Makala
Uislamu-Utangulizi
Fiqhi na Sheria 
Akhlaaq-Tabia
Sira ya Mtume
Nasaha za dini
Maswali na Majibu
Uliza Suala la dini
Jiunge na Mtandao !!!

 

Akhlaaq-Tabia  

"Hakika si vingine nimetumwa kuja kutimiza TABIA NJEMA" Hadith Tukufu

III) UONGO

 
Uongo au kusema uongo ni miongoni mwa tabia mbaya ambazo muumini wa kweli anapaswa kujiepusha nazo. Mwenyenyezi Mungu Mtukufu anatuambia:-

"WANAOZUA UWONGO NI WALE WASIOZIAMINI AYA ZA MWENYEZI MUNGU; NA HAO NDIO WAONGO" ?[16:105]

Kwa mujibu wa aya tabia ya kuzua uongo ni sifa waliyopambika nayo watu wasiyo waumini, muumini mkamilifu wa imani hawi muongo. Mtume wa Mwenyezi Mungu aliulizwa: muumini anaweza kuwa mwoga? Akajibu "Ndiyo(anaweza)" Akaulizwa(tena): anaweza kuwa bakhili (Muumini)? Akajibu: "Ndiyo." Akaulizwa (tena Muumini) anaweza kuwa muongo? Akajibu: Hapana Muumini hawi muongo."

Ikiwa Bwana Mtume anaikanusha Imani kwa mtu mwenye tabia ya kusema uwongo, huo uwongo basi ni nini? Wanazuoni wanasema: Uongo ni kueleza jambo au kitu kinyume na vile kilivyo kwa kujua au kutokujua, kwa makusudi au bila ya kukusudia. Bwana Mtume anasema: "Atakayemwambia mtoto mdogo njoo uchukue (akaja) na asimpe (kitu) huo ni uongo." Ahmad

Kwa nini mtu anasema uongo.? Nini sababu ya kusema uongo.? Tabia hii ni mbaya inatokana na maumbile ya mwanadamu ya kutaka kujivutia manufaa na kujiondoshea madhara kwa hali na gharama yoyote ile. Mwanadamu anaweza kuona kusema uongo ndiko kutakakomvua na kumuepusha na janga linalomkabili kama vile kufungwa jela au kufukuzwa kazi, hapo husema uwongo ili asalimike, pia hulazimika kusema uongo anapoona kusema ukweli kutamletea madhara kama vile kutoa ushahidi dhidi ya mzazi wake, ushahidi utakaopelekea ahukumiwe kifo, hapo husema uongo bila ya kujali kauli ya Bwana Mtume alipotuambia:

"Jilazimisheni (kusema) ukweli kwani ukweli humuongoza(mtu) katika wema na bila shaka wema humuongozea (mtu)katika uovu, na uovu (nao) humuongozea motoni na mtu huandikwa mbele ya Mwenyezi Mungu muongo." Bukhaariy na Muslim

Tabia hii mbaya ya kusema uongo ina madhara mengi sana kwa mzuaji uongo na kwa jamii kwa ujumla. Muongo akibainika kwa kudhihiri ukweli, huaibika na kudharauliwa na jamii, pia hupoteza uaminifu kwa watu na akhera anangojewa na adhabu kali. Mtu muongo pia husababisha chuki, uhasama na hata ugomvi baina ya watu. Ni kutokana na madhara haya na mengineyo ndio sababu Uislamu umeikemea vikali tabia hii mbaya.

iv) KUKAA NA WATU KWA WEMA

Ukiirejea historia utangudua kuwa kuishi vema na watu au ujirani mwema aliokuwa nao Bwana Mtume ulikuwa ni sababu ya kuwavuta watu kuingia katika dini ya Mwenyezi Mungu. Bwana Mtume atuatuambia.

"Mche Mwenyezi Mungu popote (pale) ulipo na ulifuatishie baya/ovu (ulilolitenda) jema litakalolifuata(baya) na kaa/ishi na watu kwa tabia njema." Tirmidhiy

Kuishi na watu kwa wema ni pamoja na :-

  1. Kuwa mkweli katika kauli na mtendo kwa wenzio
  2. Kuwa na bashasha mbele yao
  3. Kuwa na shukrani kwa wema wanaokutendea
  4. Kuwa wa kwanza kuwatolea salamu kila mkutanapo
  5. Waite kwa majina mazuri wayapendayo
  6. Wataje kwa wema
  7. Wasamehe waliokukosea
  8. Linda hadhi na heshima zzao
  9. Usizifichue siri zao walizokueleza
  10. Usijifakharishe mbele zao kwa hadhi, cheo au utajiri wako
  11. Shirikiana nao kwa hali na mali katika huzuni na furaha
  12. Usiwaudhi kwa kuwafanyia usilopenda wao kukufanyia
  13. Waheshimu wakubwa na wahurumie wadogo
  14. Wape nasaha/ushauri kwa maneno mazuri yaliyo laini unapowaona wamepotea
  15. Usiwabague watu kwa sababu ya utajiri au umasikini.

Ukiishi na watu kwa kuzingatia nasaha hizi, utapendwa na jamii na utaishi katika jamii kwa furaha na amani ya kweli . Bwana Mtume -Allah anamshushie Rehema na Amani - anatuambia:-

"Miongoni mwa tabia za mitume na watu wakweli ni bashasha waonanapo na kupeana mikono wakutanapo."



Forum | Guestbook | Tuandikie |