemu yake
inayomkamilisha na kumfanya mwanamume kamili atakayeitwa mume, baba na
hatimaye babu. Haya yote yanaonyesha nafasi ya mwanamke kwa mwanamume. Ni
nafasi yake hii ukiachilia mbali ubinadamu wake inayomstahikisha heshima
na kuthaminiwa sambamba na kutambuliwa utu wake. Mume asijione kuwa ana
haki na kila sababu ya kufanya atakavyo kwa mkewe, hii ni dhana lemavu
inayokwenda kinyume na mafundisho sahihi ya uislamu. Si haki na wala si
sheria mume kumdhalilisha mkewe kwa kumtukana na kumtolea maneno machafu
peke yao chumbani, seuze mbele ya watoto au watu kando. Si halali hata
kumuabisha kwa jambo la kweli kama hali duni ya nyumbani kwao. Haijuzu
kumtukania wazazi wake kwa sababu ya magomvi yenu ya ndani, haya si
matendo wala tabia za muislamu wa kweli.
Hizi ni baadhi tu
ya haki za mke kwa mujibu wa sheria, haki ambazo ni wajibu mume
amtekelezee.
|